Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Siku ya Arusi Nilifurahia sana ule mfululizo wa makala kuu wenye kichwa “Siku ya Arusi Yenye Shangwe.” (Februari 8, 2002) Mimi ni kijana kwa hiyo najitayarisha kupiga hatua hiyo muhimu ya kufunga ndoa. Makala hizo zilinisaidia kujua jinsi ya kufanya matayarisho na kuepuka mfadhaiko unaowapata wenzi wengi na pia ulinifahamisha jinsi ya kufanya muungano huo uwe wenye furaha. Tafadhali endeleeni kutusaidia sisi ambao tunajitahidi kufanya yale ambayo Yehova anataka tufanye.

F. C., Italia

Sikuzote mimi hustaajabu sana kuona Yehova akiandaa mwongozo ninapouhitaji sana. Toleo la Amkeni! la Februari 8, 2002 lilikuja pia kwa wakati barabara. Mimi na mchumba wangu tumekuwa tukipanga ndoa yetu kwa miezi michache iliyopita, na tulikuwa tumeanza kuwa na wasiwasi. Makala za kwanza zilitukumbusha kwamba tunapaswa kuwa na shangwe katika miezi ya matayarisho kwa sababu mahangaiko hufadhaisha tu.

H. M., Australia

Ukurasa wa 10 wa mfululizo wa makala kuu wadokeza kwamba mume anaruhusiwa kuhama nyumbani ikiwa anaamini kwamba ana sababu halali za kutengana na mwenzi wake. Mimi na mke wangu hatuoni jambo lolote kwenye Biblia linalounga mkono wazo hilo. Kinyume chake, yaonekana kwamba mke ndiye anayeweza kuhama, lakini ni lazima mume abaki nyumbani. Andiko la Mwanzo 2:24 lasema kwamba mwanamume anapaswa ‘kuambatana na mkewe.’ Na andiko la 1 Wakorintho 7:11 lasema, “kwa kweli [mke]akiondoka,” kisha mstari huo waongezea kwamba, “mume hapaswi kumwacha mke wake.”

K. L. Australia

“Amkeni!” linajibu: Ni lazima andiko la Mwanzo 2:24 lichunguzwe katika muktadha wake. Mungu hakutoa agizo hilo kuwa mwongozo kwa wenzi wanaotaka kutengana. Barua ya Paulo kwa Wakorintho inaonyesha wazi kwamba Yehova anaheshimu sana ndoa, na ni lazima wenzi wa ndoa wafanye yote wawezayo ili kudumisha ndoa yao. Hata hivyo, yaonekana kwamba Paulo hakuwa na nia ya kuweka kanuni mbili—moja ya mke na nyingine ya mume. Mstari wa 10 na wa 11 unawahimiza mume na mke wasitengane, ikiwezekana. Kwa hiyo, maagizo yanayomhusu mke yanamhusu mume pia.

Kea Nilifurahi sana na kuangua kicheko niliposoma makala yenye kichwa “Kea—Kasuku wa Milimani Apendaye Kucheza.” (Februari 8, 2002) Kwa kweli Yehova ni Mungu mwenye furaha! Ni Muumba mwenye upendo tu anayeweza kuumba kiumbe anayewafurahisha sana wanadamu. Ninatazamia siku ambayo nitamjua kwa undani zaidi ndege huyo mwenye kuchekesha anayeitwa kea. Asanteni sana kwa ajili ya makala hiyo na kwa ajili ya makala nyingine zenye kuvutia na zenye kuimarisha imani mnazoandika.

R. R., Ujerumani

Muda mfupi tu baada ya mume wangu kuniacha, nilipokea gazeti la Amkeni! la Februari 8, 2002. Haikuwa rahisi kwangu kukubaliana na picha ya jalada kuhusu siku ya arusi. Nilijiuliza hivi, ‘Kwa nini mimi na mume wangu hatungeweza kuwa na furaha kama wenzi walio kwenye jalada hilo?’ Hata hivyo, niliposoma makala juu ya yule kasuku anayeitwa kea kwenye gazeti hilo, niliangua kicheko. Sikumjua kamwe ndege huyo mwenye kupendeza! Moyo wangu ulisisimuka sana. Ni kana kwamba Yehova alikuwa akinitia moyo kwa kuniambia hivi: “Furahia maisha!” Asanteni sana.

M. Y., Japan