Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo Waonyeshwa Kupitia Kazi Kubwa ya Kutoa Msaada

Upendo Waonyeshwa Kupitia Kazi Kubwa ya Kutoa Msaada

Upendo Waonyeshwa Kupitia Kazi Kubwa ya Kutoa Msaada

KWA kawaida ni vigumu kumpendeza Richard Vara, mhariri wa gazeti la Houston Chronicle mwenye ujuzi wa miaka mingi. Hata hivyo, mwaka jana alivutiwa na jambo fulani. “Sijawahi kuona jambo lolote kama hilo!” alisema. “Siamini.” Maoni yake yalikuwa kama ya Lee P. Brown, meya wa Houston, Texas, Marekani. Meya huyo alisema hivi: “Laiti kila mkazi wa Houston angeona yale mliyofanya. Nimevutiwa sana.” Watu hao walikuwa wakizungumza kuhusu nini? Mhariri huyo na meya walikuwa wakizungumza kuhusu kazi ya kutoa msaada iliyofanywa na Mashahidi wa Yehova huko Houston. Kazi hiyo ilihusisha nini? Mbona ilihitajika? Na kwa nini ilivutia sana? Ili kupata majibu, hebu tuanze mwanzo kabisa.

Furiko Kubwa Zaidi Kuwahi Kutokea Houston

Mapema katika Juni 2001, dhoruba kali iliyoitwa Allison ilikumba eneo tambarare lililoko kusini-mashariki mwa Texas. Kisha, siku ya Ijumaa, Juni 8, dhoruba hiyo ilisababisha mvua kubwa ya milimeta 1,000 kwa muda wa saa 24 huko Houston—jiji la nne kwa ukubwa huko Marekani. * Punde si punde, maji yakazidi kuwa mengi na kuingia madukani, ofisini, na ndani ya makumi ya maelfu ya nyumba. Barabara kuu za jiji zilifurika kama mito na kufunika magari na malori marefu ambayo hayangeweza kusonga. Maji hayo yalifanya iwe vigumu hata kwa malori ya wazima-moto na magari mengine ya kutoa msaada kupita kwenye baadhi ya barabara za jiji zilizofurika. Ilibidi helikopta na magari makubwa ya kijeshi yatumiwe kuwaokoa watu.

Mawingu ya mvua yalipotokomea mnamo Jumatatu, Juni 11, ilibainika kwamba dhoruba ya Allison ilikuwa imesababisha vifo na uharibifu mkubwa. Watu 22 walikufa, kutia ndani Mashahidi wa Yehova wawili: Jeffrey Green, mzee Mkristo, na shemeji yake Frieda Willis. * Zaidi ya hayo, nyumba 70,000 hivi ziliharibiwa. Hivyo, furiko hilo ni mojawapo ya misiba mibaya zaidi ya asili kuwahi kutokea katika jiji kubwa. Dhoruba ya Allison ilisababisha hasara kubwa zaidi za kifedha kuliko dhoruba nyingine yoyote nchini Marekani, kwani iliharibu mali zenye thamani ya dola bilioni 5 hivi za Marekani.

Wengi Walijitolea

Watu walishtuka. Mfanyakazi mmoja wa kutoa msaada alisema hivi: “Vitanda vyao vililowa chepechepe. Zulia lao lililowa. Picha walizopigwa walipokuwa watoto zilifagiliwa kabisa.” Wengi kati ya wale Mashahidi wa Yehova zaidi ya 16,000 huko Houston walipata hasara. Majumba ya Ufalme manane na mamia ya nyumba za Mashahidi ziliharibiwa. Baadhi ya nyumba hizo zilikuwa zimejaa maji kwa sentimeta kadhaa; nyingine zilifunikwa hadi kwenye paa. Kwa ujumla, zaidi ya makutaniko 80 ya Mashahidi wa Yehova yaliathiriwa. Hata hivyo, wale walioathiriwa walitegemezwa. Siku chache baadaye, umati wa wafanyakazi waliojitolea ulikuja kuwasaidia. Hilo liliwezekanaje?

