Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini Zakutana Huko Assisi Kutafuta Amani

Dini Zakutana Huko Assisi Kutafuta Amani

Dini Zakutana Huko Assisi Kutafuta Amani

“Ujeuri hautakuwapo tena! Vita haitakuwapo tena! Ugaidi hautakuwapo tena! Katika jina la Mungu, kila dini na ilete haki na amani, msamaha na uhai, na upendo!”—Papa John Paul wa Pili.

ASSISI, ITALIA, Januari 24, 2002—Wajumbe wa dini mbalimbali ulimwenguni walikusanyika kuombea amani, amani ambayo inatishwa na ugaidi, chuki, na ukosefu wa haki. Mkutano huo ulitangazwa na papa miezi miwili baada ya shambulizi la yale Majengo Mawili huko New York City. Viongozi wengi wa kidini walikubali mwaliko wa Vatikani kwa shauku nyingi.

Mara mbili kabla ya wakati huo, papa alikuwa ametayarisha mikutano ya kuombea amani kwenye mji huo wa Italia—kwanza katika mwaka wa 1986 kisha mwaka wa 1993. * Zaidi ya waandishi wa habari elfu moja kutoka kote ulimwenguni walifika kwenye mkutano huo wa mwaka wa 2002. Dini nyingi ziliwakilishwa katika mkutano huo—kulikuwa na wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo (Wakatoliki, Walutheri, Waanglikana, Waothodoksi, Wamethodisti, Wabaptisti, Wapentekoste, wafuasi wa Mennonite, wafuasi wa Jamii ya Marafiki, na wengineo), Waislamu, Wahindu, Wakonfyushasi, Makalasinga, Wajaini, wafuasi wa Tenrikyo, Wabudha, wafuasi wa Dini ya Kiyahudi, wafuasi wa dini za kiasili za Afrika, Washinto, na Wazoroasta. Pia, kulikuwa na wajumbe wa dini nyingine, na mwakilishi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Matangazo ya Amani

“Gari-moshi la amani” lilianza safari saa 2:40 asubuhi kutoka kituo kidogo cha Vatikani. Gari-moshi hilo lilikuwa na mabehewa saba yenye kustarehesha, na lilisindikizwa na helikopta mbili za ulinzi. Iliwachukua muda wa saa mbili kufika Assisi. Kulikuwa na ulinzi mkali—polisi wapatao elfu moja walikaa chonjo.

Viongozi hao wa kidini walikusanyika katika uwanja mmoja wa zamani uliokuwa na hema kubwa. Ndani ya hema, wajumbe waliketi kwenye jukwaa kubwa jekundu lenye muundo wa herufi ya V, na kiti cha papa kiliwekwa katikati. Kando ya jukwaa, kulikuwa na mzeituni—ishara ya amani. Wageni mashuhuri zaidi ya 2,000 waliketi mbele ya jukwaa. Maafisa wa cheo cha juu wa Italia waliketi katika mstari wa mbele. Kwaya zenye kusisimua sana ziliimba nyimbo za kutukuza amani baada ya hotuba mbalimbali. Katika sehemu nyingine za mji, maelfu ya watu, hasa vijana, walibeba maandishi makubwa ya kulaani vita yaliyoandikwa kwa lugha mbalimbali na kuimba nyimbo za amani. Wengi wao walibeba matawi ya mizeituni.

Papa aliingia jukwaani na kuwakaribisha wajumbe wa dini mbalimbali. Halafu, baada ya wimbo wa Kilatini uliotegemea andiko la Isaya 2:4—ambalo linatabiri kuhusu wakati ambapo “taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine”—wajumbe mbalimbali waliovalia mavazi rasmi ya kidini, walisimama na kila mmoja akatoa tangazo la amani. Yafuatayo ni baadhi ya matangazo hayo.

“Katika pindi hii muhimu wanadamu wanataka kuona matendo ya amani na kusikia maneno ya tumaini.”—Kadinali François Xavier Nguyên Van Thuân.

Mungu “si Mungu wa vita wala wa mapigano bali ni Mungu wa amani.”—Kiongozi wa Ekumeni Bartholomeus wa Kwanza.

“Tofauti za kidini hazipaswi kuwafanya [watu] wawapuuze, au hata kuwachukia wengine.”—Dakt. Setri Nyomi, wa Muungano wa Makanisa ya Reformed Ulimwenguni Pote.

“Haki na upendo wa kidugu ndizo nguzo mbili muhimu za amani ya kweli kati ya watu.”—Amadou Gasseto, mwakilishi wa dini za kiasili za Afrika.

