Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Suluhisho?

Je, Kuna Suluhisho?

Je, Kuna Suluhisho?

UFANYE nini na kitu ambacho huhitaji? Inaonekana kwamba suluhisho rahisi ni kukitupilia mbali. Hata hivyo, kuondosha takataka si jambo rahisi. Zipelekwe wapi? Shirika moja la mazingira huko Italia linakadiria kwamba inachukua miaka 1,000 kwa chupa iliyotupwa baharini kuoza. Kwa upande mwingine, karatasi huoza baada ya miezi mitatu tu. Kichungi cha sigara hubaki baharini kwa miaka 5; mifuko ya plastiki, miaka 10 hadi 20; vitu vilivyotengenezwa kwa nailoni, miaka 30 hadi 40; mikebe, miaka 500; na aina fulani ya plastiki inayoitwa polystyrene, miaka 1,000.

Takataka za aina hizo zimeongezeka sana. Siku hizi kuna vitu vingi vya kununua, na watangazaji wa bidhaa hizo wanataka tuamini kwamba tunazihitaji zote. Gazeti la Uingereza la The Guardian linasema hivi kifupi: “Watangazaji wa bidhaa hutusaidia kutosheleza mahitaji ambayo hatukujua tulikuwa nayo.” Ndiyo, sisi hushawishiwa kununua vitu vyote vipya vinavyopatikana kwa sababu tunaogopa tutakosa nafasi ya kuvifurahia. Bila shaka, katika matangazo ya biashara “kitu kipya” kinamaanisha “kitu kizuri na kilicho bora,” na “kitu cha zamani” kinamaanisha “kitu duni au kisichofaa tena.”

Kwa hiyo, tunashawishiwa mara nyingi kununua kitu kipya badala ya kurekebisha kile cha zamani kilichoharibika. Inasemekana kwamba kununua kitu kipya ni rahisi na si bei ghali kama kurekebisha kile kilichoharibika. Jambo hilo ni kweli nyakati nyingine. Hata hivyo, kwa kawaida, kutupa kitu cha zamani na kununua kitu kipya hugharimu pesa nyingi na si jambo la lazima sikuzote.

Vitu vingi vinavyotengenezwa siku hizi hukusudiwa kutumiwa kwa muda mfupi kisha kutupwa. Huenda visiweze kurekebishwa kwa urahisi, jambo ambalo linapaswa kufikiriwa wakati wa kununua vitu vipya. Gazeti moja la Ujerumani lenye ushauri kwa wanunuzi lilisema hivi: ‘Vitu havidumu kwa muda mrefu kama zamani. Vitu vilivyopendwa muda mfupi uliopita havipendwi leo, navyo hutupwa mara nyingi. Kwa hiyo, vitu vinavyoweza kutumiwa tena hutupwa kila siku kana kwamba ni takataka tu!’

Je, kununua vitu vingi visivyo vya lazima ni kwa faida ya wanunuzi? Bila shaka wale wanaofaidika hasa ni wanabiashara wanaotaka faida nyingi. Gazeti la Uswisi la Die Weltwoche linatoa hoja hii: “Kwa hakika uchumi ungeharibika iwapo kila mtu angetumia gari lake na fanicha kwa muda wote wa maisha au hata kuvitumia kwa muda mrefu zaidi.” Ni wazi kwamba kuharibu uchumi si suluhisho hata kidogo kwa kuwa jambo hilo lingemaanisha kwamba hata wanunuzi wangepoteza kazi. Basi, tatizo hilo linaweza kusuluhishwa jinsi gani?

Kutupa, Kutumia Tena, au Kupunguza?

Ili kutatua tatizo hilo katika nchi zao, baadhi ya nchi zilizoendelea hupeleka takataka zake hadi nchi zinazoendelea. Kwa mfano, ripoti moja inaonyesha kwamba “kwenye jaa moja la takataka linalojulikana sana huko Nigeria, kuna mapipa zaidi ya 8,000 yenye tani 3,500 za kemikali hatari. Mapipa hayo ambayo yameshika kutu yanavuja kemikali hizo ambazo zinaharibu udongo na maji.” Yaelekea hiyo si njia nzuri ya kuondoa takataka wala haionyeshi heshima kwa wengine.

Namna gani kutengeneza vitu vipya kutokana na vitu visivyohitajika tena, badala ya kuvitupa tu? Ili jambo hili liwezekane ni lazima takataka zitenganishwe. Tayari katika sehemu fulani jambo hilo ni takwa la kisheria. Wenye mamlaka wanaweza kuagiza kwamba karatasi, chuma, kioo, na vyakula vitupwe katika mapipa tofauti-tofauti. Kisha, huenda ikawa lazima kutenganisha vioo kulingana na rangi.

