Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kimbilio la Wachapaji wa Biblia

Kimbilio la Wachapaji wa Biblia

Kimbilio la Wachapaji wa Biblia

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI UBELGIJI

Karibu miaka 500 iliyopita, baadhi ya Biblia nzima za kwanza zilichapwa huko Antwerp, Ubelgiji. Kwa nini wachapishaji wa Biblia walihamia jiji hilo? Walipata magumu gani kwa sababu ya kuchapisha Biblia? Ili tupate majibu ya maswali hayo, itatubidi turudi nyuma hadi mapema katika miaka ya 1500.

ANTWERP liko kilometa 89 kutoka Bahari ya Kaskazini, kwenye mlango wa Mto Scheldt. Katika miaka ya 1500, jiji hilo la Antwerp lilifanikiwa sana kiuchumi. Jiji hilo lilipanuka upesi na kuwa na bandari kubwa zaidi Ulaya na likawa mojawapo ya majiji machache ya Ulaya Magharibi yenye wakazi zaidi ya 100,000.

Upanuzi huo uliwavutia wafanya-biashara wengi kutoka sehemu zote za Ulaya. Upanuzi huo pamoja na ufanisi ulioongezeka ulifanya baraza la jiji liruhusu mawazo mengi mapya kuliko majiji mengine, na kufanya Antwerp kuwa kitovu cha mawazo mapya. Uhuru ulioletwa na mawazo hayo uliwavutia wapiga chapa waliohisi kwamba jiji hilo lilikuwa mahali salama pa kupigia chapa na kueneza mawazo hayo mapya. Muda si muda, Antwerp lilikuwa na wapiga chapa, wachapishaji, na wauzaji wa vitabu 271. Wakati huo mahakimu walisema kwamba jiji lao lilikuwa “kimbilio na kitovu cha kila aina ya sanaa, sayansi, taifa na maadili.”

Kuchoma Vitabu na Watawa wa Kiume

Kati ya mawazo mapya yaliyochapwa na kusambazwa ni yale ya Martin Luther (1483-1546). Yeye alikuwa kiongozi wa Mageuzo, ule uasi wa kidini uliokuwa mwanzo wa Uprotestanti. Miezi sita tu baada ya Mageuzo hayo kuanza, vichapo vya Luther vilikuwa tayari vinauzwa katika maduka ya vitabu ya Antwerp. Si ajabu, Kanisa Katoliki halikufurahishwa na jambo hilo. Mnamo Julai 1521, kanisa lilihimiza uchomaji wa vitabu 400 vilivyosemekana kuwa vya uasi. Miaka miwili baadaye, watawa wawili wa kiume kutoka Antwerp wa kundi la Augustine waliounga mkono mawazo ya Luther walitundikwa mtini na kuteketezwa wakiwa hai.

Mashambulizi hayo hayakukomesha jitihada za wachapaji jasiri wa Biblia. Ujasiri wa wapiga chapa hao ulichangia sana kusambazwa kwa Biblia kwa watu wa kawaida. Baadhi ya wapiga chapa hao walikuwa nani?

Mpiga-Chapa Awa Mfia-Imani

Adriaen van Berghen alikuwa mpiga chapa na muuzaji wa vitabu. Mnamo 1522 yeye alifungwa miguuni kwa pingu kwa sababu ya kuuza vitabu vya Luther na muda mfupi baadaye alihukumiwa kifungo cha gereza. Alipata msamaha lakini mara moja alirudia kazi yake. Alianza kupiga chapa tena—mara hii sehemu za “Agano Jipya” ya Luther katika Kiholanzi. Tafsiri hiyo ilichapishwa katika mwaka wa 1523, mwaka mmoja tu baada ya kuchapishwa kwa “Agano Jipya” la Luther katika Kijerumani.

Hata hivyo, mnamo mwaka wa 1542 wakati vitabu vingi vilipatikana katika nyumba yake huko Delft, Uholanzi, Van Berghen alikamatwa tena. Kwanza, hakimu alimhukumia kusimama kwa muda wa saa mbili mahali ambapo wafungwa walinyongwa akiwa na “baadhi ya vitabu vilivyopigwa marufuku shingoni mwake.” Lakini baadaye, hukumu ilibadilishwa ikawa ya kifo, na mpiga chapa huyo mjasiri alikatwa kichwa kwa upanga.

Elezo la Pambizoni Lamfanya Auawe

Wakati huo mpiga chapa mwenye matokeo zaidi wa Biblia za Kiholanzi alikuwa Jacob van Liesvelt. Yeye alichapisha Biblia tofauti tofauti 18 za Kiholanzi. Mnamo 1526 alipiga chapa Biblia nzima ya Kiholanzi. Biblia hiyo ilitolewa miaka minne kabla ya Biblia nzima ya kwanza ya Kifaransa na miaka tisa kabla ya Biblia nzima ya kwanza ya Kiingereza! Biblia ya Van Liesvelt ilitegemea sana ile ya Kijerumani ya Luther ambayo haikuwa imekamilika.

