Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ujasiri Wakati wa Msiba Asanteni kwa mfululizo wa makala za kwanza wenye kichwa “Ujasiri Wakati wa Msiba—Siku Ambayo Ile Minara Miwili Iliporomoka.” (Januari 8, 2002) Makala hizo zilinigusa moyo sana, na zikanifanya nitambue kwamba wakati na tukio lisilotazamiwa linaweza kumpata mtu yeyote. Mimi hushikwa na majonzi ninapofikiria watu wengi waliokufa.

S.B.R., Denmark

Asanteni kwa kuchapisha ile habari kuhusu “Sala ya Tatiana.” Nililia nilipokuwa nikisoma makala za kwanza, lakini nililia kwa sauti kubwa zaidi niliposoma habari hiyo. Ninasali kwamba watoto waliofiwa na wazazi wao katika shambulizi hilo la magaidi waweze kukua kiroho ili wakutane nao katika ulimwengu mpya. Makala hiyo pia ilinisaidia nithamini zaidi tumaini zuri la wakati ujao ambalo ninalo nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

T. A., Japan

Hata ingawa ninaishi nchini Ujerumani, mambo yaliyotukia Septemba 11 yalinishtua sana mimi na familia yangu. Baada ya miezi mitatu, binti yangu mwenye umri wa miaka tisa bado alikuwa akichora picha za ndege ikigonga jengo refu. Tunatazamia siku ambayo misiba kama hiyo haitakuwapo tena.

E. G., Ujerumani

Nilipoona mambo yaliyotukia New York, nilimwomba Yehova awaimarishe waokokaji na kuzipa tumaini familia za waliokumbwa na msiba huo. Niliposoma makala hizo, niliona jinsi sala zangu pamoja na za watu wengine wengi zilivyojibiwa. Nilichunguza upya maisha yangu kwa sababu niligundua kwamba msiba waweza kumpata mtu wakati wowote.

M. V., Italia

Tunafurahia kusoma hasa masimulizi ya watu waliokumbwa na hali hiyo. Tulitiririkwa na machozi tuliposoma maelezo ya wale waliookoka msiba huo. Tunamwomba Yehova awasaidie wote walioathiriwa na msiba huo na tunasali ili wafarijiwe na gazeti la Amkeni! Tukiwa vijana, tunatiwa moyo na maswali ambayo yanatusaidia kutafakari kuhusu maisha yetu na mambo tunayotanguliza. Tunatumaini kwamba mtaendelea kuchapisha gazeti hili.

T. M. na A. P., Slovenia

Mimi ni mwanafunzi mwenye umri wa miaka 14 na niko kwenye kidato cha kwanza. Niliposoma makala hizo, nilifahamu jinsi tukio hilo lilivyowatia watu woga. Niliona jinsi watu walivyojitoa mhanga ili kuwaokoa wengine. Nilisikia kwenye taarifa ya habari kwamba wazima-moto wengi walikufa, hata hivyo sikuwa nimeathiriwa sana na habari hizo hapo awali. Nililia niliposoma lile sanduku kuhusu “Sala ya Tatiana.” Baba yangu aliugua akafa nilipokuwa katika darasa la saba. Habari ya Tatiana ilinifanya nijiulize hivi: ‘Je, ulimwengu mpya ni halisi kwangu kama ulivyo kwa Tatiana?’ Ninataka kuwapa walimu wangu pamoja na marafiki wangu wengi gazeti hili. Tafadhali endeleeni kuchapisha magazeti haya mazuri sana!

H. T., Japan

Sura Mpya Inapendeza mno kuona jinsi ambavyo sura ya Amkeni! imebadilika tangu nilipoanza kusoma gazeti hili mwaka wa 1978. Nilipochunguza toleo la Januari 8, 2002, nilivutiwa mno na sura na mpangilio wa kurasa zake. Vichwa vya makala vinaonekana wazi, na picha zinavutia sana. Mpangilio huo unafanya usomaji upendeze. Nina hakika kwamba sura hiyo mpya itawavutia watu wengi zaidi walio wanyofu kwa Yehova.

V.P.L., Brazili