Ni wazi kwamba kuna faida kutumia vitu visivyohitajiwa ili kutengeneza vitu vipya badala ya kuvitupa. Kitabu 5000 Days to Save the Planet kinasema kwamba kutumia upya alumini “huokoa nishati nyingi sana,” na kunaweza “kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na uchimbaji wa madini aina ya bauxite.” Kitabu hicho kinaongeza: “Ili kutengeneza karatasi kwa kutumia karatasi zilizotupwa, nusu tu ya nishati na asilimia kumi tu ya maji huhitajika. . . . Takataka za viwanda zinaweza kutumiwa kutengeneza vitu vingine au kutumiwa tena. . . . Hata wakati viwanda fulani visipoweza kutumia takataka zake vyenyewe, huenda viwanda vingine vinaweza kuzitumia . . . Huko Uholanzi, viwanda vimebadilishana takataka kwa mafanikio tangu mwanzoni mwa miaka ya 1970.”

Baadhi ya watu wenye mamlaka hukazia mbinu za kupunguza takataka badala ya kutafuta njia za kuziondosha. Kitabu kilichotajwa mapema kinaonya kwamba “ni lazima hatua ichukuliwe haraka” ikiwa wanadamu “wataacha uchumi unaoendelezwa na kununua na kutupa vitu ovyoovyo . . . na kujenga jamii inayotumia vitu kwa uangalifu ili kupunguza takataka na matumizi ya mali.”

Hata hivyo, itawabidi wale wanaotaka “kuacha uchumi unaoendelezwa na kununua na kutupa vitu ovyoovyo” wawe tayari kutumia vitu vyao kwa muda mrefu iwezekanavyo, na kuvitupa tu visipoweza kurekebishwa tena. Ni lazima wawe tayari kuwapa watu wengine vitu visivyoharibika ambavyo hawavihitaji tena. Idara ya Darmstadt ya taasisi fulani ya mazingira huko Ujerumani, inayoitwa Öko-Institut, inakadiria kwamba takataka zingepungua kwa asilimia 75 iwapo watu wangefuata kwa uthabiti kanuni “Tumia badala ya kununua na kutupa.”

Lakini je, watu wengi watafuata kanuni hizo? La, haielekei hivyo. Tatizo la takataka linalowakumba wanadamu ni dalili tu ya matatizo makubwa zaidi. Siku hizi, mbali na kuwa na tabia ya kununua na kutupa vitu ovyoovyo, watu wengi wamesitawisha mwelekeo wa kutupatupa vitu. Acha tuchunguze mwelekeo huo, na baadhi ya matokeo yake mabaya.

Hatari Zinazosababishwa na Mwelekeo wa Kutupatupa Vitu

Mbali na kutupa tu vitu ovyoovyo, mwelekeo huo unaweza kuwafanya watu wakose uthamini na upendo, na kuwafanya watupe chakula kingi bila kujali na kuharibu mali nyinginezo. Watu wenye ubinafsi na wanaofuata mitindo mbalimbali na mapendezi yao yasiyo muhimu, huvutiwa mara nyingi kununua nguo mpya, vyombo vya nyumbani, na vitu vingine vipya, na kutupa vile walivyo navyo.

Hata hivyo, yaelekea mwelekeo huo wa kutupatupa vitu hauhusishi vitu tu. Hivi majuzi, ripoti iliyohusu mradi mmoja nchini Ujerumani wa kutumia tena vitu vya nyumbani vilivyotupwa, ilisema hivi: ‘Sisi huwatendea wanadamu wenzetu jinsi tunavyozitendea fanicha. Tunazitupa baada ya miaka mitano na kununua mpya kwa sababu hatuzipendi tena. Jamii yetu inaweza kustahimili mwelekeo huo kwa muda gani?’ Ripoti hiyo inaeleza hivi: “Mara tu mtu anaposhindwa kufanya kazi kwa kadiri inavyotakiwa, yeye hufutwa kazi. Kwa vyovyote, kuna watu wengi wa kuajiri.”

Al Gore, aliyekuwa Makamu wa Rais huko Marekani aliuliza swali hili muhimu katika kitabu chake Earth in the Balance: “Ikiwa tunavitupa ovyoovyo vitu tunavyovitumia, je, tumebadili maoni yetu juu ya wanadamu wenzetu kwa njia iyo hiyo? . . . Je, tumesahau kwamba kila mtu ni wa pekee na muhimu?”

