Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nifanyiwe Upasuaji wa Kubadili Sura?

Je, Nifanyiwe Upasuaji wa Kubadili Sura?

Vijana Huuliza . . .

Je, Nifanyiwe Upasuaji wa Kubadili Sura?

“Kabla sijafanyiwa upasuaji uliobadili pua langu, nilifanyiwa mzaha sana. Sikutaka kuwa na pua la kipekee, bali nilitaka kupata lile lililonifaa. Matokeo ya upasuaji huo yamenifurahisha sana, na singesita kufanyiwa upasuaji mwingine kukiwa na uhitaji.”—Eleni. *

“Mbona nifuate maoni ya wengi kuhusu lile wanaloona kuwa umbo zuri? Ikiwa ningebadili viungo vyangu ningehisi nikiwa kama pesa bandia. Singekuwa mtu halisi.”—Mathias.

“Ni lazima kila mtu ajiamulie mwenyewe. Ni vigumu sana kwa mtu mwingine kukuamulia.”—Manuela.

“MTU yeyote ambaye ni mrembo kuliko mimi bila shaka amejipodoa.” Msemo huo wenye kuchekesha hutumiwa Ujerumani na wale ambao hufikiri kwamba hawana umbo zuri. Siku hizi, katika nchi fulani msemo huo unaweza kufanywa uwe wa kisasa zaidi: “Mtu yeyote ambaye ni mrembo kuliko mimi bila shaka amefanyiwa upasuaji wa kubadili umbo lake.” Kwa kweli, upasuaji wa kubadili sura unazidi kuwa jambo la kawaida.

“Wakati ambapo upasuaji wa kubadili sura ulifanyiwa matajiri pekee umepita,” linasema gazeti la Uswisi Neue Zürcher Zeitung, likiongeza kusema: “Mielekeo miwili imeonekana: Wanaume wengi zaidi wanafanyiwa upasuaji wa kubadili sura . . . , na wateja wa kike wanazidi kuwa wachanga kuliko wakati mwingine wowote.” Kulingana na uchunguzi uliofanywa Ujerumani, karibu asilimia 20 ya watu wenye umri wa kati ya miaka 14 na 29 waliofanyiwa uchunguzi, walikuwa ama wamefanyiwa upasuaji wa kubadili sura, wanapanga kufanyiwa, au wamewahi kufikiria kufanyiwa upasuaji huo. * Huenda baadhi ya rafiki zako, wanashule wenzako, au watu wa familia yenu wamefanyiwa upasuaji huo.

Namna gani wewe? Umewahi kufikiria kuboresha umbo lako kwa kufanyiwa upasuaji? Je, unaona masikio yako yakiwa makubwa, matiti yako yakiwa makubwa au madogo sana, tumbo lako au mapaja yako yakiwa manene, ama pua lako kukosa sura nzuri? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayehisi hivyo. Kikundi cha wanafunzi wa shule ya upili waliandika makala katika gazeti moja la Ujerumani na kusema hivi: “Hakuna msichana wa rika letu ambaye nyakati nyingine haridhishwi na mwili wake.” Tamaa ya kuvutia wengine na kupendwa ni ya kawaida. Lakini je, suluhisho ni kufanyiwa upasuaji?

Je, Upasuaji Ndio Suluhisho la Matatizo Yako?

Wafikirie vijana unaowajua. Je, ungeshangaa kujua kwamba wengi wao—labda hata baadhi ya wale ambao unaona wakiwa na umbo zuri—hawaridhishwi na jinsi walivyo? Lakini huenda hivyo ndivyo mambo yalivyo. Swali ni, Je, unafikiri kwamba wote wanapaswa kufanyiwa upasuaji wa kurekebisha sura zao? Au, je, unaona kwamba wengi wao wangekuwa katika hali nzuri ikiwa wangeridhika na mambo mazuri kuhusu umbo lao? Je, wewe mwenyewe unaweza kutumia kanuni hiyo?

