Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inafaa Kutafuta Mwongozo Katika Namba?

Je, Inafaa Kutafuta Mwongozo Katika Namba?

Je, Inafaa Kutafuta Mwongozo Katika Namba?

JE, KUBASHIRI kwa kutumia namba kunapatana na akili na sayansi? Je, namba zinaweza kufunua wakati wetu ujao? Je, inafaa kupanga maisha yako ya baadaye kwa kutegemea mafumbo na ubashiri wa namba?

Wabashiri wengi wanaotumia namba wametatizwa na kipingamizi kimoja. Kipingamizi hicho ni kwamba tamaduni mbalimbali zinatumia kalenda tofauti. Kwa mfano, vipi ikiwa mtu anaishi nchi inayotumia kalenda ya Kichina? Fikiria tarehe ile iliyotajwa kwenye makala ya kwanza—Septemba 11, 2001. Kulingana na kalenda ya Kichina, tarehe hiyo ilikuwa siku ya 24 ya mwezi wa saba, mwaka wa 18 wa mzunguko wa 78. Kalenda ya Julian inaonyesha tarehe hiyo ni Agosti 29, 2001. Kulingana na kalenda ya Waislamu, ilikuwa tarehe 22 Jumada II 1422, na kwenye kalenda ya Waebrania ilikuwa 23 Eluli 5761. Tarehe inayoandikwa kwa njia nyingi hivyo inawezaje kuwa na ujumbe muhimu? Jambo jingine ni hili: Mara nyingi majina huandikwa kwa njia maalumu katika lugha mbalimbali. Kwa mfano, herufi zilizo katika jina la Kiingereza John zinawakilishwa na namba 2, lakini herufi za jina hilohilo katika Kihispania—Juan—zinawakilishwa na namba 1.

Ingawa vitu vingi katika ulimwengu vinategemea fomyula za hesabu, fomyula hizo zinaweza kujaribiwa na kuthibitishwa. Lakini kudai kwamba jina lako lilichaguliwa kimbele lifaane na tarehe yako ya kuzaliwa na kwamba lingeweza kuambatanishwa na namba fulani ili ujue wakati wako ujao ni jambo tofauti kabisa.

Mkataa ni wazi: Si jambo la kiakili kuamini kwamba kubashiri kwa kutumia namba ni sahihi kwa kuwa kunategemea mambo mbalimbali yanayotofautiana sana kama vile kalenda na lugha.

“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”

Baadhi ya watu huvutiwa na ubashiri huo kwa sababu wana hamu ya kujua mambo yao ya wakati ujao. Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba maisha ya mwanadamu hayawezi kupangwa kimbele. Tunasoma hivi: “Si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” “NW”] huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, italiki ni zetu.) Naam, mambo mengi hutukia ghafula. Hatuwezi kamwe kubashiri mambo kulingana na tarehe ya kuzaliwa au namba zinazowakilisha jina kwa sababu ya matukio hayo ya ghafula.

Fikiria mfano mwingine: Biblia inatutia moyo tuwe wakarimu inaposema hivi: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi. Uwagawie sehemu watu saba, hata wanane; maana hujui baa gani litakalokuwa juu ya nchi.” (Mhubiri 11:1, 2, italiki ni zetu.) Mara nyingi, misiba hutukia ghafula na watu hawawezi kujua ni lini itakapotokea. Kwa hiyo, profesa wa hesabu Underwood Dudley anaandika hivi kuhusu wabashiri wanaotumia namba: “Wanapuuza kabisa uwezekano wa mambo kutukia ghafula. Mambo yenye kustaajabisha yanaweza kutukia ghafula tu bila mpango wowote.”

Ni kweli kwamba huenda wabashiri hao wakatabiri mambo fulani na yakatokea. Kwa nini? Nyakati nyingine, mambo hayo yanaweza kutukia kwa usahihi bila kutarajiwa. Nyakati nyingine, wabashiri hao wanaweza kutabiri mambo mengi ambayo yanaweza kuhusiana na matukio kadhaa. Lakini kuna jambo jingine zito sana ambalo linahitaji kufikiriwa.

Je, Ni Namna Fulani ya Uaguzi?

Biblia haitaji moja kwa moja ubashiri wa kutumia namba. Lakini inamtaja Hamani, Mwamaleki ambaye alipanga njama ya kuwaangamiza Wayahudi walioishi Uajemi katika karne ya tano K.W.K. Biblia yasema hivi: “Hamani aliagiza kura (yaani Purimu) ifanywe kupata siku na mwezi ambapo angetekeleza njama zake. Basi, kura ikaangukia siku ya kumi na nne ya mwezi wa kumi na mbili uitwao Adari.”—Esta 3:7, Biblia Habari Njema, italiki ni zetu.