Chapa ya mwisho ya Van Liesvelt ya Kiholanzi ya 1542, ilikuwa na maelezo ya ziada na maandishi ya pambizoni. Kwa mfano, kando ya Mathayo 4:3, kulikuwa na picha ya Ibilisi akiwa mtawa wa kiume mwenye ndevu, akiwa na rozari na miguu ya mbuzi. Hata hivyo, maelezo ya pambizoni hasa ndiyo yaliyokasirisha Kanisa Katoliki. Elezo moja, lililosema “Wokovu unakuja kupitia Yesu Kristo pekee,” lilitumiwa kumhukumia kifo Van Liesvelt. Ingawa alijitetea kwamba Biblia yake ilichapishwa kwa heshima na ruhusa ya kanisa, alikatwa kichwa huko Antwerp, mwaka wa 1545.

Iliruhusiwa, Halafu Ikapigwa Marufuku

Wakati huohuo, huko Ufaransa mteteaji maarufu wa haki za binadamu aliyekuwa Mkatoliki, Jacques Lefèvre d’Étaples, alikuwa akitafsiri Biblia katika Kifaransa akitumia Biblia ya Kilatini, ingawa pia alitumia Biblia ya Kigiriki. D’Étaples alitaka watu wa kawaida wasome Biblia. Yeye aliandika hivi: “Wakati utakuja ambapo Kristo atahubiriwa kwa njia safi bila kuchanganywa na mapokeo ya wanadamu, jambo ambalo halifanywi sasa.” Mnamo mwaka wa 1523 alichapisha tafsiri ya Kifaransa ya “Agano Jipya” huko Paris. Wanatheolojia wa Chuo Kikuu maarufu cha Sorbonne, waliipinga tafsiri hiyo kwa sababu ilikuwa katika lugha ya kienyeji. Kwa sababu ya kushambuliwa, D’Étaples alitoroka Paris na kukimbilia Strasbourg kaskazini mashariki mwa Ufaransa.

Kwa sababu ya upinzani huo, wapiga chapa nchini Ufaransa hawakuthubutu tena kuchapa Biblia za Kifaransa. Basi D’Étaples angechapa Biblia yake wapi? Antwerp ndilo jiji lililofaa. Biblia yake ya mwaka wa 1530 ilichapwa huko Antwerp na Merten de Keyser na ilikuwa tafsiri ya kwanza ya Biblia nzima ya Kifaransa. Jambo la kupendeza ni kwamba De Keyser alitoa Biblia hiyo kwa ruhusa ya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Louvain, ambacho ni cha kale zaidi nchini Ubelgiji, na ya Maliki Mtakatifu Mroma Charles wa Tano mwenyewe! Hata hivyo, mnamo mwaka wa 1546 tafsiri ya D’Étaples iliwekwa kwenye orodha ya vitabu vilivyopigwa marufuku kwa wasomaji Wakatoliki.

“Askofu Alikuwa na Vitabu . . . Tyndale Alikuwa na Pesa”

Wakati huohuo, nchini Uingereza, kasisi William Tyndale, alitaka kutafsiri Biblia katika Kiingereza. Hata hivyo Askofu wa London, Cuthbert Tunstall, alimpinga vikali. Tyndale alipotambua kwamba hangeweza kutafsiri Biblia akiwa Uingereza, alitorokea Ujerumani. Hatimaye, mnamo Februari 1526, tafsiri yake ya kwanza ya Kiingereza ya “Agano Jipya” zima ilichapwa. Kabla mwezi mmoja haujapita, baadhi ya Biblia hizo zilifika Uingereza.

Hata hivyo, Askofu Tunstall aliazimia kuzuia watu wa kawaida wasisome Biblia. Hivyo, alichoma Biblia zote za tafsiri ya Tyndale alizopata. Na bado zilisambazwa. Kwa hiyo, askofu alipanga, kupitia mfanya-biashara mmoja aliyeitwa Packington, kununua Biblia zote za Tyndale kabla hazijafika Uingereza. Tyndale alikubali na akatumia pesa alizopata kuboresha tafsiri yake na akatoa chapa nyingine iliyosahihishwa. Mwandishi mmoja wa wakati huo alieleza: ‘Kwa hiyo maafikiano yao yakaleta matokeo mazuri, askofu alikuwa na vitabu, Packington alipata shukrani, na Tyndale alikuwa na pesa.’ Hivyo, askofu wa London aligharimia utafsiri wa Biblia ya Tyndale bila kujua!

Tyndale na Antwerp

Hata baada ya Biblia hizo zote kununuliwa na kuteketezwa, “Agano Jipya” la Tyndale liliendelea kuingizwa huko Uingereza kwa wingi. Hilo liliwezekanaje? Wapiga chapa wawili jasiri wa Antwerp, Hans na Christopher van Ruremond, walitoa chapa kadhaa za “Agano Jipya” la Tyndale walipokuwa mafichoni. Ingawa chapa hizo zilikuwa na makosa mengi ya uchapishaji, watu wa Uingereza walitaka sana kuzinunua.

