Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yajaribiwa Huko Slovakia

Imani Yajaribiwa Huko Slovakia

Imani Yajaribiwa Huko Slovakia

SIMULIZI LA JÁN BALI

NILIZALIWA mnamo Desemba 24, 1910, huko Záhor, kijiji kilicho mashariki mwa Slovakia leo. Wakati huo kijiji chetu kilikuwa sehemu ya Milki ya Austria na Hungaria. Mnamo mwaka wa 1913, Mama alinipeleka Marekani kujiunga na baba, aliyekuwa ameondoka Záhor mapema. Miaka miwili baada ya sisi kuwasili Gary, Indiana, dada yangu Anna, alizaliwa. Kisha Baba akaugua na kufa katika mwaka wa 1917.

Nilikuwa mwanafunzi mwenye bidii, na nilipenda dini sana. Nilipokuwa nikihudhuria mafundisho ya watoto ya siku ya Jumapili katika Kanisa la Calvin, mwalimu alitambua kuwa nilipenda mambo ya kiroho. Ili atosheleze njaa yangu ya kiroho, alinipa Biblia ya Holman iliyokuwa na maswali na majibu karibu 4,000. Hiyo ilikuwa habari chungu nzima kwa mtoto mwenye umri wa miaka 11.

‘Huu Ni Ukweli’

Katika miaka hiyo ya mapema, watu fulani katika ujirani wetu waliokuwa wametoka Slovakia wakawa Wanafunzi wa Biblia kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Mmoja wao alikuwa mjomba wangu, Michal Bali, ambaye alitufundisha kweli za Biblia. Hata hivyo, mnamo mwaka wa 1922, Mama, dada yangu na mimi tulirudi Záhor, mji ambao wakati huo ulikuwa sehemu ya Czechoslovakia mashariki.

Muda mfupi baadaye, mjomba wangu Michal alinitumia mabuku yote ya Studies in the Scriptures, yaliyoandikwa na Charles Taze Russell, na magazeti ya Mnara wa Mlinzi tangu nakala ya kwanza iliyoandikwa katika Julai 1, 1879. Nilivisoma vichapo vyote hivyo na kurudia sehemu fulani mara kadhaa, na nikasadikishwa kwamba nilikuwa nimepata ukweli wa Biblia niliokuwa nikitafuta.

Karibu na wakati huo, Wanafunzi fulani wa Biblia kutoka Marekani walirejea makwao Slovakia. Walifanyiza vikundi vya kwanza vya Kislovaki vya Wanafunzi wa Biblia nchini Czechoslovakia. Mama yangu na mimi tulihudhuria mikutano ya vikundi hivyo vya mapema katika kijiji chetu cha Záhor na kwingineko ujiranini.

Mikutano hiyo ilifanana na ile ya Wakristo wa karne ya kwanza. Tulikutana kwa ukawaida katika nyumba ya mmoja wa Wanafunzi wa Biblia, ambapo tuliketi kuzunguka meza na taa ya mafuta iliwekwa katikati. Nilikuwa mchanga kuliko wote, hivyo niliketi nyuma kidogo nikisikiliza gizani. Hata hivyo, wakati mwingine nilialikwa kushiriki. Wakati wengine waliposhindwa kuelewa jambo fulani katika usomaji wa Kislovaki, wangeniambia: “Naam, Ján, Kiingereza kinasemaje hapo?” Nilifanya hima kusonga karibu na taa na kueleza jinsi kichapo cha Kiingereza kilivyosema katika Kislovaki.

Michal Šalata alikuwa mmoja wa Wanafunzi wa Biblia waliorudi katika ile iliyokuja kuwa Czechoslovakia kutoka Marekani. Yeye alirejea kwenye kijiji jirani cha Sečovce alikoishi zamani, na akasaidia kupanga kazi ya kuhubiri nchini Czechoslovakia. Ndugu Šalata alienda nami kuhubiri. Halafu, mnamo mwaka wa 1924, nikiwa na umri wa miaka 13, nilimwomba anibatize. Ingawa Mama aliniona kuwa mchanga sana kuchukua hatua hiyo nzito, nilimsadikisha kwamba huo ulikuwa uamuzi wangu thabiti. Hivyo, katika kusanyiko la siku moja lililofanywa katika mwezi wa Julai karibu na Mto Ondava, nilibatizwa katika maji ya mto huo ili kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova.

