Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Atakayeleta Amani ya Kudumu?

Ni Nani Atakayeleta Amani ya Kudumu?

Ni Nani Atakayeleta Amani ya Kudumu?

KWA nini Mungu hajibu maombi ya amani yanayotolewa na viongozi wa dini mbalimbali ulimwenguni? Biblia inatoa jibu la kustaajabisha. Si kwamba Mungu hapendi amani, kwa kweli yeye anataka sana kuleta amani kuliko viongozi hao wa dini. Tayari Mungu amefanya mipango hususa ya kuleta amani ulimwenguni. Hata amechukua hatua madhubuti ili kutimiza kusudi hilo. Amewajulisha wanadamu yale anayokusudia kufanya. Hata hivyo, kwa kusikitisha, dini za ulimwengu zinaendelea kupuuza yale ambayo Mungu amesema.

Zamani Mungu aliahidi “uzao,” mtawala, ambaye Biblia imemfafanua hatua kwa hatua, ikitoa habari zaidi na zaidi kumhusu. (Mwanzo 3:15; 22:18; 49:10) Nabii Isaya, aliyetoa unabii mwingi kumhusu Mesiya, alisema kwamba Kiongozi huyo aliyetabiriwa angekuwa “Mfalme wa Amani” juu ya dunia na kwamba wakati wa utawala wake ‘amani haingekoma.’ (Isaya 9:6, 7, Biblia Habari Njema) Akiwa Mtawala mbinguni, atawaharibu waovu na kuigeuza dunia iwe paradiso isiyo na ukosefu wa haki, magonjwa, umaskini, wala kifo. Kutakuwa na amani na watu wataishi milele. (Zaburi 72:3, 7, 16; Isaya 33:24; 35:5, 6; Danieli 2:44; Ufunuo 21:4) Hilo litatukia lini?

Amani ya Ulimwenguni Pote Imekaribia

Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba kabla ya mwisho wa ulimwengu huu mwovu na mwanzo wa jamii mpya ya wanadamu kungekuwa na mambo yenye kutisha ulimwenguni, ambayo yangetukia yote pamoja kwa wakati mmoja. (Mathayo 24:3, 7-13) Mengi ya matukio hayo—vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na mengineyo—yameonekana ulimwenguni pote katika pindi tofauti. Hata hivyo, mambo hayo hayajatukia pamoja na kwa ghafula kama katika siku zetu. Matokeo ya misiba hiyo yamekuwa mabaya sana kuliko hapo awali kwa sababu sasa dunia ina watu wengi zaidi.

Pia, Biblia ilitabiri kuhusu uharibifu wa mazingira unaoendelea sasa. (Ufunuo 11:18) Ni lazima pia kazi ya ulimwenguni pote ya kuonya wanadamu itekelezwe kabla ya mwisho uliotabiriwa kuja, yaani, kuhubiriwa kwa ‘habari njema ya ufalme.’ Leo Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi hiyo ulimwenguni pote.—Mathayo 24:14.

Utimizo wa unabii huo mbalimbali ni habari njema kwa wanadamu wote waaminifu. Ulimwengu mpya wenye amani ya kudumu uliotabiriwa umekaribia! Katika ulimwengu huo, chuki na ugaidi havitakuwapo tena kamwe. Biblia inasema: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Maombi Ambayo Mungu Husikia

Kuomba Mungu si kazi bure wala desturi isiyo na maana. Biblia inamtaja Yehova kuwa “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Kwa hiyo wakati wowote, yeye husikia sala za watu wengi wanyofu duniani. Je, kuna matakwa yoyote yanayopaswa kutimizwa ili maombi yasikiwe? Biblia hudokeza kwamba watu wenye mioyo minyoofu wanaojifunza kweli za Biblia kumhusu Mungu wanahitaji kuitikia ujumbe huo na kuwa “waabudu wa kweli,” ambao wanamwabudu kwa “roho na kweli.” (Yohana 4:23) Yeye hajibu maombi ya wale ambao hawaheshimu matakwa yake: “Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, hata sala yake ni chukizo.”—Mithali 28:9.

Kwa kusikitisha, viongozi wengi wa dini leo hawafundishi wala hawaombi kuhusu kusudi la Mungu la kuleta amani. Badala yake, wao huomba serikali za wanadamu zisuluhishe matatizo hayo, ilhali neno la Mungu linasema waziwazi kwamba “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.

Ilitabiriwa kwamba “katika siku za mwisho,” wakati huu wetu, wapendao amani wangemiminika kwenye “mlima wa nyumba ya BWANA,” yaani, katika ibada ya kweli. Watu hao wangefanya maendeleo makubwa maishani mwao: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:2-4.

Je, kuna dini yoyote inayojaribu kuishi kupatana na maneno hayo? Au je, dini zote husema kuhusu amani na huku zinachochea vita? Utakapokutana na Mashahidi wa Yehova, tunakukaribisha uzungumze nao kuhusu amani ili ujue ni dini gani inayofundisha watu kuishi kwa amani na watu wote.