Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Mzazi Wangu Hanipendi?

Mbona Mzazi Wangu Hanipendi?

Vijana Huuliza . . .

Mbona Mzazi Wangu Hanipendi?

“Kabla ya baba yangu kumtaliki mama, tulikuwa tukienda ufuoni, kwenye mikahawa, na kutembelea sehemu mbalimbali kwa gari lake. Kisha mambo yote hayo yakaisha kabisa. Baba alibadilika. Nadhani alinitaliki pia.”—Karen. *

VIJANA wengi sana huhisi hivyo. Kama Karen, wao huona kwamba mzazi wao ameacha kuwapenda—au hakuwapenda kamwe. Hatuzungumzii zile hisia mbaya ambazo hutokea kwa sababu ya vijana na wazazi kutoelewana kwa muda mfupi; wala hatuongei kuhusu kukasirika ambako hutokea mara kwa mara kwa sababu ya kutiwa nidhamu na mzazi. Badala yake, katika visa fulani, wazazi huwapuuza watoto kabisa, hawawajali wala kuwatia nidhamu. Katika visa vingine, watoto hunyanyaswa vikali labda kwa kutukanwa au kupigwa.

Kukataliwa na mzazi ni jambo linaloumiza sana. Karen anasema hivi: “Jambo hilo lilifanya nihisi nimepuuzwa na kwamba sipendwi.” Ikiwa umewahi kupatwa na hali hiyo ngumu, hebu fikiria baadhi ya madokezo ya kukabiliana na hisia zako. Uwe na hakika kwamba hata kama mzazi wako ataacha kukutegemeza, unaweza kufaulu maishani!

Kumwelewa Mzazi Wako

Kwanza, mzazi wako ana wajibu wa kukupenda. Upendo wa mzazi kwa mtoto wake unapaswa kuwa wa kweli na wa kudumu. Mungu anataka wazazi wawe na upendo wa aina hiyo. (Wakolosai 3:21; Tito 2:4) Kwa hiyo mbona wazazi nyakati nyingine huwapuuza, huwaacha, au kuwanyanyasa watoto wao?

Jambo moja linaloweza kusababisha hali hiyo ni mambo waliyokabili maishani. Jiulize, ‘Wazazi wangu walijuaje jinsi ya kulea watoto?’ Mara nyingi wazazi hujua jinsi ya kulea watoto kutokana tu na jinsi wao wenyewe walivyolelewa na wazazi wao. Katika ulimwengu huu wenye taabu na ambao una watu wengi sana “wasio na shauku ya kiasili,” mara nyingi mbinu za kulea watoto huwa na kasoro. (2 Timotheo 3:1-5) Nyakati nyingine, kasoro hizo hurudiwa, na wazazi huwanyanyasa watoto wao kama walivyonyanyaswa pia.

Isitoshe, wazazi wanaweza kukasirishwa na mambo mbalimbali. Wazazi fulani hujaribu kuepuka majonzi na mfadhaiko kwa kujishughulisha sana na kazi, kunywa pombe kupita kiasi, au kutumia dawa za kulevya. Kwa mfano, baba ya William na Joan alikuwa mlevi. “Baba yangu hakuwa akitupongeza,” asema Joan. “Hata hivyo, jambo baya zaidi ni kwamba alikuwa mwenye hasira alipoanza kunywa pombe. Alikuwa akimpigia mama kelele usiku kucha. Niliogopa sana.” Hata wazazi wasipoonyesha ujeuri wao waziwazi, mazoea yao yanaweza kuwachosha sana kiasi cha kutowapenda watoto wao na kuwapuuza.

William anafikiri kwamba anaelewa kile kilichomfanya baba yake awe na tabia hiyo yenye kubadilika-badilika. William anaeleza hivi: ‘Baba yangu alilelewa huko Berlin, Ujerumani, wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Alipokuwa mvulana, aliona mambo mengi yenye kuogopesha na mauaji mengi. Ilimbidi ajikakamue kila siku ili apate chakula. Naona kwamba baba yangu aliathiriwa sana na mambo aliyokabili maishani.’ Naam, Biblia hukubali kwamba watu wanaodhulumiwa sana wanaweza kutenda bila kufikiri.—Mhubiri 7:7.

Je, William na Joan wanaona kwamba ilikuwa sawa kudhulumiwa na baba yao eti kwa sababu alikabili hali ngumu? “La,” asema William. “Hali ambazo baba alikabili hazifanyi mwenendo wake mbaya na zoea lake la ulevi kuwa sawa. Hata hivyo, kuelewa mambo yaliyompata baba kumenisaidia kumwelewa vizuri zaidi.”

Kutambua kwamba wazazi wako si wakamilifu na kujua jinsi maisha yao yalivyokuwa kunaweza kukusaidia sana uwaelewe. Mithali 19:11 inasema: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.”

Kukabiliana na Hisia Zako

Hali ya nyumbani inaweza kukufanya uwe na hisia nyingine mbaya. Kwa mfano, Patricia alihisi kwamba “hafai wala hapendwi” kwa sababu ya kupuuzwa na wazazi wake. LaNeisha aliona ni vigumu kuwaamini wanaume baada ya baba yake kuondoka nyumbani alipokuwa na umri wa miaka minane tu. Na Shayla alitamani kupendwa na mtu yeyote yule, ili kuziba pengo lililoachwa na mama yake aliyezoea kutumia “dawa za kulevya.”

