Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Vijana Wenzako Wanaweza Kukuathiri Sana?

Je, Vijana Wenzako Wanaweza Kukuathiri Sana?

Vijana Huuliza . . .

Je, Vijana Wenzako Wanaweza Kukuathiri Sana?

“Mimi sifikiri kwamba ninaathiriwa na vijana wenzangu.” —Pamela, mwanafunzi wa shule ya sekondari.

“Nadhani kwamba sasa siathiriwi tena na vijana wenzangu. Mimi mwenyewe ndiye ninayejiongoza.”—Robbie, mwanamume kijana.

JE, UMEWAHI kuhisi hivyo? Naam, huenda unajua kwamba Biblia inasema: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Lakini, huenda bado ukajiuliza hivi, ‘Je, kweli uvutano wa marika ni wenye nguvu sana kama vile wazazi wangu na watu wazima wengine wanavyosema?’

Iwapo wewe hujiuliza hivyo mara kwa mara, kumbuka kwamba vijana wengine pia hujiuliza swali hilo. Lakini tunakuomba uchunguze jambo hili. Je, inawezekana kwamba mtu aathiriwe sana na marika wake? Vijana wengi wameshangaa wanapotambua jinsi ambavyo wameathiriwa sana na marika wao. Kwa mfano, Angie anakubali kwamba anafanya juu chini ili apendwe na watu. Anasema hivi: “Nyakati nyingine uvutano wa marafiki unaweza kuwa wenye nguvu sana kiasi cha kumfanya mtu asitambue kuwa anaathiriwa na marika wake. Unaweza kufikiri kwamba ni wewe mwenyewe unayejiongoza kufanya mambo.”

Vivyo hivyo, Robbie, aliyenukuliwa hapo juu, anasema kwamba yeye hasa ndiye anayejiongoza. Hata hivyo, anakubali kuwa si rahisi kuishi katika jiji kubwa. Kwa nini? Kwa sababu watu huathiriwa sana wanapoishi miongoni mwa watu wenye tamaa ya mali. Anasema hivi: “Huku jijini, mali huonwa kuwa muhimu sana.” Kwa wazi, uvutano wa marika si mchezo. Basi, ni kwa nini vijana wengi hufikiri kwamba hawawezi kuathiriwa na marika wao?

Kuathiriwa Sana Bila Kutambua

Marika wanaweza kumwathiri mtu bila yeye kujua. Kwa mfano: Tunapokuwa kwenye usawa wa bahari, hewa iliyo juu yetu huendelea kutushinikiza. Kila sehemu yenye ukubwa wa sentimeta moja ya mraba hupata shinikizo la kilogramu moja. * Huenda unashinikizwa hivyo kila siku bila kujua. Kwa nini? Umezoea.

Ni kweli kwamba shinikizo la hewa haliwezi kudhuru. Lakini watu wanapotushinikiza bila sisi kujua, wanaweza kutufanya tubadilike pole kwa pole. Mtume Paulo alijua kwamba watu wanaweza kuathiriwa sana na wenzao. Aliwaonya hivi Wakristo huko Roma: “Msiache ulimwengu unaowazunguka uwafinyange kulingana na muundo wake.” (Waroma 12:2, The New Testament in Modern English) Tunaweza kujipataje katika hali hiyo?

Jinsi Watu Wanavyoathiriwa na Marika

Je, wewe hupenda kukubaliwa na wengine? Wengi wetu wanaweza kukubali jambo hilo. Hata hivyo, tamaa yetu ya asili ya kukubaliwa inaweza kuleta faida au madhara. Je, sisi hufanya juu chini ili tukubaliwe na wengine? Hata ikiwa tuna uhakika kwamba hatuwezi kuathiriwa na marika kiasi hicho, vipi watu wengine tunaoshirikiana nao? Je, wanajaribu kuepuka kuathiriwa na marika wao, au wanajiachilia wafinyangwe nao?

