Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Hupuuza Udhaifu Wetu?

Je, Mungu Hupuuza Udhaifu Wetu?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Hupuuza Udhaifu Wetu?

‘Mimi si mwovu! Nimejaribu sana kuacha mazoea yangu mabaya, lakini mimi ni dhaifu sana!’

JE, WEWE au mtu fulani unayemjua ana maoni hayo? Watu wengi wamefikia mkataa wa kwamba haiwezekani kushinda udhaifu wetu wa kiadili. Wengine wamezoea kunywa pombe, kuvuta sigara, na kutumia madawa ya kulevya. Wengine wengi wameshindwa na pupa. Wengine pia wana mazoea ya kufanya ngono haramu, wakidai eti wamekuwa wazoefu na hawawezi kubadilika.

Kama andiko la Mathayo 26:41 linavyoonyesha, Yesu alieleza kwa fadhili jinsi anavyoelewa udhaifu wa wanadamu. * Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova Mungu na Yesu wanawahurumia sana wanadamu. (Zaburi 103:8, 9) Lakini je, tutamtazamia Mungu apuuze makosa yetu yote?

Musa na Daudi

Fikiria mfano wa Musa. Alijulikana kuwa mtu “mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi,” na alijitahidi kudumisha sifa hiyo nzuri. (Hesabu 12:3) Waisraeli walipotembea nyikani, mara nyingi walitenda bila kufikiri na kukosa kumheshimu Mungu na wawakilishi wake. Wakati wote huo, Musa alitafuta mwongozo wa Mungu kwa unyenyekevu.—Hesabu 16:12-14, 28-30.

Hata hivyo, mwishoni-mwishoni mwa safari hiyo ndefu, yenye kuchosha, yeye alikasirikia taifa hilo na akakosa kutii maagizo ya Mungu. Ingawa Mungu alimsamehe, je, alipuuza kosa hilo? La. Alimwambia Musa: ‘Kwa kuwa hukuniamini mimi . . . , hutaingiza kusanyiko hili katika ile nchi niliyowapa.’ Musa hangeingia katika Nchi ya Ahadi. Baada ya kutafuta pendeleo hilo zuri kwa miaka 40, udhaifu mkubwa wa kibinadamu ulimfanya alikose.—Hesabu 20:7-12.

Mfalme Daudi alikuwa mtu mwingine mwenye kumhofu Mungu aliyekuwa na udhaifu. Katika pindi moja, yeye alijiruhusu ashindwe na tamaa na kufanya ngono na mke wa mwanamume mwingine. Halafu alijaribu kufunika kosa hilo kwa kupanga mumewe auawe. (2 Samweli 11:2-27) Baadaye, alitubu sana, na Mungu akamsamehe. Lakini tayari Daudi alikuwa ameharibu jamaa hiyo, na Yehova hakumzuia asipatwe na maafa yaliyofuata. Mtoto wa kiume wa Daudi akawa mgonjwa sana, na Yehova hakumponya ingawa Daudi alisali kwa ajili yake. Mvulana huyo akafa, halafu kukawa na misiba mingi katika nyumba ya Daudi. (2 Samweli 12:13-18; 18:33) Daudi alipata matokeo mabaya sana kwa sababu ya kujiachilia mwenyewe ashindwe na udhaifu wa kiadili.

Mifano hiyo inaonyesha kwamba Mungu huona kuwa wanadamu wanawajibika kwa makosa yao. Wale ambao wanataka kumtumikia wanapaswa kujitahidi kushinda udhaifu wao wa kiroho ili wawe Wakristo bora. Wengi walifanya hivyo katika karne ya kwanza.

Kupigana na Dhambi

Mtume Paulo aliweka mfano mzuri kwa Wakristo. Lakini je, ulijua kwamba alikuwa akishindana na udhaifu wake? Andiko la Waroma 7:18-25 hueleza waziwazi kuhusu shindano hilo, au kama mstari wa 23 unavyosema, alikuwa na “vita.” Paulo alipigana kufa na kupona, kwa sababu alijua vita hiyo haikuwa rahisi.—1 Wakorintho 9:26, 27.

Washiriki fulani wa kutaniko la Kikristo katika Korintho la zamani walizoea kufanya dhambi awali. Biblia husema kwamba hapo awali walikuwa ‘waasherati, wazinzi, wanaume walalao pamoja na wanaume, wezi, watu wenye pupa, walevi.’ Lakini, Biblia inasema pia kwamba walikuwa ‘wameoshwa wakawa safi.’ (1 Wakorintho 6:9-11) Jinsi gani? Waliimarishwa na ujuzi sahihi, ushirika wa Kikristo, na roho ya Mungu ili kuacha mazoea hayo maovu. Hatimaye, walitangazwa kuwa waadilifu na Mungu katika jina la Kristo. Naam, Mungu aliwasamehe, na hivyo akawapa dhamiri safi.—Matendo 2:38; 3:19.

Paulo na Wakristo wa Korintho hawakupuuza mielekeo yao yenye dhambi. Badala yake, walipigana nayo, na kwa msaada wa Mungu walishinda. Waabudu hao wa karne ya kwanza wakawa na maadili mema, licha ya mazingira yaliyowazunguka na hali yao ya kutokamilika. Namna gani sisi?

Mungu Hutaka Tupambane na Udhaifu Wetu

Kupambana na udhaifu wetu hakumaanishi kwamba tutauondolea mbali kabisa. Ingawa hatupaswi kujiachilia tushindwe na hali yetu ya kutokamilika, hatuwezi kuikomesha. Kutokamilika hutokeza udhaifu ambao unaweza kuwa mgumu kukomeshwa. Hata hivyo, hatupaswi kujiachilia tushindwe na udhaifu wetu. (Zaburi 119:11) Kwa nini hilo ni muhimu sana?

Kwa sababu Mungu haruhusu kutokamilika kuwe udhuru wenye kuendelea wa mwenendo mbaya. (Yuda 4) Yehova anataka wanadamu wajitakase, waishi maisha ya adili. Biblia husema: “Kirihini lililo ovu.” (Waroma 12:9) Kwa nini Mungu hudai viwango vya juu jinsi hiyo?

Sababu moja ni kwamba tukipuuza udhaifu wetu tunaweza kupata madhara. “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia,” yasema Biblia katika Wagalatia 6:7. Wale wanaojiachilia washindwe na mazoea mabaya, pupa, na maadili mabaya ya ngono, mara nyingi hujiharibia maisha kabisa. Lakini kuna sababu muhimu hata zaidi.

Dhambi humkasirisha Mungu. Hiyo ‘hututenga’ na Yehova. (Isaya 59:2, Biblia Habari Njema) Kwa sababu wale wanaotenda dhambi hawawezi kupata kibali cha Mungu, anawasihi: “Jiosheni, jitakaseni; . . . acheni kutenda mabaya.”—Isaya 1:16.

Muumba wetu ni mwenye upendo na rehema. “Hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Tukijiachilia tushindwe na udhaifu wetu kila wakati, hatutapata kibali cha Mungu. Basi, kwa kuwa Mungu hapuuzi udhaifu wetu, sisi pia hatupaswi kuupuuza.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Yesu alisema: “Roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.”