Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi

Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi

Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi

“Nina uchungu mwingi moyoni. Mimi hujifungia kwenye bafu mara nyingi nikilia usiku kucha. Mambo ni magumu.” —JANET, MAMA ASIYE NA MUME, MWENYE WATOTO WATATU.

KUNA sababu nyingi zinazofanya familia ziwe na mzazi mmoja tu. Familia kadhaa hubaki na mzazi mmoja tu kwa sababu ya vita, misiba ya asili, au magonjwa.

Wazazi fulani huamua kutooana. Kwa mfano, huko Sweden karibu nusu ya watoto huzaliwa na akina mama ambao hawajaolewa. Talaka pia inafanya familia nyingine zibaki na mzazi mmoja tu. Makadirio yanaonyesha kwamba zaidi ya nusu ya watoto Wamarekani wataishi katika familia zenye mzazi mmoja tu kwa muda fulani katika utoto wao.

Kuelewa Magumu

Hali ya akina mama ambao wamefiwa na waume zao hivi karibuni ni ngumu zaidi. Itawabidi kuanza kutunza familia zao huku wakiomboleza kifo cha waume zao. Inaweza kuchukua miezi kadhaa, hata miaka, kwa mama hao kuzoea wajibu huo, huku wakikabili magumu ya kiuchumi na daraka la kuwafariji watoto wao. Inaweza kuwa vigumu sana kwa mama aliye mjane kutekeleza madaraka hayo ya ziada. Huenda hali hiyo ikamfanya mtoto asitunzwe wala kuongozwa ifaavyo ijapokuwa anahitaji sana msaada na kutiwa moyo.

Mama wengi ambao hawajaolewa na baba ya mtoto wao ni wachanga na hawana ustadi mwingi. Huenda walilazimika kuacha shule. Kwa sababu ya kukosa elimu nzuri, wengi wao ni maskini nao hufanya kazi za mshahara mdogo. Ikiwa watu wa ukoo, kama vile wazazi wao, hawawezi kuwasaidia, itawabidi wapate mtu wa kumtunza mtoto wanapokwenda kazini. Huenda mama asiyeolewa akalemewa pia na aibu na upweke. Huenda wengine wakahofia kwamba hawataweza kupata mume kwa sababu wana mtoto. Watoto wanaolelewa na mzazi mmoja wanapokua, wanaweza kusumbuka kwa kujiuliza maswali kumhusu mzazi yule mwingine na kuhisi kwamba wanahitaji kupendwa naye.

Hali kadhalika, wazazi waliotalikiwa wana mfadhaiko mwingi sana. Baadhi ya wazazi huwa na hasira nyingi kwa sababu ya talaka. Wazazi fulani wanaona vigumu kufikiria mahitaji ya kihisia ya watoto wao kwa sababu wao wenyewe wanahisi kwamba hawafai na kwamba wametupwa. Akina mama, wanaolazimika kufanya kazi ya kuajiriwa kwa mara ya kwanza, huenda wakaona vigumu kushughulikia madaraka yote ya familia. Huenda wakahisi kwamba hawana wakati wala nguvu za kutosha kufikiria mahitaji hayo ya watoto wao. Kwa hiyo itawabidi watoto wakabili mabadiliko makubwa maishani mwao peke yao baada ya talaka ya wazazi.

Magumu Ambayo Wazazi Waliotalikiwa Hukabili

Wazazi wasio na wenzi wa ndoa hutambua kwamba mahitaji ya kila mtoto ni tofauti nayo hubadilika daima. Wazazi ambao wametalikiwa hukabili magumu yasiyo ya kawaida wanapojitahidi kuwapa watoto wao mwongozo wa kiroho.