Hata hivyo, Hans alifungwa huko London kwa kuchapisha nakala 1,500 za “Agano Jipya” za Tyndale na kuingiza nakala 500 huko Uingereza. Yaelekea Hans alikufa gerezani huko Uingereza. Mnamo mwaka wa 1531, ndugu yake Christopher pia alitiwa gerezani kwa kuuza “Agano Jipya.” Yaelekea naye alikufa gerezani.

‘Tafsiri Bora Zaidi ya Tyndale’ —Ilichapwa Antwerp

Kutoka mwaka wa 1529 hadi mwaka wa 1535, Tyndale alitumia muda wake mwingi jijini Antwerp, ambapo aliweza kufanya kazi yake vizuri zaidi. Ni huko ambako mnamo mwaka wa 1530, Merten de Keyser alichapa tafsiri ya vitabu vitano vya kwanza vya Biblia ya Tyndale, ambayo ilikuwa na jina Yehova kwa mara ya kwanza katika Kiingereza.

Mnamo Mei 1535, Tyndale alikamatwa huko Antwerp. Alipoteseka gerezani, mmoja wa wanafunzi wake, Miles Coverdale, alikamilisha tafsiri ya Tyndale ya Maandiko ya Kiebrania. Mnamo Oktoba 6, 1536, huko Vilvoorde, Ubelgiji, Tyndale alifungwa kwenye mti, akanyongwa na kuteketezwa. Maneno yake ya mwisho yalikuwa: “Bwana, fumbua macho ya Mfalme wa Uingereza!”

Urithi Alioacha Tyndale

Punde tu baada ya Tyndale kuuawa, Mfalme Henry wa Nane wa Uingereza aliruhusu tafsiri fulani ya Biblia isomwe makanisani. Tafsiri hiyo ilichapwa na Matthias Crom, mpiga chapa mwingine mashuhuri wa Antwerp. Sehemu kubwa ya Biblia hiyo, inayoitwa kwa ukawaida Biblia ya Matthew (jina hilo linatokana na jina la Thomas Matthew), ni tafsiri ya Tyndale. * Maaskofu sasa walitumia tafsiri ambayo walikuwa wameteketeza miaka michache mapema—iliyomfanya Tyndale auawe!

Sehemu kubwa ya tafsiri ya Tyndale inapatikana katika Biblia ya King James Version. Kwa hiyo, semi nyingi maarufu katika Biblia ya King James Version ambazo hutumiwa sana katika Kiingereza zilitokana na tafsiri ya Tyndale iliyopigwa chapa kwa mara ya kwanza huko Antwerp. Kulingana na Profesa Latré, Tyndale aliathiri lugha ya Kiingereza kuliko Shakespeare!

Mwishoni mwa miaka ya 1500, Antwerp lilipoteza uhuru wake wa kidini na nafasi yake ya kuwa kimbilio la wachapaji wa Biblia. Badiliko hilo lilisababishwa hasa na mnyanyaso uliofanywa na Kanisa Katoliki ili kupinga Mageuzo. Hata hivyo, ujasiri na kujidhabihu kwa wapiga chapa hao wa mapema wa Biblia katika Antwerp kumechangia sana kueneza Neno la Mungu kwa wasomaji wa Biblia ulimwenguni leo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Thomas Matthews huenda lilikuwa jina jingine la John Rogers, rafiki na mfanya-kazi mwenzi wa Tyndale.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Juu: Kupanga herufi kwa mkono; Martin Luther akitafsiri Biblia; ramani ya zamani ya jiji la Antwerp

[Picha katika ukurasa wa 20]

Duka la vitabu la Jacob van Liesvelt

[Picha katika ukurasa wa 21]

Jacques Lefèvre d’Étaples na ukurasa unaoonyesha kichwa cha chapa yake ya Biblia ya 1530, iliyochapwa Antwerp

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kuteketeza hadharani Biblia za Kiingereza huko London

[Picha katika ukurasa wa 22]

William Tyndale, ukurasa mmoja wa Biblia yake, na Miles Coverdale

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

Ukurasa wa 19: Mpiga-chapa: Printer’s Ornaments/by Carol Belanger Grafton/Dover Publications, Inc.; Luther: From the book Bildersaal deutscher Geschichte; ramani: By courtesy of Museum Plantin-Moretus/Stedelijk Prentenkabinet Antwerpen; ukurasa wa 21: Picha: From the book Histoire de la Bible en France; Ukurasa wa Biblia: © Cliché Bibliothèque nationale de France, Paris; kuchoma Biblia: From the book The Parallel Bible, The Holy Bible, 1885; ukurasa wa 22: Tyndale: From the book The Evolution of the English Bible; Coverdale: From the book Our English Bible: Its Translations and Translators