Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Bado Mataifa Hayajajifunza Somo

Bado Mataifa Hayajajifunza Somo

Bado Mataifa Hayajajifunza Somo

‘Iwapo sisi wanadamu tungeweza kujifunza kutokana na yaliyopita—tungejifunza masomo muhimu sana! Lakini hisia kali na migawanyiko hutupofusha, na masomo tunayopata kutokana na mambo tuliyojionea ni kama taa iliyowekwa kwenye sehemu ya nyuma ya mashua ambayo inaangazia tu mawimbi yaliyo nyuma yetu!’—Samuel Taylor Coleridge.

JE, UNAKUBALIANA na maneno hayo ya mshairi Mwingereza, Samuel Coleridge? Je, hisia zetu kwa ajili ya harakati fulani zaweza kutupofusha sana hivi kwamba turudie kufanya makosa makubwa ambayo yalifanywa na vizazi vya kale?

Vita ya Dini

Kwa mfano, hebu fikiria mambo fulani ambayo watu walifanya wakati wa zile Vita za Dini. Mnamo mwaka wa 1095 W.K., Papa Urban wa Pili aliwachochea “Wakristo” kuwanyang’anya Waislamu ile Nchi Takatifu. Wafalme, watu wenye vyeo, mashujaa, na watu wa kawaida katika mataifa yote yaliyosimamiwa na Urban wa Pili walikubali mwito wake. Mwanahistoria mmoja wa zama za kati alisema kwamba “karibu mataifa yote yaliyoishi kulingana na sheria ya Kristo” yaliitikia mwito huo haraka.

Mwanahistoria Zoé Oldenbourg anasema kwamba wapiganaji wengi wa zile Vita za Dini “walisadiki kabisa kwamba [walikuwa] wakimtumikia Mungu Mwenyewe walipopigana vita hizo.” Anasema kwamba walijiona kuwa “malaika waangamizi wanaowashambulia watoto wa ibilisi.” Pia, kama vile mwandishi Brian Moynahan anavyosema, waliamini kwamba wapiganaji “wote ambao walikufa wangepata tuzo huko mbinguni ya wale wanaofia imani.”

Huenda ikawa wapiganaji wa zile Vita za Dini hawakufahamu kwamba adui zao waliamini vivyo hivyo. Katika kitabu chake Shorter History of the World, mwanahistoria J. M. Roberts anasema kwamba wanajeshi Waislamu walienda vitani pia wakisadiki kwamba walikuwa wakimpigania Mungu na “kwamba baada ya kuuawa na kafiri vitani wangeingia katika paradiso” huko mbinguni.

Wapiganaji wa pande zote mbili walifundishwa kwamba walikuwa wakipigana vita ya uadilifu—iliyokubaliwa na kubarikiwa na Mungu. Viongozi wa kidini na wa kisiasa waliendeleza maoni hayo na kuchochea hisia za raia zao. Na pande zote mbili zilitenda mambo mengi ya ukatili yenye kuogopesha.

Ni Watu wa Aina Gani Waliohusika?

Ni watu wa aina gani waliotenda maovu hayo? Wengi wao walikuwa watu wa kawaida—ambao hawakuwa tofauti na watu wanaoishi leo. Ni wazi kwamba wengi wao walichochewa na maoni mazuri na tamaa ya kutaka kurekebisha hali mbaya zilizokuwapo ulimwenguni wakati huo. Kwa sababu walikuwa na hisia kali sana, hawakutambua kwamba harakati zao za kupigania “haki,” zilisababisha ukosefu wa haki, maumivu, na kuteseka kwa mamia ya maelfu ya wanaume, wanawake, na watoto wasio na hatia ambao hawangeweza kutoroka maeneo ya vita.

