Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uvumbuzi wa Kusisimua Kuhusu Jicho

Uvumbuzi wa Kusisimua Kuhusu Jicho

Uvumbuzi wa Kusisimua Kuhusu Jicho

KWA muda mrefu wanasayansi walijua kwamba macho ya wanyama wanaonyonyesha yana chembe za kupeleka habari ambazo huathiriwa na mwangaza na kudumisha saa ya mwili. Kwa muda mrefu ilidhaniwa kwamba kazi hiyo ya kutambua mwangaza ilifanywa na chembe ziitwazo rods na cones. Lakini mnamo mwaka wa 1999, kulingana na gazeti Science, watafiti walivumbua kwamba “panya ambao hawakuwa na chembe za rods na cones [hali inayowafanya kuwa vipofu] bado walidumisha saa ya mwilini inayoathiriwa na mwangaza.” Kwa hiyo, watafiti hao walifikia mkataa wa kwamba “kulikuwa na chembe nyingine ndani ya macho ambazo pia ziliathiriwa na mwangaza.”

Sasa chembe hizo zisizoonekana kwa urahisi zinazotambua mwangaza zimevumbuliwa. Ingawa chembe hizo huwa zimechangamana na chembe za rods na cones, “zinafanyiza mfumo tofauti wa kuona, unaotenda sambamba na mfumo ule mwingine wa kuona,” laeleza gazeti Science. Baadhi ya kazi za mfumo huo uliovumbuliwa ni kurekebisha ukubwa wa mboni ya jicho na kutoa homoni iitwayo melatonin, kurekebisha saa ya mwili ili iende sambamba na mzunguko wa mwangaza na giza. Pia mfumo huo unaweza kuchangia badiliko la hisia.

Kwa kupendeza, mfumo huo wa mwangaza hauathiriwi na mabadiliko madogo ya mwangaza, ila tu yale yanayodumu kwa muda mrefu, la sivyo saa ya mwili ingetatanika. Mwanasayansi mmoja alieleza uvumbuzi huo kuwa “wenye kusisimua” kisha akaongeza kusema kwamba “ulikuwa uvumbuzi mkubwa zaidi unaoonyesha chembe za wanyama wanaonyonyesha ambazo huathiriwa na mwangaza.”

Ni wazi kwamba kadiri tuendeleavyo kujua mambo mengi zaidi kuhusu uhai, ndivyo tunavyotambua ubuni uliofichika na ulio tata zaidi. Uvumbuzi kama huo huwasukuma wengi kusema maneno haya ya Biblia ya kumsifu Muumba: “Nakusifu maana nimefanywa kwa namna ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, wewe wanijua kabisa-kabisa.”—Zaburi 139:14, Biblia Habari Njema.