Kwa mfano, watu wengi leo huona kwamba viwango vya Biblia kuhusu maadili ni vya kizamani ama havifai katika ulimwengu wa sasa. Wengi wanaonelea kwamba si lazima kumwabudu Mungu kulingana na matakwa yake yaliyo katika Neno lake. (Yohana 4:24) Kwa nini wanaonelea hivyo? Huenda sababu kuu ni kwamba wameathiriwa na watu wengine. Kwenye Waefeso 2:2, Paulo anasema kwamba kuna “roho” fulani au mtazamo fulani ulioenea katika mfumo wa mambo. Roho hiyo huwachochea watu wafikiri kama watu wa ulimwengu wasiomjua Yehova. Tunaweza kuathiriwaje?

Shughuli tunazofanya kila siku, kama vile kwenda shuleni, kujifunza, kutunza madaraka ya familia, na kufanya kazi hutulazimu tushirikiane na watu ambao hawafuati maadili ya Kikristo kikamili. Kwa mfano, huenda shuleni kuna vijana wengi ambao wanajitahidi kwa udi na uvumba kuwa mashuhuri, wanaofanya uasherati, au hata wanaotumia dawa za kulevya na pombe. Ni nini kinachoweza kutukia tukiwa na marafiki wanaofanya mambo hayo au wanaoyaona kuwa ya kawaida, au hata kuwa mazuri? Huenda tukaanza—pole kwa pole—kuiga mwenendo wao. “Roho,” au “hewa,” ya ulimwengu itatuathiri sana na kutufanya tuwe kama watu wa ulimwengu.

Wataalamu wa mambo ya kijamii wamefanya majaribio fulani ambayo yanaunga mkono kanuni hizo za Biblia. Hebu fikiria lile jaribio maarufu la Asch. Katika jaribio hilo, mtu huombwa ajiunge na kikundi cha watu walioketi pamoja. Dakt. Asch huwaonyesha watu hao kadi kubwa yenye mstari ulio wima, kisha anawaonyesha kadi nyingine yenye mistari mitatu iliyo wima yenye urefu mbalimbali. Halafu anawaomba watu walio katika kikundi hicho wachague mstari unaofanana na ule mstari wa kwanza. Jibu ni rahisi. Mara chache za kwanza, wote wanakubaliana. Lakini wanapoulizwa swali hilohilo mara ya tatu, mambo yanabadilika.

Kama ilivyokuwa mara zile nyingine, ni rahisi kuchagua mistari inayofanana. Lakini yule mtu anayejaribiwa hajui kwamba washiriki wale wengine wa kikundi hicho wamelipwa ili kufanya jaribio hilo. Sasa, wanapoulizwa swali hilo mara ya mwisho wote katika kikundi wanaamua kuchagua mstari usiofaa. Matokeo huwa nini? Ni asilimia 25 tu ya watu wanaojaribiwa hivyo ambao huchagua mstari sahihi kwenye jaribio hilo la mwisho. Lakini wengine wote hufuata maoni ya kikundi angalau mara moja—hata ingawa wao wenyewe wanaona kwamba mistari hiyo hailingani!

Ni wazi kwamba watu hutaka sana kukubaliwa na watu wanaoshirikiana nao hivi kwamba wanaweza kukataa mambo wanayojua kuwa ya kweli. Vijana wengi wameathiriwa hivyo. Daniel, mwenye umri wa miaka 16, anakubali hivi: “Vijana wenzako wanaweza kukufanya ubadilike. Na unapokuwa kati ya watu wengi, uvutano huo huongezeka. Unaweza hata kuanza kufikiri kwamba wanafanya mambo mazuri.”

Angie, aliyenukuliwa hapo awali, anaeleza jambo lililotukia shuleni: “Nilipoingia katika shule ya sekondari, hungevalia nguo zozote tu. Vijana walipenda kuvalia nguo zenye lebo. Iliwabidi vijana wanunue shati za dola 50 za Marekani wapende wasipende.” Kama vile Angie anavyosema, ni vigumu kujua kwamba unaathiriwa na vijana wengine. Lakini je, tunaweza kuathiriwa na vijana wenzetu kufanya mambo mabaya hata zaidi?