Katika nyakati za kale, kupiga kura kulikuwa njia halali ya kukomesha ubishi. * (Mithali 18:18) Lakini Hamani alitumia kura kufanya uaguzi—zoea ambalo linashutumiwa na Biblia. Andiko la Kumbukumbu la Torati 18:10-12, BHN, lasema kwamba Mungu anamchukia kabisa ‘mtu apigaye ramli, mwaguzi, mpiga bao, mchawi, mlozi, mwenye kutaka kauli kwa mizimu na pepo. Yeyote atendaye mambo haya ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.’

Biblia inaonyesha kwamba uaguzi na nguvu za kiajabu zinahusiana na kuwasiliana na roho waovu. Roho waovu wanaweza kutumia matukio fulani ili kutimiza makusudi yao. Lolote liwalo, jambo moja ni hakika: Mungu anashutumu zoea la kuwasiliana na roho waovu, na kufanya hivyo kunaweza kumfanya mtu awe mtumwa wa roho waovu.—1 Samweli 15:23; Waefeso 6:12.

Kubashiri kwa kutumia namba hakupatani kabisa na sayansi, wala si jambo la kiakili. Na jambo baya zaidi ni kwamba ubashiri huo ni namna fulani ya uaguzi na hivyo ni kinyume cha mafundisho ya Biblia. Kwa hiyo, kubashiri kwa kutumia namba si njia inayofaa ya kupangia maisha yako au miradi yako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kura zilipigwa kwa kutia vitu vidogo-vidogo—kama vile vijiwe au vipande vidogo vya mbao—katika mapindo ya nguo au katika chombo fulani na kuvitikisa. Mtu ambaye kura yake ilitwaliwa kwanza ndiye aliyechaguliwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

KALENDA MBALIMBALI ZINAZUSHA KIPINGAMIZI KUHUSU KUBASHIRI KWA KUTUMIA NAMBA

GREGORY Septemba 11, 2001

KICHINA siku ya 24 ya mwezi wa 7, mwaka wa 18 wa mzunguko wa 78

JULIAN Agosti 29, 2001

WAISLAMU 22 Jumada II 1422

WAEBRANIA 23 Eluli 5761

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

JE, NYOTA ZA UNAJIMU ZINATEGEMEKA?

“Nyakati nyingine wewe ni mwenye urafiki, lakini nyakati nyingine u kimya tu. Unaona haifai kuwaambia watu usiowajua mambo yako ya kibinafsi. Wewe hufuati tu maoni ya watu, unahitaji kuthibitishiwa jambo lolote kabla ya kulikubali. Unapenda mabadiliko, na unahuzunika unapowekewa sheria nyingi. Una uwezo mbalimbali ambao bado hujautumia kikamili. Una mwelekeo wa kujichambua-chambua.”

Je, maelezo hayo yanakufaa? Ikiwa wafikiri hivyo, basi huenda unayachukua maelezo hayo kwa uzito mno, kwa sababu watu wengi wana sifa hizo. Wasomaji huelekea kukubali maelezo ambayo wanaona ni sahihi na kupuuza yale ambayo si sahihi. Kitabu Why Do Buses Come in Threes—The Hidden Mathematics of Everyday Life (Kwa Nini Mabasi Huja Matatu-MatatuHesabu ya Siri Katika Maisha ya Kila Siku) kinasema kwamba “watafiti wamegundua kuwa watu wengi hushindwa kutambua maelezo ya nyota yao wakati alama za nyota zinapoondolewa, lakini wao huamini kuwa maelezo ya nyota yao ni sahihi wanapoona alama hizo.”

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Namba za Mfano Katika Biblia

Biblia hutaja namba fulani za mfano kulingana na muktadha wa Maandiko. Kwa mfano, namba nne hutumiwa kuonyesha ujumla au jambo linalohusu kila mtu. Hoja hiyo inaelezwa na misemo kama vile “ncha nne za dunia” na “pepo nne za mbinguni.” (Isaya 11:12; Danieli 8:8) Nyakati nyingine, namba sita huwakilisha kutokamilika. Kitabu cha Ufunuo kinasema kwamba tengenezo la kisiasa la Shetani hapa duniani lina “nambari ya binadamu”—666. (Ufunuo 13:18) Namba sita imetajwa mara tatu, na hilo linakazia kutokamilika kwa tengenezo hilo ambalo linafananishwa na hayawani. Wakati ambapo namba saba hutumiwa kwa njia ya mfano, hiyo huwakilisha ukamilifu. (Mambo ya Walawi 4:6; Waebrania 9:24-26) Namba hizo na nyinginezo zinazotumiwa kwa njia ya mfano katika Maandiko hueleweka kulingana na unabii unaozungumziwa.

Ingawa Maandiko hukazia umuhimu wa namba fulani, Biblia haituhimizi tupatanishe herufi za maneno fulani na namba ili kujua mambo fulani hakika ya kifumbo.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Hamani alitumia uaguzi ili kuchagua tarehe ya kutekeleza njama yake ya kuwaangamiza Wayahudi wote