Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Imani Inategemea Vitu vya Kale Vilivyochimbuliwa?

Je, Imani Inategemea Vitu vya Kale Vilivyochimbuliwa?

Maoni ya Biblia

Je, Imani Inategemea Vitu vya Kale Vilivyochimbuliwa?

Mnamo mwaka wa 1873 kasisi Mwingereza Samuel Manning aliandika hivi kuhusu Yerusalemu: “Wasafiri wa kidini kutoka ulimwenguni pote huvutiwa na mahali hapa. Kuta zinazokaribia kubomoka, barabara zenye harufu mbaya, na mabaki ya nyumba za kale, huvutia sana mamilioni ya watu wenye staha ya kidini, kuliko sehemu nyingine yoyote duniani.”

NCHI Takatifu imewavutia watu wengi tangu wakati wa Maliki Mroma Konstantino. * Kwa miaka 1,500 hivi, wasafiri wa kidini wametembelea Nchi hiyo Takatifu. Hata hivyo,ilikuwa mwanzoni mwa karne ya 19 ndipo wasomi walipoandamana na wasafiri wengine wa kidini, na kuanza kuchimbua vitu vya kale vya nyakati za Biblia—kwa madhumuni ya kuchunguza maisha ya watu wa kale, sehemu mbalimbali, na lugha za Nchi Takatifu.

Uchunguzi wa vitu vya kale vilivyofukuliwa ardhini umeongeza uelewevu wa mambo mbalimbali ya nyakati za Biblia. Pia, vitu vilivyochimbuliwa vimepatana mara nyingi na matukio ya Biblia. Je, uelewevu huo ni wa lazima katika imani ya Kikristo? Ili tujibu swali hilo, hebu tuchunguze jiji la Yerusalemu na hekalu lake, ambalo limekuwa kitovu cha uchimbuzi mwingi wa vitu vya kale.

‘Jiwe Halitaachwa Juu ya Jiwe’

Mnamo Nisani 11, kulingana na kalenda ya Kiyahudi, kwenye majira ya kuchipua ya mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo aliondoka kwenye hekalu la Yerusalemu kwa mara yake ya mwisho, akiandamana na baadhi ya wanafunzi wake. Walipoelekea kwenye mlima wa Mizeituni, mwanafunzi mmoja alimwambia Yesu: “Mwalimu, ona! namna ya mawe na namna ya majengo!”—Marko 13:1.

Wayahudi hao waaminifu walikuwa na upendo mwingi kwa Mungu na hekalu lake. Walijivunia majengo hayo yenye fahari na mapokeo ambayo hekalu hilo liliwakilisha kwa miaka 1,500. Yesu alitoa jibu lenye kushtua: “Waona majengo makubwa haya? Kwa vyovyote jiwe halitaachwa hapa juu ya jiwe lisitupwe chini.”—Marko 13:2.

Mungu angewezaje kuruhusu hekalu lake liharibiwe, na Mesiya alikuwa amewasili tayari? Kwa msaada wa roho takatifu, wanafunzi wa Yesu wangeelewa sababu yenyewe pole kwa pole. Hata hivyo, maneno ya Yesu yanahusuje uchimbuzi wa vitu vya nyakati za Biblia?

Jiji “Jipya”

Katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., taifa la Kiyahudi lilipoteza kibali cha Mungu. (Mathayo 21:43) Hilo lilitoa nafasi kwa ajili ya serikali ya mbinguni ambayo ingeleta baraka kwa wanadamu wote. (Mathayo 10:7) Kama Yesu alivyokuwa ametabiri, jiji la Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa katika mwaka wa 70 W.K. Uchimbuzi wa vitu vya kale unaunga mkono simulizi la Biblia la tukio hilo. Hata hivyo, imani ya Wakristo haitegemei kuchimbuliwa kwa magofu ya hekalu hilo la kale. Imani yao inategemea jiji tofauti, Yerusalemu jingine.