Hata kabla ya maji kuanza kupungua, wazee Wakristo wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huko Houston walichukua hatua mara moja. “Tuliwapigia simu na kuwatembelea ndugu na dada zetu,” alisema mzee mmoja. “Kisha tukakagua hasara iliyotokea, na kufikia Jumatatu, Juni 11, tulikuwa tumetayarisha ripoti kamili yenye majina ya wale walioathiriwa, idadi ya nyumba zilizoharibiwa, na kiwango cha uharibifu. Ripoti hiyo ilitumwa kwa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York.” Siku chache baadaye, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Marekani ilianzisha halmashauri ya kutoa msaada ya wazee wanane Wakristo kutoka Houston na pia ikatoa fedha za msaada. Halmashauri hiyo ilipaswa kufanya nini? Kuwafariji wale walioathiriwa na kurekebisha nyumba za Mashahidi zilizoharibika—nyumba zaidi ya 700!

Washiriki wa Halmashauri ya Mashahidi wa Yehova ya Kutoa Msaada huko Houston ya mwaka wa 2001 walijiuliza: ‘Tutawezaje kutimiza kazi kubwa hivi?’ Walifanya kazi hadi usiku sana wakipanga jinsi watakavyoanza kutoa msaada na wakaomba usaidizi wa yale makutaniko ya Mashahidi zaidi ya 160 katika eneo la Houston. “Wengi sana waliitikia mwito huo,” alisema mwenyekiti wa halmashauri hiyo. “Zaidi ya Mashahidi 11,000 walijitolea, wakakubali kutumia wakati wao, nguvu zao, na ustadi wao bila malipo.”

Waliojitolea Wapambana na Kuvu

Siku chache baada ya furiko hilo, wale waliojitolea walienda kwenye nyumba zilizoharibika wakaondoa mazulia yaliyolowa chepechepe, sakafu na kuta zilizoharibika, makabati yaliyolowa, milango iliyopindika, na kila kitu kilichoharibiwa na maji machafu. Mmoja aliyejitolea alisema hivi: “Mbali na kuwarekebishia ndugu zetu nyumba zao, tulitaka pia kulinda afya yao.” Kwa kuwa kuvu zenye sumu zingeanza kuota nyuma ya kuta na ndani ya makabati, ilibidi kwanza nyumba zisafishwe kabisa kwa dawa.

Ili kujua jinsi ya kufanya kazi hiyo kwa njia salama, Mashahidi kadhaa waliomba wazoezwe na shirika moja la serikali linaloshughulikia misiba. Baada ya hapo, kila Shahidi aliyezoezwa alienda kwenye nyumba iliyoharibika pamoja na wengine kumi waliojitolea ambako aliwafundisha jinsi ya kusafisha nyumba hiyo vizuri kwa dawa. Siku iliyofuata kila mmoja wa hao kumi waliozoezwa aliwafundisha wengine kumi. Mmoja aliyejitolea anasema hivi: “Baada ya siku chache, mamia ya wafanyakazi hao walikuwa wamejua jinsi ya kufanya kazi hiyo.” Kuvu ziliondolewa kabisa! Watu waliostaafu na vijana waliokuwa wamefunga shule walifanya kazi mchana. Usiku, wengine waliendelea kufanya kazi hiyo. Baada ya majuma sita, nyumba zote za Mashahidi zilizokuwa na maji machafu zilikuwa safi na salama.