Mapendeleo Mazuri ya Utumishi

Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 17, nilipata habari kwamba kulikuwa na mazishi yaliyokuwa yamepangwa kilometa chache kutoka kijiji nilimokuwa nikihubiri. Yalikuwa mazishi ya kwanza kufanywa na Wanafunzi wa Biblia katika eneo hilo. Nilipowasili, niliwapita watu wote na kwenda hadi alipokuwa msemaji. Aliniambia: “Nitazungumza kwanza, kisha utaendelea.”

Hotuba yangu ilitegemea andiko la 1 Petro 4:7, linalosema: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” Nilionyesha Maandiko yaliyosema kwamba hata mwisho wa mateso na kifo ulikuwa karibu, na pia nikaeleza kuhusu tumaini la ufufuo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Nilionekana nikiwa mdogo kuliko umri wangu. Pengine hiyo ndiyo sababu iliyowafanya watu wote wanisikilize kwa makini.

Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1931 lilikuwa na habari za kusisimua. Lilisema kwamba hatungejulikana kama Wanafunzi wa Biblia tena au kwa jina jingine lolote, bali tulitaka kuitwa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kusoma habari hizo, Wanafunzi wa Biblia katika eneo letu walipanga mkutano wa pekee. Karibu Wanafunzi wa Biblia 100 walikutana katika kijiji cha Pozdišovce. Nilipata pendeleo la kutoa hotuba yenye kichwa “Jina Jipya,” iliyotegemea makala hiyo ya Mnara wa Mlinzi.

Kulikuwa na shangwe nyingi wahudhuriaji walipoinua mikono yao, kuonyesha kwamba walikubali azimio ambalo waamini wenzao katika sehemu nyingine za ulimwengu walikuwa wamekubali. Halafu tukatuma telegramu kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, iliyosema: “Sisi, Mashahidi wa Yehova tuliokusanyika hapa Pozdišovce leo, tumekubali maelezo ya Mnara wa Mlinzi kuhusu jina jipya, na tunakubali kuitwa kwa jina hilo jipya, Mashahidi wa Yehova.”

Eneo kubwa la Slovakia na Transcarpathia, lililokuwa sehemu ya Czechoslovakia kabla ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, lilikuwa na matokeo mazuri katika huduma ya Kikristo. Tulihubiri eneo hilo kubwa kwa miguu, na pia kwa kutumia gari-moshi, basi, na baiskeli. Wakati huo tulitumia “Photo-Drama of Creation,” ambayo ilikuwa na picha na slaidi zilizoambatana na sauti, kuwahubiria watu katika majiji mengi. Baada ya kila onyesho, anwani za watu waliopendezwa ziliandikwa. Nilipewa anwani nyingi na kuombwa nipange Mashahidi wawatembelee watu waliopendezwa. Katika majiji fulani, tulikodi jumba na kisha nikatoa hotuba ya pekee kuhusiana na picha hizo.

Katika miaka ya 1930, nilipendelewa kuwa mjumbe kwenye makusanyiko makubwa kwenye jiji kuu la Prague. Katika mwaka wa 1932, kusanyiko la kwanza la kimataifa lilipangwa nchini Czechoslovakia. Tulikutana katika Jumba la Michezo ya Kuigiza la Varieté. Kichwa cha hotuba ya watu wote, “Ulaya Kabla ya Uharibifu,” kiliwavutia wengi, na karibu watu 1,500 walihudhuria. Kusanyiko jingine la kimataifa lilifanywa Prague mnamo mwaka wa 1937, na nilikuwa na pendeleo la kutoa hotuba moja. Wajumbe kutoka nchi nyingi za Ulaya walihudhuria, na sote tulitiwa moyo kuvumilia magumu yaliyofuata upesi wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu.

