Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Vijana Wanapokutana Kirafiki Nawashukuru sana kwa makala “Vijana Huuliza . . . Kuna Hatari Gani Mvulana na Msichana Wanapokutana Kirafiki?” (Desemba 22, 2001) Hivi majuzi, nilimuuliza mama yangu swali hilohilo—‘Kukutana kirafiki kuna ubaya gani?’ Nilijua jibu, lakini nilitaka kusadikishwa zaidi juu ya jambo hilo. Niliposoma makala hiyo nilihisi ni kama Yehova alikuwa amesoma mawazo yangu. Makala hiyo iliimarisha azimio langu la kungoja hadi niwe tayari kuolewa, ndipo niwe na rafiki wa jinsia tofauti. Nimefurahi kwa sababu makala zenu huja kwa wakati unaofaa kabisa! Ninasema tena, asanteni sana.

L. F., Marekani

Nilisoma makala hiyo mara tu nilipoipokea, na nilitiwa moyo sana. Nina umri wa karibu miaka 15, na kuna msongo mwingi sana wa marika shuleni. Karibu wanashule wenzangu wote wana marafiki wa kiume, na mara nyingi hunifanyia mzaha kwa sababu mimi sina rafiki wa kiume. Kwa hiyo makala hiyo ilikuwa muhimu sana! Makala kama hizo hutusaidia kukazia zaidi akilini ushauri wa Biblia.

J. R., Finland

Nina umri wa miaka 16, na nimetamani sana kuwa na rafiki wa jinsia tofauti—au kuhisi tu ninathaminiwa. Hata hivyo, nimefikiri kuhusu jambo hilo kwa uzito, na nimeona kwamba ni muhimu nikomae vya kutosha kabla ya kuanza kutafuta urafiki na mtu wa jinsia tofauti. Hilo litatusaidia kuepuka hatari na kutochukua majukumu ambayo hatuna ujuzi wa kuyashughulikia.

A. G., Italia

Nina umri wa miaka 16. Makala hiyo ilikuja kwa wakati ulionifaa mimi na marafiki zangu. Tukitambua kwamba kuna hatari za wavulana na wasichana kukutana kirafiki, sote tuliketi na kuisoma. Makala hiyo ilitusaidia pia kuona maana halisi ya kuwa na rafiki wa jinsia tofauti na maoni ya Biblia kuhusu jambo hilo. Umalizio wa makala hiyo ulinisaidia nitambue kuwa nikisubiri hadi wakati unaofaa ili nikutane kirafiki na mtu wa jinsia tofauti nitaweza kufanya maendeleo ya kiroho na nitatumia “mchanuko wa ujana” kufanya maendeleo hayo.—1 Wakorintho 7:36.

R.L.W., Marekani

Simulizi la Maisha Niliona ni vizuri niwaandikie ili niwajulishe jinsi nilivyofurahia makala yenye kichwa “Nilitegemezwa kwa Kumwamini Mungu Kabisa.” (Desemba 22, 2001) Simulizi la Rachel Sacksioni-Levee lilionyesha jinsi Yehova Mungu anavyowategemeza watumishi wake katika majaribu yao. Hali za ulimwengu zinapozidi kuwa ngumu, masimulizi kama hayo hutusaidia kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu hata tunapopatwa na majaribu.

J. F., Uingereza

Yabisi-Kavu Asanteni sana kwa mfululizo wa makala kuhusu ugonjwa wa yabisi-kavu. (Desemba 8, 2001) Nina umri wa miaka 19, na nilitambua nina ugonjwa wa yabisi-kavu nilipokuwa mwenye umri wa miaka 8. Ninahisi uchungu siku zote, ingawa siku fulani mimi huumwa zaidi. Mimi hufarijiwa na tumaini la kupata uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu, wakati ambapo hatutaugua magonjwa yoyote yenye kuumiza. Hadi wakati huo, nina uhakika wa kwamba atanipatia nguvu ya kuvumilia ugonjwa huu wenye kuumiza.

M. R., Brazili

Habari iliyokuwa kwenye makala hizo ilikuwa yenye kupendeza sana. Nina umri wa miaka 28, na kwa miaka mitatu iliyopita nimeugua aina ya pekee ya yabisi-kavu. Nikiwa na tumaini lililoonyeshwa na makala hizo, ninaweza kuendelea kumtumikia Yehova.

M. U., Italia

Asanteni sana kwa makala zilizohusu yabisi-kavu. Ninatamani Ufalme wa Mungu uje upesi sana ili niweze ‘kuruka-ruka kama kulungu.’ (Isaya 35:6) Nina umri wa miaka saba, na ninaugua baridi-yabisi katika magoti yangu.

E. I., Ugiriki