Kituo Kikuu na Vituo Saba Vidogo

Wakati huohuo, halmashauri ya kutoa msaada ilinunua vibao vingi vya kutengeneza kuta na tani nyingi za vifaa vingine vya ujenzi. Lakini vitu hivyo vingewekwa wapi? Msemaji wa halmashauri hiyo ya kutoa msaada alisema hivi: “Meneja wa kampuni moja alipojua mahitaji yetu, alituruhusu tutumie bohari lake—lenye ukubwa wa meta 5,000 za mraba—bila malipo!” Zaidi ya kuhifadhi vifaa vya ujenzi, bohari hilo pia lilikuwa na nafasi ya kujenga ofisi mbalimbali. Baada ya muda, bohari hilo likawa kituo kikuu cha usimamizi wa kazi ya kutoa msaada, ambako watu 200 hadi 300 hivi waliojitolea walifanya kazi mchana, usiku, na mwishoni mwa juma.

Kwa sababu nyumba zilizoharibika zilikuwa kotekote, vituo vingine vidogo vya kutoa msaada vilianzishwa katika Majumba saba ya Ufalme. Mwishoni mwa juma, kila kituo kidogo kilikuwa na wafanyakazi wengi wa kujitolea. (Ona sanduku “Kituo Chenye Shughuli Nyingi.”) Wengi wao walikuwa wamefanya kazi pamoja hapo awali katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme ya eneo hilo. Ama kwa hakika, mafundi wa kujitolea kutoka katika Halmashauri 11 za Ujenzi za Mkoa huko Arkansas, Louisiana, Oklahoma, na Texas walisaidia kufanya kazi hiyo. * Katika kila kituo kidogo, maseremala, wapaka-rangi, mafundi wa mabomba, na wafanyakazi wengine stadi walisimamia kazi na kuwazoeza wengine.—Ona sanduku “Mipango ya Mazoezi.”

Ratiba na Habari za Kompyuta

Wale waliojitolea walifuata ratiba ya ujenzi iliyopangwa katika hatua saba mbalimbali. Vifaa vya ujenzi vilipelekwa kwenye nyumba zilizopasa kurekebishwa katika safari nne, na kazi ya urekebishaji wa kila nyumba iliratibiwa kufanywa kwa miisho juma mitatu. Hivyo, kazi yote ya kutoa msaada ingekamilishwa kwa kipindi cha miezi sita hivi.

Ili kufanikisha mpango huo, halmashauri hiyo ilipanga idara 22, kutia ndani idara ya kupanga habari, ya ununuzi, ya mahali pa kulala, na ya usafirishaji. Idara zote zilifaidika kutokana na habari kemkemu za kompyuta zilizotayarishwa na wale waliojitolea. Kabla ya kazi ya urekebishaji kuanza, wafanyakazi waliojitolea waliingiza habari katika kompyuta kwa muda wa siku kumi. Ripoti moja ya habari ilisema hivi: “Kazi ya kuingiza habari hizo ilikuwa nyingi sana.” Hata hivyo, mwishoni mwa siku hizo kumi, habari nyingi muhimu zingeweza kutumiwa. Habari hizo za kompyuta zilionyesha wakati ambapo wale wafanyakazi 11,000 wa kujitolea wangepatikana, stadi walizokuwa nazo, na jinsi ya kuwasiliana nao. Pia, zilionyesha urekebishaji uliohitajika, vibali vya ujenzi vilivyohitajika, na habari nyingine kuhusu nyumba zilizoharibika. Habari hizo za kompyuta zilionwa kuwa “kitovu cha mradi huo wa kutoa msaada.”

Waliguswa Hisia Sana na Kushukuru

Mafundi wa ujenzi waliojitolea walienda kwenye nyumba kavu ambazo hazikuwa na kuvu ili kujua kile kilichohitajiwa kurekebisha sehemu zilizoharibika. Msemaji wa mradi huo alisema hivi: “Wafanyakazi hao wa kujitolea wangeweza kukadiria idadi hususa ya vifaa vilivyohitajiwa hata idadi ya misumari iliyohitajiwa. Hatukutaka kutumia vibaya pesa wala vifaa vilivyochangwa.” Wakati huohuo, wafanyakazi wengine wa kujitolea walipata vibali vya ujenzi vilivyohitajika kutoka kwa maofisa wa jiji.

