Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Walimu Nimekuwa mwalimu wa shule ya msingi kwa miaka minne, na nilifurahi kusoma ule mfululizo wenye kichwa “Walimu Ni Muhimu Sana.” (Machi 8, 2002) Nasikitika sana kuona kwamba watoto wengi hawawezi kutofautisha jema na baya. Kazi ya walimu inakuwa ngumu sana watoto wanapofahamu haki zao zote kabla ya kujua wajibu wao. Hata hivyo, kazi ya kufundisha inaridhisha sana, hasa unapowafundisha wanafunzi wanaopenda masomo na wanaofanya vyema.

J. K., Marekani

Asanteni kwa makala hizo. Zilinisaidia kuelewa jinsi walimu wanavyojitolea sana kutusaidia, hata ingawa mara nyingi hatuwashukuru.

S. M., Italia

Nina umri wa miaka minane. Makala zenu kuhusu walimu zilinisaidia kuelewa kwamba walimu wanawapenda wanafunzi. Wanapenda kuwafundisha watoto hata ingawa si kazi rahisi. Nilimpa mwalimu wangu barua ya kumshukuru. Mimi na dadangu mwenye umri wa miaka minne tunawapenda watu na hivyo tunajifunza jinsi ya kuwafundisha juu ya Yehova—hata ingawa si rahisi nyakati nyingine.

T. M., Marekani

Miaka minne baada ya kuacha kazi ya ualimu, mwanafunzi mmoja aliniandikia barua na kunishukuru kwa sababu ya msaada niliompa. Alinitumia pia kifaa cha kuweka kwenye ukurasa wa kitabu ambacho alikitengeneza mwenyewe. Hebu wazia nilivyofurahi kupokea barua hiyo!

A. R., Slovenia

Nilimpa mwalimu mkuu gazeti hilo na pia walimu wawili katika shule ambayo watoto wangu husomea. Niliwatembelea baada ya siku mbili ili nipate maoni yao. Waliomba magazeti 20 ya Kihispania na Kiingereza ili kuwapa wazazi.

M. M., Marekani

Mwaka uliopita, nilifundisha shule ya msingi kwa miezi minne. Walimu wenzangu walisema kwamba kazi yao ilikuwa ngumu kwa sababu wazazi hawaithamini. Kwa hiyo nilifurahi sana kwa sababu mfululizo huo wa makala unazungumzia kwa heshima kazi ya walimu wenye bidii. Nilipoacha kazi, nilipokea barua nyingi za shukrani kutoka kwa wanafunzi wangu. Ninazithamini sana barua hizo!

S. I., Japan

Kusafiri kwa Puto Asanteni sana kwa makala yenu nzuri yenye kichwa “Kuambatana na Upepo.” (Machi 8, 2002) Kwa muda mrefu nimetamani sana kusafiri kwa puto lakini sijafaulu. Makala hiyo ilinifanya nihisi kana kwamba nilikuwa nikisafiri kwa puto! Kwa kweli “nilihisi” kikapu kikipaa angani huku kikiyumbayumba. Haikosi ulimwengu huonekana ukiwa mdogo sana kutoka angani, lakini Yehova anauthamini ulimwengu na wanadamu.

S. A., Ujerumani

Kuhisi Hatia Nilihitaji sana makala “Maoni ya Biblia: Je, Kuhisi Hatia Ni Kubaya Sikuzote?” (Machi 8, 2002) Nilishindwa kudhibiti hisia zangu nilipokuwa nikishughulika na mwenzi wangu katika kazi ya kuhubiri wakati wote, kwa sababu nilitarajia mengi mno. Lakini makala hiyo ilisema kwamba si jambo la upendo kuendelea kuwafanya watu wajihisi wana hatia eti kwa sababu nyakati nyingine hawafanyi mambo jinsi tunavyotaka. Kufanya hivyo kunaweza kuwazuia wasifanye mambo vizuri. Ninafurahi kwamba nilibadili maoni yangu. Tafadhali endeleeni kutufundisha maoni ya Yehova.

K. K., Japan