Ndoa, na Majaribu Makali

Tuliporudi Czechoslovakia, mimi na Mama tulishirikiana kwa ukaribu na Wanafunzi wa Biblia wenzetu kuhubiri katika kijiji jirani cha Pozdišovce. Huko nilikutana na Anna Rohálová, msichana mwenye kuvutia. Tulipokuwa wakubwa kidogo, tulitambua kuwa hisia zetu hazikuwa zile za upendo wa kawaida tu kati ya ndugu na dada Wakristo. Mnamo mwaka wa 1937, tulioana. Kuanzia wakati huo, Anna alinitegemeza, hata wakati wa “majira yenye taabu” yaliyokuwa karibu.—2 Timotheo 4:2.

Muda mfupi baada ya arusi yetu, ilibainika wazi kwamba Ulaya ilikuwa ikijitayarisha kwa ajili ya Vita ya Pili ya Ulimwengu. Kufikia Novemba 1938, sehemu za kusini za Transcarpathia na Slovakia zilinyakuliwa na Hungaria ikishirikiana na Ujerumani ya Nazi. Mikutano yetu ilipigwa marufuku na polisi wa Hungaria na ilitubidi kuripoti katika kituo cha polisi mara kwa mara.

Vita ya Pili ya Ulimwengu ilipoanza mnamo Septemba 1939, baadhi yetu kutoka Záhor, wanaume kwa wanawake, tulikamatwa na kupelekwa katika jumba moja la kale la kifalme karibu na Mukacheve, mji ulio katika eneo la Ukrainia leo. Huko tuliwapata Mashahidi wengi kutoka makutaniko ya Transcarpathia. Baada ya kuhojiwa kwa muda wa miezi mitatu au minne na kupigwa mara kwa mara, tulipelekwa katika mahakama maalumu ya kijeshi. Sote tuliulizwa swali moja tu: “Je, mtakubali kupigana katika vita ya Hungaria dhidi ya Muungano wa Sovieti?” Tulikataa na tukahukumiwa na kupelekwa kwenye gereza la Budapest, Hungaria, katika barabara ya 85 Margit Boulevard.

Wafungwa wote walipewa chakula kidogo sana. Punde magonjwa yakaanza kuenea na wafungwa wakaanza kufa. Mke wangu alisafiri mwendo wote huo kutoka Záhor kuja kuniona. Nilifurahi sana! Ingawa tulizungumza tu kwa dakika tano hivi kupitia vyuma vya gereza, nilimshukuru Yehova kwa kupata mwenzi mwaminifu kama huyo. *

Kutoka Gereza Hadi Kambi ya Kazi Ngumu

Kutoka gereza hilo nilipelekwa moja kwa moja hadi Jászberény, Hungaria, ambapo niliwakuta Mashahidi 160. Huko afisa Mhungaria alitupatia nafasi ya mwisho kutoka kwa serikali ya Hungaria akisema: “Yeyote aliye tayari kutumika jeshini, aje hapa mbele.” Hakuna aliyejitokeza. Afisa huyo akasema: “Ingawa sikubaliani na mambo mnayofanya, ninavutiwa na imani yenu thabiti.”

Siku chache baadaye, tulipanda meli katika Mto Danube na kusafiri kuelekea kambi ya kazi ngumu karibu na jiji la Bor, Yugoslavia. Tulipokuwa melini, wanajeshi na kamanda wao walijaribu mara nyingi kutushawishi tukane imani yetu. Kamanda aliwaamuru wanajeshi watupige kwa bunduki zao, buti zao, na kututesa kwa njia nyinginezo.

Tulipokewa na kamanda wa kambi ya kazi ngumu ya Bor, Luteni Kanali András Balogh, ambaye alituambia: “Iwapo yale nimeambiwa kuwahusu ni kweli, mtakufa baada ya muda mfupi.” Hata hivyo, aliposoma barua iliyokuwa imefungwa kutoka kwa maafisa wa serikali, alitutendea kwa heshima. Balogh alitupatia kiasi fulani cha uhuru wa kutembea na hata akaturuhusu tujijengee makao yetu. Ingawa chakula kilikuwa haba, tulikuwa na chumba chetu cha kupikia, hivyo chakula kiligawanywa kwa usawa.