Pia, huenda kukawa na matatizo kwa sababu ya hasira na wivu. Karen aliona “wivu sana wakati fulani” alipoona baba yake, ambaye alikuwa ameoa tena, akipendezwa na familia yake mpya badala ya kumpenda yeye. Nyakati nyingine, Leilani hata aliwachukia wazazi wake. Anasema hivi: “Nilibishana nao kila wakati.”

Kwa kufikiria hali hizo, inaeleweka ni kwa nini watu huhisi hivyo. Lakini, unawezaje kukabiliana ifaavyo na hisia hizo mbaya? Hebu fikiria madokezo yafuatayo.

Mkaribie Yehova Mungu. (Yakobo 4:8) Unaweza kufanya hivyo kwa kusoma Biblia kila siku na kushirikiana kwa ukawaida na watu wake. Unapoona jinsi Yehova anavyoshughulika na wengine, utafahamu kwamba yeye ni mwaminifu. Unaweza kumtumaini. “Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake?” Yehova akawauliza Waisraeli. “Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe,” ndivyo alivyoahidi. (Isaya 49:15) Kwa hiyo, sali kwa Mungu kwa ukawaida. Usiwe na wasiwasi kuhusu maneno utakayotumia. Anakuelewa. (Waroma 8:26) Tambua kwamba Yehova anakupenda hata inapoonekana kwamba hakuna mwingine anayekupenda.—Zaburi 27:10.

Zungumza na mtu mzima unayemwamini. Pata marafiki waliokomaa kiroho. Watajie hisia zako na mahangaiko yako waziwazi. Katika kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, unaweza kupata akina baba na akina mama wa kiroho. (Marko 10:29, 30) Hata hivyo, huenda ukahitaji kuchukua hatua ya kwanza kuwaeleza hisia zako waziwazi. Wengine hawawezi kujua jinsi unavyohisi usipowaeleza. Unaweza kufarijiwa sana unapofunua moyo wako.—1 Samweli 1:12-18.

Jishughulishe kwa kuwasaidia wengine. Ili kuepuka kujisikitikia, jitahidi kutofikiria sana hali mbaya unayokabili. Badala yake, jitahidi kuthamini yale uliyo nayo. Jitahidi kufanikiwa kwa njia mbalimbali kwa ‘kufuliza kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yako mwenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ (Wafilipi 2:4) Weka miradi ya kiroho, kisha ujitahidi kuifikia ukiwa na imani kwamba utafaulu. Kuwatumikia wengine katika huduma ya Kikristo ni njia bora ya kuwafikiria wengine badala ya kujifikiria.

Endelea kuwaheshimu wazazi wako. Sikuzote na ukumbuke kutii kanuni na viwango vya Biblia. Hiyo inatia ndani kuwaheshimu wazazi wako. (Waefeso 6:1, 2) Ukiwaheshimu, hutataka kamwe kulipiza kisasi. Kumbuka, hata ukiona kuwa mzazi wako amekosea, hiyo haikupi ruhusa ufanye makosa. Kwa hiyo acha Yehova ashughulikie mambo hayo. (Waroma 12:17-21) Yeye “hupenda haki” na anapenda sana kuwalinda watoto. (Zaburi 37:28; Kutoka 22:22-24) Unapoendelea kuwaheshimu wazazi wako, jaribu kusitawisha matunda ya roho ya Mungu—na zaidi ya yote, tunda la upendo.—Wagalatia 5:22, 23.

Unaweza Kufaulu

Bila shaka mtoto huumia sana anapokosa kupendwa na mzazi. Lakini makosa ya mzazi hayapasi kubadili utu wako. Unaweza kupata heri na fanaka maishani ukifuata kanuni za Biblia zilizotajwa.

William, aliyenukuliwa hapo awali, amejitolea kufanya kazi wakati wote katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Yehova ametupatia misaada mingi ili kutuwezesha kukabiliana na hali hizo ngumu. Ni pendeleo lililoje kuwa na Baba wa mbinguni mwenye upendo na mwenye kujali!” Dada yake, Joan, ni painia, anayetumikia wakati wote mahali ambapo kuna uhitaji mkubwa wa wahubiri. Joan anasema hivi: “Tulipoendelea kukua, tuliona tofauti iliyo wazi ‘kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.’” (Malaki 3:18) “Mambo tuliyojionea maishani yalituimarisha kuipigania kweli na kuifanya iwe mali yetu.”

Hata wewe unaweza kufanikiwa. Biblia inasema hivi: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.” (Zaburi 126:5) Mstari huu unatumikaje hapa? Ukijitahidi kutumia kanuni zinazofaa katika hali ngumu, badala ya kulia machozi utafurahia baraka ya Mungu hatimaye.

Kwa hiyo, endelea kujitahidi kumkaribia Yehova Mungu. (Waebrania 6:10; 11:6) Hata ikiwa umetaabika, umefadhaika, na kuhisi hatia kwa miaka mingi, hisia hizo zinaweza kwisha pole kwa pole na badala yake unaweza kupata “amani ya Mungu izidiyo fikira yote.”—Wafilipi 4:6, 7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

Je, Unahisi . . .

• Kwamba hufai kamwe?

• Kwamba haifai wala si jambo la busara kuwaamini wengine?

• Kwamba unahitaji kutiwa moyo kila wakati?

• Kwamba huwezi kudhibiti hasira au wivu?

Iwapo jibu lako kwa maswali hayo ni ndiyo, zungumza upesi iwezekanavyo na mzazi mwenye kutumainika, mzee, au rafiki aliyekomaa kiroho.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Chukua hatua zinazofaa kukabiliana na hisia zako