Kisha, familia zilizoathiriwa zilialikwa kwenye bohari ili kuchagua mazulia, makabati, sakafu za plastiki, na vifaa vingine vilivyokuwepo ili vitumiwe badala ya vile vilivyoharibika. Wale walioathiriwa na furiko hilo waliguswa hisia sana na mara nyingi walilia walipoona vitu vyote walivyokuwa wameandaliwa. Pia, walipewa mashauri na wengine wenye ujuzi katika masuala ya bima na mipango ya serikali. Kisha, nyumba zilirekebishwa kulingana na ratiba, na madereva waliojitolea walisafirisha vifaa vya ujenzi siku ambayo vilihitajiwa na wajenzi. Mtu mmoja asiye Shahidi ambaye nyumba yake ilikuwa ikirekebishwa alimwambia hivi mke wake ambaye ni Shahidi: “Ndugu zako ni watu wa ajabu sana. Kikosi kimoja cha wajenzi kinaondoka, kisha kingine kinaingia. Wanafanya kazi kama chungu!”

Katika kila nyumba marekebisho makubwa yalifanywa kwa miisho juma mitatu hivi. “Hata hivyo, nyakati nyingine, marekebisho yalifanywa kwa majuma matano au hata manane,” alisema mwenyekiti wa halmashauri hiyo. Kuta zilipobomolewa katika nyumba kuukuu, wafanyakazi waliojitolea waligundua sehemu zilizokuwa zimeharibika, na hawakutaka kujenga kuta mpya kabla ya kurekebisha sehemu hizo. Fundi mmoja aliyejitolea, alisema hivi: “Nyakati nyingine tuligundua kwamba miimo ilikuwa imeliwa na mchwa, kwa hiyo tulihakikisha kwamba mchwa hao wameangamizwa. Mara nyingi ilitubidi kurekebisha mihimili na nguzo kabla ya kurekebisha sehemu nyinginezo. Tuliondoka kwenye nyumba hizo zilipokuwa katika hali nzuri.” Mmoja aliyeathiriwa na furiko hilo, alieleza hisia zake zinazofanana na za watu wengine wengi ambao nyumba zao zilirekebishwa wakati alipomwambia mgeni wake hivi: “Sasa nyumba yangu ni nzuri kuliko ilivyokuwa nilipoinunua!”

Milo Iliyotayarishwa na Kupakuliwa Haraka

Ili kuwaandalia wafanyakazi wa kujitolea chakula, kikundi fulani cha Mashahidi kilitumia bohari iliyokuwa nyuma ya Jumba moja la Ufalme kama kituo cha kutayarisha na kugawa chakula. Mashahidi kotekote katika nchi hiyo walichanga friji, mashine za kuosha vyombo, meko, na vifaa vingine vya jikoni. Kila Jumamosi na Jumapili, wapishi 11 na wafanyakazi wengine 200 wa kujitolea walitayarisha milo mingi katika kituo hicho. Mfanyakazi wa kujitolea aliyesimamia upishi katika jiko hilo, alisema hivi: “Kwa miaka 19, tumekuwa tukitayarisha milo wakati wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme, lakini mradi huu ulikuwa mkubwa zaidi kuliko tulivyodhania.”

Milo hiyo iliwekwa katika masanduku makubwa 120. Kisha masanduku hayo yakapakiwa ndani ya magari 60 na kupelekwa kwenye kile kituo cha usimamizi na vituo vyote vidogo vya kutoa msaada. Wakati huohuo, kila kikosi kilichofanya kazi ya kurekebisha nyumba kilituma mtu kwenye kituo kidogo ili kuchukua chakula kwa ajili ya wafanyakazi wote katika kikosi hicho. Wafanyakazi hao wa kujitolea walikula katika nyumba hizo na kuendelea na kazi yao mara moja.

Kazi Yakamilika!