Kama Eleni alivyosema, upasuaji wa kubadili sura unaweza kuzuia usichekwe na kufanyiwa mzaha. Kwa upande mwingine, upasuaji huo hautatui matatizo yote. Upasuaji huo hauondoi umuhimu wa kuishi vizuri, ambako kwaweza kuboresha umbo lako sana. Na ingawa daktari-mpasuaji anaweza kubadili sura yako, hawezi kubadili utu wako, au kukuondolea mahangaiko yako ama kukufanya ujistahi zaidi.

Pia, kumbuka kwamba madaktari na zahanati fulani hutoa ahadi wasizoweza kutimiza. Ingawa huenda wakaahidi kukuongezea furaha, huenda wakapendezwa zaidi na pesa zako kuliko na furaha yako. Inasikitisha kwamba kuna madaktari wachache ambao wanaweza kufanya upasuaji ambao hauhitajiki, hauelekei kufanikiwa au hata ambao ni hatari, maadamu tu watalipwa.

Pia, fikiria wakati wako ujao. Kwa mfano, umbo ambalo halikupendezi ukiwa na umri wa miaka 16 huenda likakupendeza unapokuwa na umri wa miaka 21. Daktari wa upasuaji wa kubadili sura, Dakt. Urs Bösch anasema: ‘Kwa ujumla, vijana wenye umri wa kati ya miaka 13 na 19 hawapaswi kufanyiwa upasuaji wa kubadili sura. Umbo la mwili wa vijana hao na maoni yao kuhusu umbo lao hubadilika wanapokuwa katika umri huo.’ Kwa kuongezea, huenda vijana wakahitaji kufanyiwa upasuaji mwingine ili kurekebisha upasuaji wa kwanza. Mwili wako unapoendelea kukua, huenda makovu yanayosababishwa na upasuaji yakawa makubwa.

Hesabu Gharama

Biblia hututia moyo tuhesabu gharama kabla ya kuanza kufanya jambo la maana. (Luka 14:28) Vijana wengi hawawezi kufanyiwa upasuaji wa kubadili sura, kwa sababu hawawezi kuugharimia. Na huenda ukagharimu hata zaidi kwa sababu ya uchunguzi unaofanywa baadaye au upasuaji mwingine ambao huenda ukahitajika.

Watu fulani wamepatwa na matatizo ya afya baada ya kupasuliwa. Kulingana na Chama cha Upasuaji wa Kubadili Sura cha Marekani, matatizo hayo yanatia ndani kuvimba kwa muda, makovu ya kudumu, kukosa hisi, kushindwa kunyonyesha, na hata kupoteza damu nyingi. Kwa mfano, Anna karibu afe alipofanyiwa upasuaji wa kuondoa mafuta mwilini mwake. Analalamika hivi: “Sasa nina makovu mabaya sana na shimo tumboni mwangu.” Kuhusu upasuaji wa aina hiyo, gazeti moja la Ujerumani lasema: “Ripoti kuhusu matatizo makubwa wakati wa upasuaji, hata kifo, zinaongezeka.” Usisahau kwamba: “Upasuaji wa kubadili sura ni kama upasuaji mwingine wowote, nao ni hatari pia,” kama lisemavyo gazeti la afya Apotheken Umschau. Hivyo, chunguza kwa makini hatari zinazohusika kabla ya kuchagua kufanyiwa upasuaji wowote, hasa ule ambao si wa lazima.

Unaweza pia kujiuliza hivi: ‘Watu watanionaje? Je, watafikiri kwamba ninaona umbo kuwa jambo la maana zaidi? Uamuzi wangu utawaathirije vijana wenzangu au wadogo wangu?’ *

Kusudi Lako

Pia, unahitaji kufikiria kwa uzito kusudi la kufanyiwa upasuaji wa kubadili sura. Na haitakuwa rahisi kulifahamu vizuri. Jiulize hivi: ‘Je, ninataka kuepuka kuchekwa kwa sababu ya sehemu fulani ya mwili isiyopendeza? Au ninafuatia mambo yasiyo na maana? Je, ninatamani kubadili sura yangu kwa sababu ya kusongwa na marika, matangazo ya biashara, au mtumbuizaji mashuhuri? Je, ninatamani kufikia kiwango cha juu sana cha urembo ambacho kimewekwa na vyombo vya habari?

