Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tiba ya Kiajabu Inayozusha Mzozo

Tiba ya Kiajabu Inayozusha Mzozo

Tiba ya Kiajabu Inayozusha Mzozo

“Mjadala kuhusu chembe za msingi umewafanya wanasayansi na watu wengine wafikirie masuala mazito kama vile, sisi wanadamu tumeumbwaje na kwa nini tuko tofauti.”—SHIRIKA LA KITAIFA LA SAYANSI, MAREKANI.

KAREN ana ugonjwa wa sukari unaodhibitiwa na insulini. Kongosho lake linaugua na hivyo halitengenezi tena kemikali ya insulini. Hebu wazia kama Karen angeweza kwenda kwa daktari na kutiwa chembe mpya za kongosho, ambazo zimekuzwa kwenye maabara. Chembe hizo mpya zingeanza kufanya kazi, na pole kwa pole Karen angeacha kutiwa insulini na kuwa na afya njema tena.

Miaka michache iliyopita, tiba kama hizo zilionekana kuwa ndoto tu, lakini sasa watafiti fulani wanaamini kwamba zinawezekana. Kwa nini? Kwa sababu mnamo mwaka wa 1998, wanasayansi walivumbua njia ya kukuza chembe nyingi za msingi za mwili wa mwanadamu (human stem cells). Chembe hizo zinaweza kusitawi na kuwa kama chembe yoyote kati ya chembe mbalimbali zaidi ya 200 zilizo katika mwili wa mwanadamu, kutia ndani chembe za kongosho. *

Ripoti moja iliyotayarishwa na Taasisi za Kitaifa za Afya huko Marekani ilisema kwamba “chembe za msingi huenda zikatokeza chembe mpya zinazoweza kuchukua mahali pa zile zinazoharibiwa na magonjwa mengi hatari.” Baadhi ya magonjwa hayo ni “ugonjwa wa kutetemeka, ugonjwa wa sukari, ugonjwa sugu wa moyo, ugonjwa hatari wa figo, kuharibika kwa ini, na kansa.” Chembe hizo zinaweza pia kufanyiza damu, na inasemekana kwamba huenda hata zikafanya benki za damu zifungwe. Isitoshe, madaktari wamekuwa wakitumia chembe hizo kwa miaka mingi kutibu magonjwa fulani ya damu. Kwa kawaida matibabu hayo hutia ndani kubadili uboho wa mifupa, ambao una chembe nyingi sana zinazofanyiza damu, lakini sasa madaktari hupenda kukusanya chembe hizo kutoka kwenye damu iliyo mwilini. Inatarajiwa kuwa matibabu yanayotumia chembe za msingi yataweza kufanyiza tishu mpya.

Hata hivyo, mambo fulani katika sayansi hii mpya yanazusha mzozo. Watu wengi, kutia ndani wanasayansi fulani, wanahisi kwamba kutumia chembe za msingi za mwili wa mwanadamu—na hasa chembe zinazotoka kwa viinitete au vijusi—ni kutothamini utakatifu wa uhai wa wanadamu. Suala hilo limezusha zogo.

Wale wanaotetea matumizi ya chembe za msingi wanatabiri kwamba zitatibu magonjwa mengi sana, kwa hivyo makala zinazofuata zinachunguza kwa undani aina mbalimbali za chembe za msingi, jinsi zinavyopatikana, na kwa nini suala hilo linazusha mzozo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Maabara mbalimbali nchini Marekani zilikuza aina mbili za chembe za msingi—chembe za kiinitete na chembe za uzazi.