Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makosa Madogo Yanaposababisha Misiba

Makosa Madogo Yanaposababisha Misiba

Makosa Madogo Yanaposababisha Misiba

MNAMO Julai 6, mwaka wa 1988, wafanyakazi wa kituo cha uchimbaji wa mafuta cha Piper Alpha kilicho katika Bahari ya Kaskazini, walikuwa wakijaribu kurekebisha pampu ya gesi lakini hawakukamilisha kazi hiyo. Wafanyakazi wa zamu iliyofuata walifungua pampu hiyo kwa sababu hawakuelezwa jambo hilo. Moto ulilipuka na kuua wafanyakazi 167 waliokwama kwenye kituo hicho katikati ya bahari.

Miaka 12 baadaye, Julai 25, mwaka wa 2000, ndege aina ya Concorde inayoenda kwa kasi zaidi kuliko ndege nyingine yoyote ilianza safari kwenye Uwanja wa Ndege wa Charles de Gaulle huko Paris, Ufaransa. Ndege hiyo iliyokuwa ikienda kwa kasi kwenye barabara ya ndege, ilikanyaga kipande cha chuma ya titani kilichopasua gurudumu lake moja. Kisha tangi la mafuta kwenye bawa la ndege hiyo likatoboka. Mafuta yalitiririka kwenye injini za kushoto nazo zikazimika, kisha moto mkubwa wenye urefu wa meta 60 ukatokea. Baada ya dakika mbili hivi, ndege hiyo iligonga hoteli moja, abiria wote waliokuwamo pamoja na watu wengine waliokuwa mahali hapo wakafa.

James Chiles asema hivi kuhusu misiba hiyo katika kitabu chake Inviting Disaster—Lessons From the Edge of Technology: “Katika ulimwengu wetu wa kisasa wenye mashine nyingi ambazo huenda mrama mara kwa mara, tunapaswa kukiri kwamba makosa ya kawaida yanaweza kusababisha hasara kubwa sana.” Jarida la Science lilisema hivi kwa muhtasari kuhusiana na kitabu cha Chiles: “Watu wamesisimuka sana kwa sababu ya maendeleo makubwa na ya haraka ya sayansi na tekinolojia ambayo yamefanywa miaka kadhaa iliyopita. Yanatufanya tuhisi kwamba tunaweza kuelewa na kubuni kitu chochote ulimwenguni. [Lakini] hatupaswi kamwe kufikiri kwamba hatuwezi kukosea kama hapo awali.”

Jarida Science lasema hivi kuhusu tekinolojia ambazo ni hatari zaidi: “Hata kosa dogo ni hatari sana. Ni lazima tufanye mambo kwa usahihi kabisa katika tekinolojia hizo.” Lakini je, yale ambayo mwanadamu amefanya katika miaka iliyopita yanaonyesha kwamba wanaweza kufanya mambo bila kukosea? La hasha! Kwa hiyo hapana shaka kwamba makosa yataendelea kusababisha misiba mbalimbali.

Lakini haitakuwa hivyo milele. Watu wanaomcha Mungu wanatumaini kuishi wakati ujao ambapo hakutakuwa na misiba inayosababisha vifo vya ghafula kwa sababu ya makosa au kutokamilika kwa wanadamu. Kwa nini? Kwa sababu Mungu atatumia Ufalme wake wa mbinguni kuondoa mambo yote yanayosababisha kifo, huzuni, na maumivu.—Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

AP Photo/Toshihiko Sato