Wengine hufikiri kwamba kubadili umbo lao kwaweza kuongeza uwezekano wa kupata mwenzi wa ndoa au kazi nzuri. Hata hivyo, je, kila mtu aliyefunga ndoa anavutia? Namna gani wale walioajiriwa? La, mambo hayo hayategemei umbo tu. Zaidi ya hilo, iwapo yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa au mwajiri wako angetilia maanani umbo zaidi ya utu wako, je ingefaa kugharimika au kujihatarisha kwa ajili yake?

Unapofikiria kusudi lako kwa makini, ongea na wazazi wako au rafiki mkomavu. Ikiwa hupendezwi na sehemu moja ya mwili wako, waombe maoni. Usitumaini tu yale unayoona kwenye kioo. Kuhusu jinsi tunavyoona kasoro zetu, Nana anasema: “Sisi huona kasoro zetu kuliko wengine kwa sababu tuna maoni tofauti.” Wachunguzi katika Chuo Kikuu cha Landau, Ujerumani, walieleza kwamba mara nyingi watu hufikiria upasuaji wa kubadili sura “si kwa sababu sehemu ya mwili ina kasoro, lakini kwa sababu mtu anaiona ikiwa na kasoro.”

Usifanye uamuzi wa haraka-haraka, bali chunguza mambo yote kwa uangalifu. Uone upasuaji kama jambo lisiloweza kubadilishwa. Itakubidi kuishi na matokeo yake kwa muda fulani.

Urembo Ulio Bora Zaidi

Furaha haitokani na ubora wa umbo lako. Ingawa umbo lako laweza kukufanya ujistahi au usijistahi, jambo la maana zaidi ni utu na mtazamo wako. Baada ya kuhatarisha uhai wake, Anna alimalizia hivi: “Nimejifunza kwamba urembo hauhusiani kwa vyovyote na umbo.”

Ingawa Biblia inasifu urembo wa kimwili, inaonyesha kwamba urembo wa kiroho ni muhimu zaidi: “Madaha huhadaa na uzuri haufai, bali mwanamke amchaye Mwenyezi-Mungu atasifiwa.” (Mithali 31:30, BHN; 1 Samweli 16:7) Ukiwa na maoni hayo unaweza kupata amani ya moyoni, licha ya kuwa na sehemu ya mwili isiyokuvutia.

Kumbuka kwamba hata uamuzi wako uwe nini, huwezi kuwa mrembo kikamili au kuwa na furaha ya kudumu sasa. Kila mtu ana kasoro fulani. (Waroma 3:23) Huwezi kubadili jambo hilo. Unaloweza kubadili ni jinsi ulivyo ndani, kama vile Biblia inavyosema “yule mtu wa siri wa moyoni.” (1 Petro 3:3, 4) Badili utu wako kwa kutokeza sifa nzuri machoni pa Mungu. Kufanya hivyo hakugharimu pesa zozote wala hakusababishi hatari yoyote, bali kunaleta manufaa nyingi!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 7 Upasuaji wa kubadili sura hufanyiwa sehemu za mtu zisizo na kasoro ili aboreshe umbo lake. Upasuaji wa kurekebisha sura hufanywa ili kurekebisha sehemu za mwili ambazo zimeumbuka kwa sababu ya majeraha, magonjwa au kasoro ambazo mtu amezaliwa nazo. Hizi zote ni aina za upasuaji wa kubadili sura.

^ fu. 17 Ona pia sura inayosema, “Sura Ni ya Maana Kadiri Gani?” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Je, “tatizo” lako ni halisi, au unahitaji kurekebisha maoni yako?