Kwa watu ambao hawathamini wala hawaheshimu wengine inaweza kuwa jambo rahisi—wala hawalioni kuwa kosa—kuwatupilia mbali marafiki na wenzi wa ndoa. Gazeti Süddeutsche Zeitung la Ujerumani linasema hivi likizungumzia maoni hayo: “Mara mbili kwa mwaka sisi hununua nguo mpya, kila miaka minne sisi hununua gari jipya, na kila miaka kumi sisi hununua fanicha mpya; kila mwaka sisi hutembelea eneo jipya wakati wa likizo; sisi huhama nyumba, na kubadili kazi na biashara kwa ukawaida. Hivyo basi, kwa nini tusibadili mwenzi wa ndoa?”

Ni kana kwamba baadhi ya watu leo huwa tayari kutupilia mbali chochote kile kinachokuwa mzigo kwao. Kwa mfano, katika nchi moja ya Ulaya, inakadiriwa kwamba paka 100,000 na mbwa 96,000 hivi walitupwa katika mwaka wa 1999. Mtu mmoja anayeshughulikia hali ya wanyama alisema kwamba wananchi wenzake “hawaelewi kwamba mnyama anahitaji kutunzwa kwa muda mrefu. Wao hununua mbwa mwezi wa Septemba na kumwacha [baada ya mwaka mmoja wanapokwenda likizoni] mwezi wa Agosti.” Jambo baya hata zaidi ni kwamba mwelekeo wa kutupatupa unaathiri maoni ya watu kuhusu uhai wa binadamu.

Kutoheshimu Uhai

Yaelekea kwamba watu wengi leo hawathamini maisha yao. Kwa nini twasema hivyo? Kwa mfano, hivi majuzi gazeti moja la Ulaya lilisema kwamba idadi ya vijana walio tayari kuhatarisha maisha yao imeongezeka katika miaka ya karibuni. Jambo hilo linaonekana wazi katika utayari wao wa kushiriki katika michezo hatari. Wao wako tayari kuhatarisha maisha ili wajifurahishe kwa muda mfupi tu! Wanabiashara wenye pupa hujipatia faida nyingi kwa sababu ya mwelekeo huo. Mwanasiasa mmoja Mjerumani alisema kwamba wale wanaoendeleza michezo hatari “huona mara nyingi pesa kuwa muhimu kuliko afya na uhai wa binadamu.”

Vipi kutupilia mbali uhai wa binadamu asiyezaliwa? Shirika la Afya Ulimwenguni linakadiria kwamba “ulimwenguni pote mimba milioni 75 hutungwa ambazo hakuna mtu anayezitaka. Wanawake wengi hawana namna nyingine ila kutoa mimba.” Watoto wachanga wamo hatarini hata baada ya kuzaliwa. Kulingana na gazeti la O Estado de S. Paulo la Brazili, “idadi ya watoto wachanga wanaotupwa inaongezeka.” Je, jambo hilo hutukia katika eneo lenu pia?

Kotekote duniani kuna uthibitisho kwamba uhai wa binadamu huonwa mara nyingi kuwa duni, usio na thamani, kana kwamba ni kitu kinachoweza kutupwa tu. Jambo hilo linaonekana wazi tukifikiria jinsi watu wengi wanavyofurahia kuwaona “watu wanaodhaniwa kuwa mashujaa” wakiwachinja “watu wabaya” wengi katika kipindi kimoja tu cha televisheni au katika sinema mbalimbali. Tunaona jambo hilo pia katika uhalifu wenye ujeuri unaoenea duniani. Wezi huwaua watu kwa sababu ya pesa kidogo sana au hata bila sababu yoyote. Tunaliona vilevile katika habari zenye kusikitisha kuhusu mashambulizi ya magaidi, mauaji ya watu wa makabila mbalimbali, na ya jamii nzimanzima, ambayo yahusisha mauaji ya bila huruma ya wanadamu wengi. Uhai wenye thamani hutupiliwa mbali kana kwamba ni takataka tu.

Hatuwezi kuepuka kuishi miongoni mwa watu wanaopenda kununua na kutupa vitu ovyoovyo, lakini tunaweza kuepuka kuwa na mwelekeo kama wao. Makala inayofuata inazungumzia jinsi tunavyoweza kukabiliana na tabia ya kununua na kutupa vitu ovyoovyo katika jamii yetu na vilevile mitazamo mibaya inayoambatana na tabia hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Katika sehemu nyingi kutengeneza vitu vipya kutokana na vitu vilivyotupwa ni takwa la kisheria

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, wewe hushurutishwa kutupa nguo nzuri na kununua mpya kupatana na mtindo?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Watoto ambao hawajazaliwa wanapaswa kupendwa, bali si kutupwa

[Hisani]

Index Stock Photography Inc./BSIP Agency

[Picha katika ukurasa wa 8]

Uhai ni wenye thamani sana na haupaswi kuhatarishwa ili kujifurahisha