“Hakuna vita takatifu, amani tu ndiyo takatifu!”—Andrea Riccardi, Kanisa Katoliki.

Wajumbe wengine walisema kwamba dini zinalaumika sana kwa kuchochea chuki na vita. Mwakilishi wa Muungano wa Kilutheri Ulimwenguni alisema kwamba ulimwengu “umejaa chuki nyingi iliyochochewa na ushupavu wa kidini.” Mwakilishi wa Dini ya Kiyahudi alisema: “Dini zimechochea vita nyingi kali ambazo zimeua watu wengi.” Mjumbe wa Kihindu alitangaza: “Matukio mengi ya zamani yanadhihirisha wazi kwamba watu wanaojidai kuwa watetezi wa dini wametumia dini kuwadhibiti watu na kuwagawanya.”

Baada ya kulaani vikali ugaidi na vita, kila kikundi kilienda mahali pake, kuomba miungu yao mbalimbali ilete amani.

Kuombea Amani

Wajumbe wa Jumuiya ya Wakristo waliomba pamoja katika kanisa la Mtakatifu Francis, karibu na kaburi linaloitwa kwa jina hilo. Papa pamoja na wajumbe wengine watatu walianza kwa “kuomba dua kwa Utatu.” Katikati ya sala mbalimbali, nyimbo za kutukuza amani ziliimbwa na kulikuwa na usomaji wa Biblia kuhusu habari hiyohiyo. Mmoja wao aliomba kuwe na “imani moja.” Mwishowe, washiriki wote waliimba Sala ya Bwana kwa Kilatini, inayotegemea andiko la Mathayo sura ya 6, mstari wa 9 hadi 13.

Wakati huohuo, wajumbe wa dini nyingine waliomba katika sehemu tofauti. Kwenye jumba linaloangalia Mecca, Waislamu walipiga magoti juu ya mazulia, na kumwomba Allah. Wazoroasta waliokuwa wakisali karibu na Wajaini na Wafuasi wa Konfyushiasi, waliwasha moto mtakatifu. Wawakilishi wa dini za kiasili za Afrika waliomba roho za wazazi wao wa kale. Wahindu waliomba amani kutoka kwa miungu yao. Wote walisali kwa miungu yao kulingana na desturi zao.

Wote Waapa Kudumisha Amani

Wajumbe walikusanyika tena kwenye hema ili kumalizia sherehe. Watawa wa kiume waliwapa wajumbe taa zilizowashwa—zilizowakilisha matumaini ya kupata amani. Tamasha hiyo ilikuwa maridadi sana. Kisha wajumbe mbalimbali wakasoma viapo vya kudumisha amani.

“Ili amani ipatikane mtu anahitaji kumpenda jirani yake.”—Kiongozi wa Ekumeni Bartholomeus wa Kwanza.

“Ujeuri na ugaidi ni mambo yasiyopatana na roho ya kweli ya dini.”—Dakt. Konrad Raiser, mjumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

“Tunajitwika wajibu wa kuwaelimisha watu kuhusu kuheshimiana na kustahiana.”—mwakilishi wa Makalasinga, Bhai Sahibji Mohinder Singh.

“Amani bila haki si amani ya kweli.”—Askofu Vasilios, wa Kanisa la Othodoksi.

Hatimaye, papa alisoma maneno yaliyo mwanzoni mwa makala hii. Mkutano huo wa dini mbalimbali ulimalizika na wajumbe wakakumbatiana kuonyesha wana amani. Baada ya hotuba hizo zilizotayarishwa vizuri na kusomwa kwa ufasaha, kulikuwa na sherehe zenye madoido mengi na shamrashamra. Hata hivyo, watu walikuwa na maoni gani kuhusu tukio hilo lenye kupendeza macho?

‘Kama Watu Wangetenda Wasemayo’

Magazeti na televisheni zilimsifu papa kwa jitihada yake. Nyingine hata zilimtaja kuwa “msemaji wa Jumuiya yote ya Wakristo.” Gazeti la Vatikani L’Osservatore Romano lilisema kwamba hiyo ilikuwa “hatua kubwa katika kujenga jamii yenye amani.” Gazeti la Corriere dell’Umbria lilikuwa na kichwa hiki, ‘Mji wa Assisi Waangazia Amani.’

Lakini si watazamaji wote waliovutiwa. Wengine walikuwa na shaka kwa sababu licha ya kuwa na siku za kuombea amani katika miaka ya 1986 na 1993, bado vita vilivyochochewa na dini viliendelea kuwaletea wanadamu mateso. Chuki ya kidini ilichochea vita vikali huko Uganda, Yugoslavia ya zamani, Indonesia, Pakistan, Mashariki ya Kati, na Ireland Kaskazini.