Kwa mfano, baadhi ya wazazi walio Mashahidi wa Yehova ambao wametalikiwa hawakupewa haki ya kulea watoto wao. Wao wamejitahidi kupanga watoto wao wawatembelee wakati wanapoweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja. Hivyo, mtoto anaweza kushirikiana na ndugu na dada katika kutaniko la Kikristo kwa ukawaida, jambo ambalo huwanufaisha sana watoto wa wazazi waliotalikiana.

Itawabidi wazazi waliotalikiana wasio na nafasi nyingi za kuwa pamoja na watoto wao watafute njia nyingine za kuwaonyesha kwamba wanawapenda. Ili kufaulu, ni lazima mzazi atambue na kuhangaikia hisia za moyoni za mtoto zinazobadilika-badilika. Jambo hilo ni muhimu hasa mtoto anapofikia umri wa kubalehe na anapoanza kupendezwa zaidi na ushirika wa watu wengine na marafiki.

Mzazi ambaye amefaulu kulea mtoto wake huelewa uwezo, utu, na mawazo yake. (Mwanzo 33:13) Mzazi huyo huwa na uhusiano wa karibu na mtoto wake, nao huongea na kushirikiana kwa upendo. Wanaweza kuongea bila kizuizi chochote. Mtoto hushiriki katika shughuli za mzazi, na mzazi hushiriki katika shughuli za mtoto.

Kuelewana Ni Muhimu

Baada ya talaka, watoto wanahitaji kushirikiana na wazazi wote wawili. Vipi ikiwa wazazi wana imani tofauti, mmoja ni Shahidi wa Yehova, na yule mwingine si Shahidi? Kuzungumza mambo waziwazi na kwa ukawaida husaidia kuzuia mgongano. ‘Mwe na sifa ya kuwa wenye kukubali sababu,’ mtume Paulo aliandika. (Wafilipi 4:5, Phillips) Watoto wanapaswa kufundishwa kwamba wazazi wote wawili wana haki ya kufuata dini yao.

Huenda mzazi asiye Shahidi akasisitiza mtoto ahudhurie ibada katika kanisa lake. Mzazi ambaye ni Shahidi wa Yehova anaweza kufanya nini katika hali hiyo? Yeye pia anaweza kumfundisha mtoto imani yake. Baadaye, mtoto ataweza kufanya uamuzi wake mwenyewe kuhusu ibada, kama kijana Timotheo, ambaye alifundishwa kanuni za Biblia na mama na nyanya yake. (2 Timotheo 3:14, 15) Mtoto akisumbuka kwa sababu ya kuhudhuria ibada ya dini nyingine, anaweza kufikiria kisa cha Naamani. Biblia inaeleza kwamba mtu huyo, hata baada ya kuwa mwabudu wa kweli, aliendelea kutimiza wajibu wake kwa kuambatana na mfalme aliyeabudu katika nyumba ya Rimoni. Huenda simulizi hilo likamhakikishia mtoto kwamba Yehova anamwelewa na kumpenda ijapokuwa yeye huhudhuria ibada nyingine ambayo hajazoea.—2 Wafalme 5:17-19.

Mzazi mzuri anajua jinsi ya kuongoza fikira za mtoto au watoto na kuelewa hisia zao. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Ni kweli kwamba wazazi wasiooa au kuolewa huenda wakaaibikia maisha yao ya awali. Hata hivyo, ni lazima wazazi hao wakumbuke kwamba watoto wana wazazi wawili. Watoto wanataka kuwajua wazazi wote wawili, na wanahitaji kujua kwamba wazazi wanawapenda. Na wanahitaji pia kujua kwamba kuzaliwa kwao hakukuwa tukio baya lisilotazamiwa. Kwa kusema kwa heshima juu ya yule mzazi mwingine na kujibu maswali yake kwa njia ambayo mtoto wa umri wake anaweza kuelewa, au anahitaji kujua, mzazi anaweza kumliwaza mtoto kwa upendo.

