Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Namba Zinavutia?

Kwa Nini Namba Zinavutia?

Kwa Nini Namba Zinavutia?

HEBU wazia ulimwengu ungekuwaje bila namba. Hakungekuwa na pesa. Watu wangebadilishana mali kwa mali. Vipi michezo? Bila namba hatungeweza kujua mshindi au hata idadi ya wachezaji katika kila timu!

Hata hivyo, mbali na matumizi hayo muhimu ya namba, watu fulani huziona kuwa na ujumbe wa siri. Hiyo ni kwa sababu namba si halisi. Huwezi kuhisi au kushika namba. Kwa mfano: Tofaa lina rangi fulani hususa, ulaini, ukubwa, umbo, harufu, na ladha hususa. Unaweza kutofautisha tofaa, limau, mpira, au kitu kingine kwa kuchunguza kila moja ya sifa hizo. Hata hivyo, huwezi kutofautisha namba kwa njia hiyo. Huenda vitu saba vilivyowekwa pamoja visiwe vinafanana na vitu vingine saba—isipokuwa kwa idadi yake. Kwa hiyo, kujua maana ya namba—kwa mfano, kujua tofauti kati ya sita na saba—ni jambo linalowaziwa tu. Na ndiyo sababu watu huona namba kuwa na ujumbe wa siri.

Sayansi ya Uwongo Badala ya Fundisho la Pythagoras

Kwa kawaida, watu wa kale waliamini kwamba namba zina ujumbe wa pekee. Mwanafalsafa na mwanahisabati Mgiriki anayeitwa Pythagoras, aliyeishi katika karne ya sita K.W.K., alifundisha kwamba vitu vyote vinaweza kufafanuliwa kwa kutumia namba. Yeye na wafuasi wake walifundisha kwamba ulimwengu wote umepangwa kwa utaratibu na usawaziko. Basi je, kuna uwezekano wa kwamba vitu vyote vinategemea hesabu?

Tangu siku za Pythagoras, namba zimetumiwa kubashiri na kufasiri ndoto na kukumbuka mambo. Zimetumiwa na Wagiriki, Waislamu, na waumini wa Jumuiya ya Wakristo. Wayahudi waliofumbua mafumbo walitumia ubashiri wa namba unaoitwa gematria. Waliambatanisha kila moja ya zile herufi 22 za alfabeti ya Kiebrania na namba fulani kisha wakadai kwamba wamepata ujumbe wa siri kwenye Maandiko ya Kiebrania.

Wabashiri wanaotumia namba siku hizi wanatumia mbinu hiyohiyo. Mara nyingi, wao huanza na jina lako na tarehe uliyozaliwa. Namba fulani huambatanishwa na kila herufi ya jina lako. Mbashiri huongeza namba hizo na namba za mwezi na za tarehe uliyozaliwa ili kupata namba zako kuu. Kisha anatoa fasiri ya pekee ya namba hizo ambazo anadhani zinaeleza kila jambo kukuhusu—kutia ndani utu wako, mambo unayotamani, na mambo yatakayokupata wakati ujao.

Labda wengi huvutiwa sana na ubashiri huo kwa sababu unaonekana kuwa sahihi. Edward Albertson asema hivi katika kitabu chake Prophecy for the Millions: “Watu wengi wameamini ubashiri wa namba baada ya kuona kwamba ujumbe wa namba fulani unawafaa kabisa watu fulani ambao wamechunguzwa.” Hata hivyo, ubashiri huo wa kutumia namba umeitwa pia sayansi ya uwongo. Kwa nini? Je, kuna sababu zinazoweza kukufanya utilie shaka ubashiri huo?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

JE, BIBLIA INA UJUMBE WA SIRI?

Katika kitabu chake The Bible Code, mwandishi wa habari Michael Drosnin adai kwamba alipata ujumbe wa siri katika Maandiko ya Kiebrania kwa kutumia kompyuta. Drosnin alidai kwamba “ujumbe huo wa siri” ulikuwa na maneno haya, “mwuaji atakayeua” kisha akaona jina Yitzhak Rabin—na alipata ujumbe huo mwaka uliotangulia kuuawa kwa Waziri Mkuu wa Israel, Yitzhak Rabin.

Kitabu The Bible Code kilizusha ubishi fulani. Mwanahisabati na mwanafizikia anayeitwa Dave Thomas alionyesha kwamba habari yoyote inayochunguzwa na kompyuta inaweza kuwa na ujumbe unaoonekana kuwa wa kifumbo. Thomas alipochunguza Maandishi yaliyochunguzwa na Drosnin alipata maneno haya, “ujumbe wa siri,” “mpumbavu,” na “uwongo.” Thomas asema kwamba “ujumbe wa siri waweza kupatikana popote, maadamu uko tayari kutumia wakati wako na nguvu zako kuchunguza kila jambo linaloweza kutukia.”

Kompyuta inaweza kutumiwa kupata mchanganyo wa herufi fulani ambazo zinaweza kutumiwa kutabiri mambo fulani kwa sababu ina uwezo wa kupiga hesabu nyingi sana. Lakini hilo hutukia tu bila kutarajiwa na halithibitishi kwamba Biblia ina ujumbe wa siri. *

[Maelezo ya Chini]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Pythagoras alifundisha kwamba vitu vyote vinaweza kufafanuliwa kwa kutumia namba

[Hisani]

Courtesy National Library of Medicine