Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sanamu kwa Ajili ya Ibilisi Mwenyewe”

“Sanamu kwa Ajili ya Ibilisi Mwenyewe”

“Sanamu kwa Ajili ya Ibilisi Mwenyewe”

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

SANAMU isiyo ya kawaida imesimama jijini Madrid, Hispania. Mtazamaji wa kawaida hawezi kushangazwa na umbo la sanamu hiyo wala jina lake—“Malaika Aliyeasi.” Hata hivyo, ukiitazama kwa makini, utagundua kwamba hiyo ni sanamu iliyojengwa kwa ajili ya Shetani Ibilisi!

Mgeni anayetembelea Hispania ambayo ni nchi yenye Wakatoliki wengi angetazamia kuona sanamu za malaika au “watakatifu” fulani, bali si moja ambayo imechongwa kwa ajili ya mtawala wa roho waovu. Hata hivyo, Ricardo Bellver, mchongaji wa sanamu Mhispania wa karne ya 19, aliamua kutofuata desturi. Yeye alifahamu mashairi yenye hadithi ya John Milton yaitwayo Paradise Lost, ambayo yanaeleza jinsi Shetani alivyofukuzwa mbinguni kwa sababu ya kiburi na uasi wake. Mnamo mwaka wa 1874, Bellver alimaliza kuchonga sanamu iliyoonyesha anguko hilo kubwa.

Bellver hakumchonga Ibilisi akiwa mnyama mwenye pembe, kama alivyoonwa na wengi wakati wake. Kinyume kabisa cha hilo, yeye alimwona mtawala huyo wa roho waovu kuwa malaika mwenye umbo zuri lakini mwovu wakati alipovurumishwa kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:9) Sanamu yake inafanana sana na yale ambayo Biblia inaeleza. *

Watu wa Madrid waliionaje sanamu hiyo? Kulingana na mwanahistoria mmoja wa sanaa, wengine wao walishtushwa na wazo la kutengeneza sanamu kwa ajili ya Shetani. Hata hivyo, serikali ya Hispania iligharimia uchongaji wa sanamu hiyo, nayo ikashinda tuzo mbili kwa sababu ya uzuri wa umbo lake, moja katika Madrid na jingine katika Maonyesho ya Kimataifa ya Paris mnamo mwaka wa 1878. Hivyo, sanaa ikashinda utamaduni, na katika mwaka wa 1879 sanamu hiyo yenye kuvutia ya shaba ikawekwa mahali pake katika bustani ya Retiro.

Katika ulimwengu wa leo usiopenda sana mambo ya kidini, sanamu hiyo ya Shetani haiwaudhi watu wengi. “Jiji la Madrid linapaswa kujivuna kwa kuwa jiji pekee duniani ambalo limeweka wakfu sanamu kwa ajili ya Ibilisi mwenyewe,” akasema María Isabel Gea katika kitabu chake Curiosidades y Anécdotas de Madrid (Udadisi na Visa vya Madrid). Ingawa huenda hilo ni kweli, ni wageni wachache tu kati ya maelfu ya wageni ambao hutembelea bustani ya Retiro kila Jumapili ambao huikazia fikira.

Vivyo hivyo, leo ni watu wachache ambao hutambua kwamba Shetani ndiye kisababishi kisichoonekana cha matatizo mengi katika ulimwengu. (Ufunuo 12:12) Hata hivyo, kwa sababu ya maelezo ya wazi kuhusu Shetani yaliyomo katika Maandiko, wanafunzi wa Biblia hawashuku kuwako kwake ama uvutano wake. Yesu alipinga vishawishi vyake vya wazi. Yeye pia alimfafanua roho huyo mwovu kuwa ‘mwongo na baba ya uwongo,’ na kuwa ‘muua-binadamu kikatili ambaye hakusimama thabiti katika kweli.’—Yohana 8:44; Mathayo 4:1-11.

Wakati huu ambapo dunia ina taabu kuliko wakati mwingine wowote, ni muhimu kupinga uvutano wa malaika huyo muasi mwenye hasira kali. * (Yakobo 4:7) Wakati huohuo, wale wanaopenda kweli na haki wanaweza kupata faraja kwa kujua kwamba kufukuzwa kwa Shetani kutoka mbinguni ni mwanzo tu wa kushindwa kwake ambako kutatukia hivi karibuni wakati Kristo ‘atakapovunja-vunja kazi za Ibilisi.’—1 Yohana 3:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Sanamu hiyo pia inaonyesha nyoka aliyejiviringisha kuzunguka mwili wa Shetani, jambo ambalo Biblia haisemi. Inaonekana Bellver alichochewa na sanamu ya Laocoon aliyoiona huko Roma. Laocoon alikuwa mwana-mfalme wa Trojan, na inasemekana kwamba yeye na wanawe wawili waliuawa na nyoka wawili.

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukinza uvutano wa Shetani, ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.