Je, si kweli kwamba mambo hayo yametukia tena na tena katika historia yote? Je, si kweli kwamba viongozi wenye uvutano wamewachochea mamilioni ya watu tena na tena kupigana vita za unyama na za ukatili dhidi ya maadui wao wa kidini na wa kisiasa hata ingawa watu hao katika hali ya kawaida hawangefikiria kamwe kufanya hivyo? Kule kujihusisha kwa pande zote mbili katika pambano hilo na yale madai kwamba Mungu aliunga mkono kila upande, yalihalalisha ukandamizaji wa maadui wa kisiasa na wa kidini. Mbinu hiyo imerudiwa tena na tena na imewafaidi watawala wa kimabavu kwa karne nyingi. Moynahan anasema kwamba mbinu hiyo ndiyo “iliyotumiwa na watu waliochochea yale Maangamizi Makubwa ya Nazi na yale mauaji ya jamii nzima-nzima katika nyakati zetu kama vile ilivyotumiwa katika vita ya kwanza ya dini.”

Lakini huenda ukasema hivi, ‘Watu wenye akili leo hawawezi kukubali kudanganywa jinsi hiyo. ‘Sisi tumestaarabika zaidi.’ Hivyo ndivyo mambo yanavyopasa kuwa. Lakini je, kweli watu wamejifunza kutokana na yaliyopita? Ni nani awezaye kusema kwamba hilo ni kweli anapozingatia mambo yaliyotukia katika muda wa miaka mia moja iliyopita?

Vita ya Kwanza ya Ulimwengu

Kwa mfano, mambo yaliyotukia wakati wa zile Vita za Dini yalirudiwa wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu. Roberts anasema kwamba ‘mojawapo ya mambo ya ajabu kuhusu mwaka wa 1914 ni kwamba katika nchi zote yaonekana watu wengi sana wa vikundi vyote, dini zote, na jamii zote, walienda vitani kwa utayari na kwa furaha.’

Mbona watu wengi sana wa kawaida walienda “vitani kwa utayari na kwa furaha”? Ni kwa sababu imani na maadili yao yaliathiriwa na falsafa za wakati huo sawa na wale wapiganaji wa zamani ambao walienda vitani kwa utayari. Ijapokuwa huenda ikawa wengine walitaka kupigania uhuru na haki, ni wazi kwamba wengi walichochewa na maoni ya kiburi kwamba nchi yao ilikuwa bora kuliko nchi nyingine na hivyo ilistahili kutawala.

Watu hao walishawishiwa kuamini kwamba vita ni jambo lisiloepukika—jambo la “asili na la lazima.” Mwandishi Phil Williams anasema kwamba nadharia moja ilifanya watu waamini kwamba vita ni njia halali ya “kuangamiza viumbe ambao hawakustahili kuishi.”

Kwa wazi, kila mtu alifikiri kwamba alikuwa akifanya jambo zuri. Na tokeo likawa nini? Mwandishi Martin Gilbert, ambaye pia ni mwanahistoria, anasema kwamba wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, “serikali zilichochea na kuunga mkono ukabila, uzalendo na uwezo wa kijeshi”—na watu wakaziunga mkono bila kufikiri. John Kenneth Galbraith, mtaalamu wa uchumi, alilelewa katika sehemu ya mashambani ya Kanada wakati wa vita hiyo. Alisema kwamba kotekote watu walizungumza kuhusu “upumbavu wa pambano hilo huko Ulaya.” Walisema kwamba “watu wenye akili . . . hawakuunga mkono upumbavu huo.” Lakini kwa mara nyingine tena walihusika. Na matokeo yakawa nini? Wanajeshi Wakanada wapatao 60,000 walikuwa kati ya wale wanajeshi zaidi ya milioni tisa ambao walikufa katika pande zote mbili za pambano hilo lenye kuchukiza ambalo baadaye liliitwa vita ya kwanza ya ulimwengu.

Somo Halijazingatiwa

Katika miaka 20 iliyofuata, kwa mara nyingine tena mtazamo uliokuwapo awali ulianza kuonekana wazi wakati utawala wa Ufashisti na wa Nazi ulipoanza. Hugh Purcell anaandika kwamba Wafashisti walianza kutumia “mbinu za kawaida za propaganda kama vile ishara na hekaya mbalimbali ili kuchochea hisia za watu.” Mbinu moja waliyotumia ambayo ilikuwa na uvutano mkubwa sana ni kuchanganya dini na siasa, kwa kumwomba Mungu awabariki wanajeshi wao.