Mnamo Machi 1944, Ujerumani ilianza kunyakua eneo la Hungaria. Wakati huo, kamanda aliyependelea Unazi, Ede Marányi alichukua mahali pa Balogh. Alianzisha sheria kali kama za kambi za mateso. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, majeshi ya Urusi yalikaribia, na wafungwa katika kambi ya Bor walihamishwa. Baadaye, tulipokuwa tukihamishwa kwa miguu, tulijionea maangamizi ya Wayahudi huko Cservenka. Tuliona kuokoka kwetu kuwa muujiza.

Tulipofika kwenye mpaka wa Hungaria na Austria, tuliamuriwa kuchimba mashimo ya kuweka bunduki za rashasha. Tulieleza kwamba sababu iliyotufanya tuwe wafungwa ilikuwa kukataa kujihusisha na shughuli za kijeshi. Kwa kuwa nilikuwa mbele ya kikundi, afisa Mhungaria alinishika na kuanza kunipiga. “Nitakuua,” akasema kwa sauti. “Usipofanya kazi, wengine watafuata mfano wako mbaya!” András Bartha, Shahidi mwenye umri mkubwa aliyekuwa ameongoza kupanga kazi yetu ya kuhubiri aliingilia kati na hilo liliokoa uhai wangu. *

Majuma machache baadaye, vita ilimalizika na tukashika njia ya kurudi nyumbani. Wafungwa wengine waliokuwa wameachiliwa kutoka Bor, waliripoti kwamba sote tuliopelekwa Cservenka tulikuwa tumeuawa. Kwa hiyo, kwa muda wa miezi sita, mke wangu alijiona kuwa mjane. Alishangaa sana siku moja kuniona nimesimama mlangoni! Tulitokwa na machozi mengi tulipokumbatiana baada ya kutenganishwa kwa miaka mingi.

Kupanga Upya Kazi

Baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, Slovakia iliunganishwa tena na Czechia na kuwa Czechoslovakia. Hata hivyo, Transcarpathia, ambayo sehemu yake kubwa ilikuwa sehemu ya Czechoslovakia kabla ya vita, ikawa sehemu ya Ukrainia ambayo ilikuwa katika Muungano wa Sovieti. Mnamo mwaka wa 1945, Michal Moskal na mimi tulienda Bratislava, ambao sasa ni mji mkuu wa Slovakia, ili kukutana na ndugu wenye madaraka kwa kusudi la kupanga upya kazi ya kuhubiri. Ingawa tulikuwa tumechoka kimwili na kihisia, tuliazimia kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14; 28:18-20.

Baada ya vita, makusanyiko yalitupatia nguvu mpya ya kuendelea na kazi yetu. Mnamo Septemba 1946 kusanyiko la kwanza la nchi nzima lilifanywa katika jiji la Brno. Nilipendelewa kutoa hotuba yenye kichwa “Mavuno, Mwisho wa Ulimwengu.”

Mnamo mwaka wa 1947 kusanyiko jingine la kitaifa lilifanywa huko Brno. Wakati huo, Nathan H. Knorr, Milton G. Henschel, na Hayden C. Covington, waliozuru kutoka makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, walitoa hotuba zenye kutia moyo. Nilipendelewa kutafsiri hotuba zao. Ijapokuwa tulikuwa wahubiri 1,400 hivi wa Ufalme huko Czechoslovakia wakati huo, karibu watu 2,300 walihudhuria hotuba ya watu wote.

