Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuepuka Mwelekeo wa Kutupatupa Vitu

Kuepuka Mwelekeo wa Kutupatupa Vitu

Kuepuka Mwelekeo wa Kutupatupa Vitu

“HAKUNA kitu kinachopotea bure . . . katika mazingira.” Kulingana na gazeti la Time, hayo ni maoni ya mtaalamu mmoja anayeheshimika wa mbinu za kutumia vitu tena. Alitaja jinsi ambavyo vitu vinavyonyauka na kuoza katika mazingira hunufaisha vitu vingine. Kulingana na gazeti hilo mtaalamu huyo anahisi kwamba “wanadamu wanaweza kuiga mazingira, lakini jambo hilo lingemaanisha kubuni tekinolojia mpya na kubadili mielekeo ya watu kabisa.”

Si watu wengi wanaoweza kubuni tekinolojia mpya. Lakini tunaweza kudhibiti mwelekeo wetu! Na tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu maadili na tabia nzuri tutaweza kukabiliana vizuri zaidi na matatizo yanayosababishwa na kununua na kutupa vitu ovyoovyo.

Epuka Kutupatupa Vitu

Mtu mmoja kati ya watano duniani hulala njaa. Kujua jambo hilo kunapaswa kutufanya tuthamini chakula na tuepuke kukitupa. Wenzi wa ndoa waliorudi Ulaya baada ya kufanya kazi ya mishonari barani Afrika kwa miaka 28 walisema kwamba ilikuwa vigumu kuzoea tena maisha katika nchi ya kwao hasa kwa sababu ya kuona jinsi ambavyo “watu hutupa chakula ovyoovyo.”

Wazazi wenye hekima huwafundisha watoto wao kujipakulia kiasi cha chakula ambacho wanaweza kumaliza. Kufanya hivyo hupunguza takataka na uharibifu wa mali. Ni afadhali kujipakulia chakula kidogo kwanza, kabla ya kuomba kuongezewa. Bila shaka wazazi wanahitaji kuwa mfano mzuri. Yesu alikuwa mfano mzuri kwetu sote kwa kuthamini kwa moyo maandalizi ya kimwili na ya kiroho ya Mungu. Biblia inaonyesha kwamba Yesu hakutupa chakula—hata ingawa kilikuwa kimeandaliwa kwa wingi kwa njia ya mwujiza!—Yohana 6:11-13.

Vilevile, haifai kutupa vitu ambavyo havijaharibika kama vile nguo, fanicha, na mashine. Sisi huonyesha kwamba tunathamini vitu tulivyo navyo kwa kuvitunza na kuvitumia kwa muda mrefu iwezekanavyo. Tusidanganywe na watangazaji wa biashara ambao hujitahidi kutufanya tusiridhike na vitu tulivyo navyo kwa kutangaza vitu vikubwa, bora, vinavyofanya kazi kwa kasi zaidi, na vyenye nguvu zaidi. Ni wazi kwamba tuna uhuru wa kununua vitu vipya hata ingawa vitu tulivyo navyo havijaharibika. Lakini kabla ya kufanya hivyo, huenda ikafaa tuchunguze mwelekeo wetu na kile kinachotusukuma kufanya hivyo.

Epuka Pupa

Waisraeli waliposafiri jangwani wakiwa njiani kuelekea Nchi ya Ahadi, walipewa chakula kilichoitwa mana. Kulingana na Biblia, kulikuwa na mana ya kutosha. Hata hivyo, Waisraeli walionywa wasiwe wenye pupa; walikuwa wachukue kiasi cha kutosha tu kwa kila siku. Wale ambao hawakutii waligundua kwamba pupa haikuwafaidi, kwa kuwa mabuu waliingia katika mana iliyobaki na ikawa na harufu mbaya. (Kutoka 16:16-20) Biblia inashutumu pupa waziwazi mara nyingi.—Waefeso 5:3.