Wazazi wanapaswa kukumbuka kwamba maoni ya mtoto kuhusu upendo, mamlaka, na nguvu hutegemea uhusiano wake pamoja na mzazi wake. Kwa kutumia mamlaka na nguvu kwa njia ya upendo mzazi Mkristo anaweza kumsaidia sana mtoto kumpenda Yehova na kuheshimu utaratibu uliopo katika kutaniko.—Mwanzo 18:19.

Ni Lazima Watoto Wasaidie

Watoto wanaolelewa na mzazi mmoja tu wanahitaji pia kuelewa kwamba ni lazima wawe tayari kusaidia ili familia yao ifanikiwe. (Waefeso 6:1-3) Kwa kumtii mzazi wao wanaonyesha kwamba wanampenda na kutambua kwamba mzazi huyo anajitahidi sana kufanya familia yao iwe na amani na furaha. Mawasiliano mazuri yanaweza kudumishwa tu ikiwa watoto watatambua kwamba wanahitaji kuunga mkono jitihada za mzazi za kuendeleza mawasiliano.—Mithali 1:8; 4:1-4.

Watoto katika familia yenye mzazi mmoja hutakiwa mara nyingi kujifunza kazi mbalimbali mapema kuliko watoto wanaolelewa na wazazi wawili. Wanapofundishwa kwa upendo na subira, wavulana na wasichana watakuwa wenye kujistahi na kujiamini wanapojifunza kushughulikia madaraka ya maisha kwa mafanikio wakiwa wenye umri mdogo. Pia, watoto wanaweza kukabidhiwa kazi fulani za nyumbani ili wasaidie kudumisha utaratibu nyumbani.

Jambo hilo halimaanishi kwamba wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanataka watoto wao wajiamulie mambo kana kwamba wao ni watu wazima wasiohitaji mwongozo wowote kutoka kwa mzazi. Si jambo la hekima kumwacha mtoto mdogo peke yake au bila mtu wa kumtunza.

Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa hufikiri kwa makosa kwamba inawabidi kuwa marafiki tu wa watoto wao. Ijapokuwa uhusiano wa karibu ni wa lazima, wazazi hao wanapaswa kukumbuka kwamba watoto wanahitaji mzazi na mtoto hana ukomavu wa kutosha ili awe rafiki au msiri wa mzazi. Watoto wako wanataka utende kama mzazi.

Wazazi wasio na wenzi wa ndoa na watoto wao wanaposhirikiana na kuwa na uhusiano wa karibu wanaweza kujenga familia yenye furaha. Kwa sababu idadi ya watoto wanaolelewa na mzazi mmoja inaongezeka, watu wote wanapaswa kutambua magumu ambayo wazazi hao na watoto wao hukabili na kuwa tayari kuwasaidia na kuwatia moyo kwa upendo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Jinsi Watoto Wanavyoathiriwa

Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa hawawezi kutumia wakati mwingi pamoja na kila mtoto kama wazazi wawili. Nyakati nyingine mzazi asiye na mwenzi wa ndoa huishi pamoja na mtu ambaye si mume wake au mke wake. Hata hivyo, watu wengi wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa hutengana kuliko wale waliofunga ndoa. Kwa hiyo, yaelekea watoto katika familia hizo watakuwa wameishi na watu wazima wengi tofauti-tofauti utotoni mwao.

Kulingana na uchunguzi kadhaa, “kwa wastani, watoto wanaolelewa na mzazi mmoja tu wanaelekea kuwa na matatizo mengi ya maadili na kihisia kuliko watoto wanaolelewa katika familia za wazazi wawili.” Hata hivyo, uchunguzi wa kindani unaonyesha kwamba mapato ya chini ndiyo “yanayofanya watoto kutoka familia mbalimbali watofautiane kuhusiana na mwenendo na maendeleo.” Bila shaka jambo hilo halimaanishi kwamba watoto wanaolelewa na mzazi mmoja hawawezi kufaulu. Wakipata mwongozo na mazoezi yanayofaa wanaweza kushinda hali ngumu.