Minyanyaso Chini ya Wakomunisti

Mnamo mwaka wa 1948, nchi ilianza kutawaliwa na Wakomunisti, na punde kazi yetu ikapigwa marufuku kwa miaka 40. Mnamo mwaka wa 1952, wengi wetu waliodhaniwa na wenye mamlaka kuwa viongozi walitiwa gerezani. Wengi walishtakiwa kuwa walitaka kupindua serikali, lakini wachache kati yetu walishtakiwa kwa uhaini. Nilitiwa gerezani na kuhojiwa kwa miezi 18. Nilipouliza jinsi nilivyokuwa msaliti, hakimu alisema: “Ulikuwa ukisema kuhusu Ufalme wa Mungu. Na unasema kwamba huo utachukua mamlaka ya ulimwengu. Hiyo inatia ndani Czechoslovakia.”

“Ikiwa ni hivyo,” nikajibu, “unapaswa kuwahukumu kuwa wasaliti wote ambao husali ile Sala ya Bwana na kuomba ‘Ufalme wa Mungu uje.’” Hata hivyo, nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano na nusu gerezani katika gereza maarufu la Kikomunisti la Jáchymov, huko Czechoslovakia.

Baada ya kutumikia karibu kifungo changu chote, nilifunguliwa. Mke wangu, Anna, alinitegemeza kwa uaminifu kupitia barua na kunitembelea na vilevile kumtunza binti yetu Mária. Hatimaye, tuliungana tena kama jamaa, na kuendelea na shughuli zetu za Kikristo, tulizofanya kichinichini.

Maisha Yenye Kuridhisha Katika Utumishi wa Yehova

Kwa miaka 70 na zaidi, Mashahidi wa Yehova katika eneo letu wamemtumikia Mungu chini ya hali tofauti-tofauti, hasa chini ya utawala wa Kikomunisti. Kweli, mimi ni mzee na dhaifu kimwili, lakini, bado ninatumikia nikiwa mzee Mkristo katika kutaniko la Záhor, pamoja na ndugu wengine waaminifu kama vile Ján Korpa-Ondo, aliye na umri wa miaka 98. * Mke wangu mpendwa, zawadi halisi kutoka kwa Yehova, alikufa katika mwaka wa 1996.

Ningali nakumbuka kinaganaga jambo lililoelezwa katika ukurasa wa 228 hadi 231 wa kitabu The Way to Paradise, kilichochapishwa katika mwaka wa 1924. Msomaji aliombwa awazie akiwa kwenye Paradiso, akiwasikiliza watu wawili waliokuwa wamefufuliwa. Watu hao hawakujua walimokuwa. Halafu mtu mmoja aliyekuwa ameokoka vita ya Har–Magedoni alikuwa na pendeleo la kuwaeleza kwamba wamefufuliwa kwenye Paradiso. (Luka 23:43) Iwapo nitaokoka Har–Magedoni, ningependa kumweleza mke wangu, mama yangu, na wapendwa wengine mambo hayo watakapofufuliwa. Lakini nikifa kabla ya vita hiyo, ninatazamia kwamba mtu fulani ataniambia kuhusu mambo yatakayotukia baada ya kifo changu.

Sasa ninaendelea kufurahia pendeleo la pekee na la ajabu kabisa la kumkaribia na kuzungumza na Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Azimio langu ni kuendelea kuishi kupatana na maneno ya mtume Paulo katika Waroma 14:8: “Tukiishi, twaishi kwa Yehova, na tukifa, twafa kwa Yehova pia. Kwa hiyo tukiishi na tukifa pia, sisi ni wa Yehova.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Ona simulizi la Andrej Hanák katika gazeti la Amkeni! la Aprili 22, 2002, ukurasa wa 19-24. Simulizi hilo limeelezea hali za jela hilo na vilevile matukio ya Cservenka, ambayo yametajwa baadaye katika makala hii.

^ fu. 28 Kwa habari zaidi kuhusu András Bartha, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1993, ukurasa wa 11.

^ fu. 39 Ona simulizi lake la maisha katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1998, ukurasa wa 24-28.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na Anna, mwaka mmoja baada ya kuoana

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa na Nathan H. Knorr kwenye kusanyiko la mwaka wa 1947 huko Brno