Mnamo mwaka wa 96 W.K., mtume Yohana, ambaye alisikia Yesu akitoa unabii kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake na akaona utimizo wa unabii huo, aliona njozi ifuatayo: “Nikaona pia jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likiteremka kutoka mbinguni kwa Mungu.” Sauti kutoka kiti cha ufalme ilisema: “Atakaa pamoja nao [wanadamu], nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.”—Ufunuo 21:2-4.

“Jiji” hilo limefanyizwa na Wakristo waaminifu ambao watatawala pamoja na Kristo huko mbinguni. Wakiwa pamoja wanafanyiza serikali ya mbinguni—Ufalme wa Mungu—ambayo itatawala dunia, na kuwarudishia wanadamu wote ukamilifu wakati wa kipindi cha miaka elfu moja. (Mathayo 6:10; 2 Petro 3:13) Wakristo Wayahudi wa karne ya kwanza ambao wangekuwa sehemu ya kikundi hicho walitambua kwamba kitu chochote walichokuwa nacho katika mfumo wa Kiyahudi, hakingelingana na pendeleo la kutawala na Kristo mbinguni.

Akirejelea cheo chake kikubwa alipokuwa katika dini ya Kiyahudi, mtume Paulo aliandika hivi kwa niaba yao wote: “Vitu vilivyokuwa mapato ya faida kwangu, hivyo nimeviona kuwa hasara kwa sababu ya Kristo. Naam, kama ilivyo, kwa kweli naona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani iliyo bora zaidi ya ujuzi wa Kristo Yesu Bwana wangu.”—Wafilipi 3:7, 8.

Kwa sababu mtume Paulo aliheshimu sana Sheria ya Mungu na mpango wa hekalu, bila shaka maneno yake hayadokezi kwamba mpango huo wa Mungu ulipaswa kudharauliwa. * (Matendo 21:20-24) Paulo alikuwa akionyesha kwamba mpango wa Kikristo ulikuwa bora kuliko ule wa Kiyahudi.

Bila shaka mtume Paulo na Wakristo wengine Wayahudi wa karne ya kwanza walijua mambo mengi hususa ya kusisimua kuhusu mfumo wa Kiyahudi. Kwa vile uchimbuzi wa vitu vya kale hufunua mambo ya kale, Wakristo wanaweza kufaidika kwa kuelewa baadhi ya mambo hayo. Hata hivyo, ona mambo ambayo Paulo alimweleza kijana Timotheo ayazingatie: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya [kuhusu kutaniko la Kikristo]; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.”—1 Timotheo 4:15.

Uchimbuzi wa vitu vya nyakati za Biblia umepanua uelewevu wetu wa matukio katika Biblia. Hata hivyo, Wakristo wanajua kwamba imani yao haitegemei uthibitisho unaotokana na uchimbuzi wa wanadamu, bali inategemea Neno la Mungu, Biblia.—1 Wathesalonike 2:13; 2 Timotheo 3:16, 17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Konstantino na mama yake, Helena, walipenda kujionea sehemu mbalimbali takatifu za Yerusalemu. Mama ya Konstantino alitembelea Yerusalemu. Kwa karne nyingi zilizofuata, watu wengine wengi walifuata nyayo zake.

^ fu. 15 Kwa muda fulani, Wakristo Wayahudi wa karne ya kwanza huko Yerusalemu walifuata mambo fulani-fulani ya Sheria ya Kimusa, yamkini kwa sababu zifuatazo. Sheria ilitoka kwa Yehova. (Waroma 7:12, 14) Tayari ilikuwa desturi ya Wayahudi. (Matendo 21:20) Ilikuwa sheria ya taifa, na hivyo kuipinga kungeleta upinzani usio wa lazima kwa ujumbe wa Kikristo.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Juu: Yerusalemu katika mwaka wa 1920; Sarafu ya Kiroma iliyotumiwa na Wayahudi, mwaka wa 43 W.K.; machanuo ya komamanga yaliyotengenezwa kwa pembe za tembo, yamkini kutoka kwa hekalu la Solomoni, karne ya nane K.W.K.

[Hisani]

Ukurasa wa 2 na 18: Sarafu: Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority; komamanga: Courtesy of Israel Museum, Jerusalem