Gazeti la Italia La Repubblica liliwanukuu wachambuzi fulani waliosema kwamba mkutano huo ulikuwa “wa kujionyesha tu.” Mshiriki wa Bunge la Ulaya alisema kwamba ili kuleta amani, watu wa dini wanapaswa “kutenda kupatana na Gospeli”—yaani, wanapaswa kufuata maneno haya, “kupenda maadui wako, kugeuza shavu lile lingine.” Kulingana na maoni yake, “hakuna yeyote anayetenda hivyo.”

Kiongozi wa Wayahudi huko Italia alisema kwamba “tutangoja tuone kama hatua zozote madhubuti zitachukuliwa na kama watu watatenda kupatana na ahadi zao.” Vivyo hivyo, mwakilishi wa Waitaliano Wabudha alisema kwamba kila mmoja alipaswa “kuhakikisha kuwa matangazo ya amani hayakuwa maneno matupu tu.” Mwandishi mmoja wa habari wa gazeti la Italia L’Espresso, alidokeza kwamba dini za Jumuiya ya Wakristo zilizowakilishwa katika mkutano wa Assisi zilikuwa na lengo tofauti. Alisema kwamba mkutano huo “ulipangwa ili kushughulikia tatizo la upungufu wa wafuasi, kushuka kwa viwango vya nidhamu, na ukosefu wa imani,” na kwamba ulijaribu kukabiliana na “hali ya kutopendezwa na mambo ya kidini” huko Ulaya licha ya “kuwa dini za Jumuiya ya Wakristo zimekuwako kwa muda mrefu.”

Wengine waliopinga vikali mkutano huo ni Wakatoliki wanaoshikilia sana tamaduni za kanisa, ambao walihofu kwamba mkutano huo ungepunguza nguvu za mafundisho yao. Akihojiwa katika televisheni, mwandishi mashuhuri Mkatoliki, Vittorio Messori, alisema kwamba mkutano huo unaweza kuficha tofauti kati ya dini mbalimbali. Lakini ni wazi kwamba viongozi wa dini walijitahidi kutoleta wazo la kwamba mkutano huo ulinuia kuchanganya dini mbalimbali. Papa mwenyewe alitoa taarifa ya kupinga madai hayo. Hata hivyo, maoni ya watu wengi ni kwamba mkutano huo ulidokeza kwamba dini mbalimbali zilikuwa njia tofauti-tofauti za kumfikia Mungu mmoja.

Dini na Amani

Hata hivyo, dini mbalimbali zaweza kufanya nini ili kuleta amani? Watu wengine huwa na maoni tofauti kuhusu swali hilo, kwa sababu dini husababisha vita badala ya kuvizuia. Wanahistoria wameeleza jinsi serikali mbalimbali zilivyotumia dini kuchochea vita. Hata hivyo, swali linalozuka ni: Kwa nini dini zimekubali kutumiwa?

Angalau dini za Jumuiya ya Wakristo zina kanuni ambayo ingewaepusha na hatia ya kujiingiza vitani. Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:16) Kama dini za Jumuiya ya Wakristo zingetii maneno hayo, hazingejihusisha na siasa, hazingekubali wala kubariki majeshi na vita.

Kwa kweli, ili viongozi wa kidini waishi kupatana na ahadi nzuri walizotoa huko Assisi, ni lazima wajitenge na siasa. Zaidi ya hilo, ni lazima wawafundishe wafuasi wao jinsi ya kutafuta amani. Hata hivyo, wanahistoria wanasema kwamba watu wengi ambao hupigana duniani wanamwamini Mungu, au angalau wanadai hivyo. Hivi majuzi, gazeti moja lilikuwa na tahariri iliyosema hivi: “Muda mfupi baada ya Septemba 11, mtu mmoja aliandika maneno haya ya kushangaza ukutani huko Washington D.C.: ‘Ee Mungu, tuokoe na watu wanaokuamini.’”

Sherehe zenye madoido na shamrashamra za Assisi hazikugusia maswali fulani. Lakini huenda swali muhimu au lile linalowasumbua sana watu wengi wa dini ni: Kufikia sasa, kwa nini Mungu hajajibu maombi ya amani yaliyotolewa na dini za ulimwengu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu siku ya kuombea amani ya mwaka wa 1986, tafadhali ona gazeti la Amkeni! la Juni 8, 1988.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wajumbe wanabeba taa zilizowashwa zinazowakilisha matumaini ya kupata amani

[Hisani]

AP Photo/Pier Paolo Cito

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

AP Photo/Pier Paolo Cito