Hatimaye, mnamo Aprili 2002, wafanyakazi 11,700 waliojitolea walikamilisha mojawapo ya miradi mikubwa zaidi ya kutoa msaada kuwahi kufanywa na Mashahidi wa Yehova. Walitumia saa 1,000,000 kurekebisha au kujenga upya Majumba ya Ufalme 8 na nyumba 723. Mmoja aliyeathiriwa na furiko hilo alizungumza kwa niaba ya wengine wengi huku akitokwa machozi ya shukrani na kusema hivi: “Ninamshukuru Yehova na wale waliojitolea kwa msaada wao wote. Inafariji kama nini kuwa miongoni mwa akina ndugu wenye upendo!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majiji ya New York, Los Angeles, na Chicago yana watu wengi zaidi. Eneo la jiji la Houston lina wakazi wapatao 3,500,000 na ni kubwa kuliko nchi ya Lebanon iliyoko Mashariki ya Kati.

^ fu. 5 Hotuba ya mazishi ilihudhuriwa na marafiki 1,300 wa Jeffrey na Frieda. Jambo hilo lilimfariji sana Abigail—mke wa Jeffrey ambaye pia ni dada ya Frieda.

^ fu. 15 Kwa kawaida, Halmashauri za Ujenzi za Mkoa hushughulikia ujenzi wa majengo ya kukutana ya Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

KITUO CHENYE SHUGHULI NYINGI

Ni Jumamosi, saa 1:00 asubuhi, kwenye Kituo Na. 4 kilichoko kaskazini-mashariki mwa Houston. Wafanyakazi wa kujitolea wanazungumza, wanacheka, wanakunywa kahawa, na kutafuna maandazi katika Jumba la Ufalme. Wengine wameendesha gari mamia ya kilometa kutoka makwao. Lakini saa 1:30 asubuhi, wananyamaza, na mwangalizi wa kituo hicho, anaongoza mazungumzo ya andiko la Biblia. Pia anatangaza kwamba Funzo la Mnara wa Mlinzi litafanywa Jumapili saa 1:30 asubuhi kabla ya wafanyakazi hao kwenda kazini, na anawatia moyo wote kushiriki katika funzo hilo kwa kutoa maelezo katika Kiingereza au Kihispania. Anawasilisha ujumbe kutoka kwa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni, na wote wanapiga makofi.

Kisha anawajulisha maendeleo ya kazi ya kutoa msaada na anawashukuru kwa uchangamfu kwa kujitolea kwa hiari. Anauliza hivi: “Je, kuna yeyote hapa asiyejua la kufanya au mahali pa kwenda leo?” Hakuna anayeinua mkono. Kisha anauliza: “Ni wangapi watakaohitaji chakula?” Wote wanainua mikono haraka na kuangua kicheko. Hatimaye, sala inatolewa, na wafanyakazi 250 wa kujitolea—wanaume, wanawake, vijana kwa wazee—wanaenda kazini, wakiwa tayari kwa siku nyingine ya kazi ngumu.

Hali iko vivyo hivyo katika vile vituo vingine sita na kwenye bohari. Wakati huohuo, wafanyakazi wengine wako katika jiko kuu ambako tayari wameanza kutayarisha chakula—kwani, kufikia saa sita adhuhuri zaidi ya wafanyakazi 2,000 katika eneo lote la Houston watasubiri kuandaliwa chakula moto!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

MIPANGO YA MAZOEZI

Wakati wa kazi hiyo ya kutoa msaada, mafundi waliojitolea walipanga vipindi vya kuwazoeza wafanyakazi wengine wa kujitolea kufanya kazi maalumu. Wengine walizoezwa kusafisha nyumba kwa dawa. Wengine walijifunza namna ya kujenga kuta na kutengeneza makabati. Na wengine wakajifunza jinsi ya kupiga plasta na kupaka rangi. Semina hizo za Kuwazoeza Wafanyakazi zilirekodiwa kwenye video, na video hizo zilitumiwa katika vile vituo vidogo kuwazoeza wafanyakazi wengine. Mshiriki mmoja wa halmashauri ya kutoa msaada alisema hivi: “Semina hizo ziliwezesha kazi ya urekebishaji iwe ya hali ya juu.”