Si Biblia pekee inayoshutumu pupa. Kwa mfano, mwanafalsafa Mroma, Seneca, aliyekuwa pia mwandishi wa michezo ya kuigiza katika karne ya kwanza, alitambua kwamba mtu mwenye pupa haridhiki kamwe. Alisema hivi: “Vitu vyote duniani haviwezi kutosheleza pupa.” Erich Fromm, mwanafalsafa aliyeishi katika karne ya 20, alikata kauli hiyohiyo: “Jitihada ya kutosheleza tamaa za pupa ni kama kujaribu kujaza shimo lisilo na mwisho. Jitihada hiyo isiyo na mwisho ya kutosheleza tamaa humchosha mtu bila kumtosheleza kamwe.” Mbali na kuepuka pupa na kuharibu mali bure, kuna mambo mengine ambayo watu wengi wameamua kufanya.

Jifunze Kutoa

Badala ya kutupa tu vitu ambavyo havijaharibika, mpe mtu ambaye angeweza kufurahia kuvitumia. Kwa mfano, nguo za watoto zisipowatosha tena, je, watoto wengine wangeweza kuzitumia? Je, ungeweza kumpa mtu mwingine vitu vingine pia ambavyo havijaharibika lakini huvitumii tena? Mpe mtu mwingine kitu ambacho wewe umefurahia ili yeye pia akifurahie. Mwandishi na mchekeshaji Mmarekani, Mark Twain, aliandika hivi: “Ili furaha yako iwe kamili ni lazima mtu mwingine aishiriki.” Huenda ikawa umeona kwamba furaha yako huongezeka unapomruhusu mtu mwingine kufurahi pamoja nawe. Zaidi ya hayo, kwa kutoa kwa njia hiyo, wewe hupunguza matokeo mabaya yanayosababishwa na mwelekeo wa kutupatupa vitu.

Kutoa husifiwa sana katika Biblia. (Luka 3:11; Waroma 12:13; 2 Wakorintho 8:14, 15; 1 Timotheo 6:18) Naam, hali ingekuwa bora sana duniani iwapo watu wote wangekuwa tayari kutoa!

Ridhika na Vitu vya Lazima

Mtu anayeridhika ni mtu mwenye furaha. Maneno hayo ni ya kweli kila mahali na kila wakati. Methali moja ya Kigiriki inasema hivi: “Mtu ambaye haridhiki na kidogo haridhiki kamwe.” Na Wajapani husema hivi: “Mtu ambaye haridhiki ndiye maskini.” Biblia pia inasifu sana uradhi. Biblia inasema hivi: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.”—1 Timotheo 6:6-8; Wafilipi 4:11.

Huenda tukahitaji ‘kubadili mwelekeo kabisa’ ili turidhike na vitu tulivyo navyo. Hivi majuzi, mwanamke kijana anayeitwa Susanne alitambua kwamba alihitaji kufanya badiliko hilo. Alisema hivi: “Niliazimia kwamba kwa kuwa sikuweza kupata kila kitu nilichopenda, ilinibidi kuanza kupenda vitu nilivyokuwa navyo. Sasa mimi ni mwenye furaha na nimeridhika.”

Kuridhika huleta furaha kwelikweli. Mtaalamu wa uzee huko Bulgaria, profesa Argir Hadjihristev, anasema hivi: ‘Ubaya wenyewe hasa ni kutoridhika na vile vitu vichache alivyo navyo mtu.’ Anapoongea juu ya jinsi kuridhika kunavyochangia afya nzuri, anaongeza hivi: “Mtu asiyeng’ang’ania kuwa na mali nyingi kuliko majirani wake wala kuongeza mali sikuzote, hashindani na wengine na kwa hiyo yeye huepuka mfadhaiko. Na jambo hilo hupunguza wasiwasi.”

Naam, kununua na kutupa vitu ovyoovyo hakuwezi kuleta furaha ya kweli, wala kuwa na mwelekeo wa kufanya hivyo. Inaonekana kwamba watu wengi zaidi wanaelewa jambo hilo. Vipi wewe?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Watoto wanahitaji kujifunza jinsi ya kuepuka kuharibu chakula

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu alionyesha mfano bora kwa kutotupa chakula

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mbona usiwapatie wengine vitu ambavyo huvitumii badala ya kuvitupa?