Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Mungu Ni Nini Kuhusu Jeuri?

Maoni ya Mungu Ni Nini Kuhusu Jeuri?

Maoni ya Biblia

Maoni ya Mungu Ni Nini Kuhusu Jeuri?

JEURI imeenea sana na kuna aina nyingi za jeuri. Mbali na jeuri inayosababishwa na vita, kuna jeuri inayotokea katika michezo, shuleni, kazini, kati ya magenge, jeuri inayosababishwa kwa kutumia dawa za kulevya na vilevile jeuri inayoonyeshwa katika televisheni na sinema. Hata yaonekana kuna jeuri katika familia nyingi. Kwa mfano, uchunguzi mmoja uliofanywa hivi majuzi ulionyesha kwamba wanaume na wanawake milioni 1.2 huko Kanada walipigwa kijeuri na wenzi wao wa ndoa angalau mara moja katika kipindi cha miaka mitano ya karibuni. Uchunguzi mwingine ulionyesha kwamba asilimia 50 hivi ya wanaume wanaowapiga wake zao huwapiga watoto wao kijeuri.

Hapana shaka kwamba wewe, kama watu wengine wengi, unachukizwa na matendo hayo ya jeuri. Hata hivyo, siku hizi jeuri ni sehemu muhimu ya burudani nyingi. Watazamaji hawavutiwi tu na jeuri inayoigizwa katika filamu bali pia na yale matendo halisi ya jeuri yanayoonyeshwa kwenye televisheni. Mchezo wa ndondi na michezo mingine ya jeuri hupendwa sana katika nchi nyingi. Lakini maoni ya Mungu ni nini kuhusu jeuri?

Jeuri Imekuwepo kwa Muda Mrefu

Jeuri imekuwapo kwa muda mrefu. Katika Biblia, kitendo cha kwanza cha jeuri ambacho mwanadamu alifanya kinaonyeshwa kwenye Mwanzo 4:2-15. Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu na Hawa, alimwonea wivu nduguye Abeli na kumwua kimakusudi. Mungu alitendaje? Biblia inaeleza kwamba Yehova Mungu alimwadhibu Kaini vikali kwa sababu ya kumwua nduguye.

Kulingana na Zaire Swahili Bible, kwenye Mwanzo 6:11 tunasoma kwamba zaidi ya miaka 1,500 baada ya tukio hilo, dunia “ikajaa na jeuri.” Tena, Mungu alitendaje? Alimwamuru Noa aliyekuwa mwadilifu kujenga safina ambayo ingemwezesha yeye na familia yake kuwa salama wakati ambapo Yehova angeleta gharika duniani, ili ‘kuharibu’ jamii hiyo yenye jeuri. (Mwanzo 6:12-14, 17) Lakini ni nini kilichowafanya watu kuwa wajeuri hivyo?

Uchochezi wa Mashetani

Simulizi la Mwanzo linaonyesha kwamba wana wa Mungu, malaika wasiotii, walijifanyia miili ya wanadamu, wakaoa wanawake, na kupata watoto. (Mwanzo 6:1-4) Watoto wao, walioitwa Wanefili, walikuwa wanaume wakubwa sana na mashuhuri. Kwa sababu ya kuchochewa na baba zao mashetani, wakawa wakandamizaji wajeuri. Maji ya gharika yalipoongezeka na kuifunika dunia, wakandamizaji hao waovu wakaangamizwa. Lakini yaonekana wale mashetani waliacha miili ya wanadamu na kurudi kwenye makao ya roho.

Biblia inaonyesha wazi kwamba tangu wakati huo, malaika hao waasi wamewachochea sana wanadamu. (Waefeso 6:12) Kiongozi wao, Shetani, anaitwa “muua-binadamu kikatili” wa kwanza. (Yohana 8:44) Kwa hiyo, ni sahihi kusema kwamba jeuri iliyopo duniani ni ya kishetani.

Biblia huonya kwamba jeuri ina uwezo wa kushawishi. Inasema hivi kwenye Mithali 16:29, ZSB: “Mutu wa jeuri anashawishi jirani yake, na kumwongoza katika njia isiyo njema.” Watu wengi leo wameshawishiwa kukubali, kuunga mkono, au kufanya matendo ya jeuri. Pia, mamilioni ya watu wameshawishiwa kufurahia burudani inayotukuza jeuri. Maneno ya Zaburi 73:6 yanaweza kutumiwa kufafanua kwa usahihi kizazi cha leo. Mtunga-zaburi anasema hivi: “Kiburi kimekuwa mkufu shingoni mwao, jeuri huwavika kama nguo.”

Mungu Huchukia Jeuri

Wakristo wanapaswa kujiendeshaje katika ulimwengu wenye jeuri? Simulizi la Biblia kuhusu wana wa Yakobo, Simeoni na Lawi, linatupatia mwongozo mzuri. Dada yao Dina alishirikiana na watu wa Shekemu wasiokuwa na maadili. Hilo lilisababisha abakwe na Mshekemu. Ili kulipiza kisasi, Simeoni na Lawi waliwaua bila huruma wanaume wote wa Shekemu. Baadaye, akiongozwa na Mungu, Yakobo alilaani hasira kali ya wanawe kwa maneno haya: “Simeoni na Lawi ni ndugu; panga zao ni silaha za jeuri. Nafsi yangu, usiingie katika siri yao, fahari yangu usiungane na kusanyiko lao.”—Mwanzo 49:5, 6.

Kupatana na maneno hayo, Wakristo huepuka kushirikiana na watu wanaounga mkono au kutenda jeuri. Kwa wazi, Mungu huwachukia wale wanaounga mkono jeuri. Biblia inasema hivi: “BWANA humjaribu mwenye haki; bali nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu.” (Zaburi 11:5) Wakristo wanashauriwa kuepuka kila namna ya hasira kali, hata usemi wa kijeuri.—Wagalatia 5:19-21; Waefeso 4:31.

Je, Jeuri Itakoma?

Nabii Habakuki wa kale alimwuliza Yehova Mungu hivi: “Kwa nini nalia: ‘Dhuluma’ nawe hutuokoi?” (Habakuki 1:2, Biblia Habari Njema) Labda umeuliza swali kama hilo. Mungu alimjibu Habakuki, akiahidi kwamba atawaondoa “waovu.” (Habakuki 3:13) Pia, kitabu cha unabii cha Isaya kinatoa tumaini. Humo, Mungu anaahidi hivi: “Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako.”—Isaya 60:18.

Mashahidi wa Yehova wana uhakika kwamba hivi punde Mungu ataondoa kutoka duniani aina zote za jeuri na wale wanaoziunga mkono. Wakati huo, badala ya kujaa jeuri, “dunia itajazwa maarifa ya utukufu wa BWANA, kama maji yaifunikavyo bahari.”—Habakuki 2:14.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Jeuri ilianza wakati Kaini alipomwua Abeli