[Picha]

Mafundi waandaa mazoezi

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

“KAZI HALISI YA MUNGU”

Mshiriki mmoja wa halmashauri ya kutoa msaada, alisema hivi: “Makampuni ya bima husema kwamba misiba ya asili ni kazi za Mungu.” Kisha akasema: “Hata hivyo, kazi halisi ya Mungu imeonekana kupitia kwa wale waliojitolea kufanya kazi hapa kwa miezi yote hiyo. Udugu wetu ni wa ajabu sana!” Wakati wa kazi hiyo ya kutoa msaada, watu 2,500 au zaidi walijitolea kusaidia wakati wa miisho ya juma. Mwenyekiti wa halmashauri hiyo alisema hivi: “Wafanyakazi hao wasiolipwa walijinyima kwenda likizo, wakapanga upya shughuli zao za kifamilia na shughuli nyingine za kibinafsi ili kufanya mojawapo ya kazi kubwa zaidi za kutoa msaada kuwahi kufanywa na Mashahidi wa Yehova.”

Kazi hiyo kubwa ya kutoa msaada ilihitaji watu wajinyime mambo fulani. Mfanyakazi mmoja aliyejitolea kuunga mkono kazi hiyo kuanzia mwanzo hadi mwisho alikuwa na kazi ya kuajiriwa ambayo aliifanya kwa muda wa saa 50 kila juma. Hata hivyo, alitumia saa 40 kila juma katika kazi hiyo ya kutoa msaada. “Yehova alinipa nguvu,” alisema. “Watu ninaowajua waliniuliza hivi, ‘Je, wewe hulipwa?’ Nami niliwaambia, ‘Hakuna mshahara wowote unaoweza kulipia kazi hii.’” Mwishoni mwa juma, baada ya kufanya kazi ya kuajiriwa juma lote, familia moja kutoka jimbo la Louisiana ilisafiri kilometa 800 kwa gari kwenda na kurudi ili kuunga mkono kazi hiyo ya kutoa msaada. Wengi walifanya kazi toka mapambazuko hadi jioni kisha wakaendesha gari kurudi makwao. Kikundi kimoja cha wafanyakazi stadi 30 wa kujitolea waliosafiri kwa gari kwa muda wa saa saba hadi kumi, kilisema hivi: “Kuna faida kubwa kuja kusaidia.” Mwingine aliyejitolea alifanya kazi ya kuajiriwa hadi saa 9:30 alasiri kisha akaenda kufanya kazi kwenye kituo cha usimamizi cha kutoa msaada hadi saa 4:00 usiku. Alisaidia pia mwishoni mwa juma. Anasema hivi: “Inaridhisha.”

Ama kweli, wafanyakazi hao na wengineo wote walikuwa tayari kusaidia kwa sababu ya upendo wao wa kidugu—kitambulisho cha Wakristo wa kweli. (Yohana 13:35) Meya wa Houston aliwaambia hivi Mashahidi kadhaa alipotembelea kituo cha usimamizi cha kazi hiyo ya kutoa msaada: “Mnaamini kwamba mnapaswa kufanya yale ambayo Mungu hutuambia tufanye. Mnatenda kulingana na imani yenu.”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Houston yakumbwa na mafuriko, mnamo Juni 9, 2001

[Hisani]

© Houston Chronicle

[Picha katika ukurasa wa 21]

Barabara kuu zilikuwa kama mito

[Picha katika ukurasa wa 21]

Maji yaliingia ndani ya nyumba

[Picha katika ukurasa wa 23]

Baadhi ya maelfu ya Mashahidi waliojitolea

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wapishi walitayarisha zaidi ya milo 250,000!

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

NOAA