Hatari za Kuathiriwa na Marika

Hebu wazia ukiogelea baharini. Unapozidi kuogelea na kupelekwa na mawimbi, huenda kukawa na nguvu nyingine ambazo huzitambui. Mawimbi hayo yanakusukuma kuelekea ufuoni, lakini huenda kuna mkondo mwingine chini ya maji. Pole kwa pole mkondo huo unakusukuma huku na huku. Kufumba na kufumbua, huwaoni tena watu wa familia yako au marafiki wako unapotazama ufuoni. Kumbe hukutambua kwamba mkondo wa maji ulikusukuma mbali sana! Vivyo hivyo, tunapoendesha shughuli zetu za kila siku, mawazo na hisia zetu huathiriwa daima. Pasipo kujua, tunaweza kuathiriwa tupuuze kanuni ambazo tulifikiri tungezishikilia kwa uthabiti.

Kwa mfano, mtume Petro alikuwa mwanamume jasiri. Usiku ule ambao Yesu alikamatwa, Petro alitumia upanga mbele ya umati wenye hasira kali. (Marko 14:43-47; Yohana 18:10) Hata hivyo, miaka mingi baadaye aliathiriwa na watu na akaonyesha ubaguzi wa wazi. Aliwahepa Wakristo Wasio Wayahudi—hata ingawa hapo awali Kristo alikuwa amemwonyesha njozi ambayo ilimwongoza asiwaone Wasio Wayahudi kuwa wasio safi. (Matendo 10:10-15, 28, 29) Huenda Petro alihisi vigumu zaidi kudharauliwa na watu kuliko kukabiliana na watu wenye mapanga! (Wagalatia 2:11, 12) Pasina shaka, uvutano wa marika unaweza kuwa hatari.

Ni Muhimu Kujua Kwamba Marika Wako Wanaweza Kukuathiri Sana

Mfano wa Petro unaweza kutufundisha somo muhimu. Kuwa na sifa fulani nzuri hakumaanishi kwamba mtu hana udhaifu wowote. Petro alikuwa na udhaifu, kama sisi sote. Haidhuru sisi ni nani, tunapaswa kufahamu udhaifu wetu. Tunaweza kujiuliza hivi kwa unyoofu: ‘Udhaifu wangu ni nini? Je, mimi hutamani utajiri? Je, nimeanza kujivuna kwa sababu ya sura yangu au mafanikio yangu? Je, ninaweza kufanya lolote liwalo ili nipate sifa, cheo, na umashuhuri?’

Naam, huenda tusijiletee balaa kimakusudi kwa kushirikiana na watu wanaotumia dawa za kulevya au wanaofanya uasherati. Lakini vipi kuhusu udhaifu wetu mbalimbali uliofichika? Tukichagua kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao wanafanya mambo mabaya yanayohusiana na udhaifu wetu, basi tutakuwa tunajiachilia tuathiriwe nao—na labda tunaweza kuangamia kabisa.

Hata hivyo, inatia moyo kukumbuka kwamba kuna uvutano unaofaa. Je, tunaweza kutumia uvutano huo vizuri—kwa faida yetu? Na tunawezaje kuepuka kuathiriwa vibaya na marika? Maswali hayo yatajibiwa katika makala moja ya wakati ujao ya “Vijana Huuliza . . . ”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Jaribio fulani sahili linaonyesha kwamba kuna shinikizo la hewa. Ukikwea mlimani na chupa tupu ya plastiki, kisha uijaze hewa na kuifunika kabisa, ni nini kitakachotokea unaposhuka mlima huo? Chupa hiyo itabonyea. Shinikizo la hewa nje ya chupa linazidi sana shinikizo la hewa nyepesi iliyo ndani ya chupa.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Mtu anaweza kuathiriwa sana anapokuwa miongoni mwa watu walio na tamaa ya mali