Adolf Hitler ni mtu mmoja alikuwa “stadi kwa kushawishi umati wa watu na vilevile msemaji hodari.” Katika kitabu cha Hitler and Nazism, Dick Geary anasema kwamba Hitler aliamini kwamba ‘watu waliongozwa na hisia zao wala si akili zao,’ kama vile viongozi wengi wa kale wenye ustadi wa kushawishi walivyoamini pia. Hitler alitumia udhaifu huo wa wanadamu kwa ujanja kuwafanya watu wamchukie adui mmoja—kama wakati ‘alipowaongoza Wajerumani kuwachukia Wayahudi,’ asema Purcell. Aliwakashifu Wayahudi, akisema, ‘Myahudi ndiye anayeharibu taifa la Ujerumani.’

Jambo la kuogopesha kuhusu kipindi hicho chote ni kwamba mamilioni ya watu wenye akili timamu walichochewa kwa urahisi kuwaua watu wengi. Geary anauliza hivi: “Watu wa nchi iliyosemekana kuwa imestaarabika waliwezaje kukubali na hata kujihusisha katika matendo ya ukatili ya serikali ya Nazi?” Zaidi ya hayo, mbali na kuwa nchi ambayo “imestaarabika,” ilikuwa pia nchi iliyosemekana kuwa ya Kikristo! Walishawishiwa kwa sababu walipenda falsafa na hila za wanadamu badala ya mafundisho ya Yesu Kristo. Na tangu wakati huo wanaume na wanawake wengi wenye nia nzuri wameongozwa kufanya matendo ya ukatili!

Georg Hegel, mwanafalsafa Mjerumani, anasema hivi: “Mambo tuliyojionea na mambo yaliyopita yanatufundisha kwamba mataifa na serikali mbalimbali hazijajifunza somo lolote kutokana na yaliyotukia wala hazijatenda kulingana na masomo yoyote ambayo zingeweza kujifunza.” Wengi wanaweza kukataa falsafa za Hegel kuhusu maisha, lakini ni wachache tu wanaoweza kupinga taarifa hiyo. Kwa kusikitisha, inaonekana ni vigumu sana kwa watu kujifunza kutokana na mambo yaliyopita. Lakini je, yapaswa kuwa hivyo kwa upande wako?

Kwa wazi, somo moja la wazi tunalojifunza ni hili: Ili tuweze kuepuka misiba iliyokumba vizazi vilivyopita, tunahitaji kitu chenye kutegemeka zaidi kuliko falsafa za wanadamu zenye kasoro. Basi, ni nini kinachoweza kuongoza kufikiri kwetu ikiwa falsafa za wanadamu haziwezi? Zaidi ya miaka elfu moja kabla ya zile Vita za Dini kuanza, wanafunzi wa Yesu Kristo walionyesha njia ya kweli ya Ukristo ambayo inafaa kufuatwa. Hebu tuchunguze kile walichofanya ili kuepuka kujihusisha katika mapambano ya umwagaji-damu ya wakati huo. Lakini je, yawezekana kwamba mataifa yaliyopo leo yatajifunza jinsi ya kufanya hivyo na kuepuka mapambano? Na bila kujali yale ambayo mataifa yatafanya, Mungu atafanya nini ili kukomesha taabu zinazowapata wanadamu?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mapambano ya wanadamu yamesababisha matendo ya ukatili na kuteseka

[Picha katika ukurasa wa 7]

Juu: Wakimbizi katika eneo lenye vita

Watu waliosemekana kuwa wamestaarabika waliwezaje kujihusisha katika matendo hayo ya ujeuri mwingi?

[Hisani]

Wakimbizi wa Rwanda: UN PHOTO 186788/J. Isaac; kuporomoka kwa jengo la World Trade Center: AP Photo/Amy Sancetta