Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kuepuka Kuathiriwa na Vijana Wenzangu?

Nawezaje Kuepuka Kuathiriwa na Vijana Wenzangu?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kuepuka Kuathiriwa na Vijana Wenzangu?

“Uvutano wa marika uko kila mahali.”—Jesse, mwenye umri wa miaka 16.

“Hali moja ngumu sana niliyokabili nilipokuwa kijana ni ule uvutano wa wanashule wenzangu.”—Johnathan, mwenye umri wa miaka 21.

AMA KWELI, uvutano wa marika ni wenye nguvu sana. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kuukinza. Kwa hakika, unaweza kuushinda na hata kuutumia kwa faida yako. Vipi?

Katika makala iliyotangulia ya mfululizo huu, tulizungumzia hatua ya kwanza iliyo muhimu sana: Tambua kwamba marika wako wanaweza kukuathiri sana. * Ni hatua gani nyingine unazoweza kuchukua? Unahitaji mwongozo ulio katika Neno la Mungu. Mithali 24:5 inasema hivi: “Mtu wa maarifa huongeza uwezo.” Unahitaji maarifa ya aina gani ili upate nguvu zaidi za kushinda uvutano wa marika? Kabla hatujajibu swali hilo, hebu kwanza tuzungumzie tatizo moja linaloweza kufanya uathiriwe sana na marika wako.

Kutojiamini Ni Hatari

Nyakati nyingine vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova huhitaji kujikakamua kushinda uvutano wa marika kwa sababu maisha yao yanahusisha kuwaeleza wengine yale wanayoamini. (Mathayo 28:19, 20) Je, nyakati nyingine wewe hushindwa kuwaeleza vijana wenzako yale unayoamini? Vijana wengine pia huhisi hivyo. Melanie, mwenye umri wa miaka 18, anasema: “Lilikuwa jambo gumu sana kuwaeleza vijana wenzangu kwamba mimi ni Shahidi.” Anaongeza hivi: “Nilipopata ujasiri wa kuwaeleza kwamba mimi ni Shahidi, woga uliniingia tena.” Yaonekana alisitasita kwa sababu ya kuathiriwa na marika wake.

Biblia inaeleza kwamba hata wanaume na wanawake wenye imani yenye nguvu waliogopa kuwaeleza wengine kumhusu Mungu. Kwa mfano, kijana Yeremia alijua kwamba angedhihakiwa na kunyanyaswa iwapo angetii amri ya Mungu ya kuhubiri kwa ujasiri. Isitoshe, Yeremia hakujiamini. Kwa nini? Alimwambia Mungu: “Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Je, Mungu alikubali kwamba Yeremia hakustahili kusema kwa sababu alikuwa kijana? La. Yehova alimhakikishia nabii huyo hivi: “Usiseme, mimi ni mtoto.” Kisha Yehova akampa kijana huyo mwenye kusitasita kazi muhimu.—Yeremia 1:6, 7.

Tusipojiamini, tunaweza kuathiriwa na marika kwa urahisi sana. Uchunguzi umeonyesha jambo hilo. Kwa mfano, katika mwaka 1937, mwanasayansi mmoja aliyeitwa Muzafer Sherif alifanya jaribio maarufu. Aliwaweka watu katika chumba chenye giza na kuwaonyesha mwangaza mdogo sana, kisha akawaomba waseme umbali ambao mwangaza huo umesonga.

Ama kweli, mwangaza haukusonga hata kidogo; macho yaliwadanganya tu. Walipojaribiwa wakiwa mmoja-mmoja, walitoa makadirio tofauti-tofauti kuonyesha umbali ambao mwangaza umesonga. Hata hivyo, walipokusanywa pamoja katika vikundi waliombwa waseme makadirio yao kwa sauti. Ikawaje? Kwa kuwa hawakujiamini, kila mmoja aliathiriwa na mwingine. Walipojaribiwa tena na tena, majibu yao yalikaribiana sana hadi kila “kikundi kikawa na jibu moja tu.” Watu hao walipojaribiwa tena wakiwa mmoja-mmoja walitoa jibu lilelile la kikundi chao.

Jaribio hilo linaonyesha jambo moja la maana. Watu wasiojiamini huathiriwa zaidi na marika. Ama kwa hakika, hilo ni jambo linalopaswa kutiliwa maanani. Maoni ya watu kuhusu masuala muhimu kama vile ngono kabla ya ndoa, matumizi ya dawa za kulevya, na hata miradi yanaweza kuathiriwa na yale ya marika wao. Tukiruhusu maoni ya “kikundi” yaathiri maoni yetu kuhusu mambo hayo, hilo linaweza kuathiri sana maisha yetu ya wakati ujao. (Kutoka 23:2) Tunaweza kuchukua hatua gani?

Tuseme ungeshirikishwa katika jaribio hilo, wewe ungejibuje iwapo ungejua kwa hakika kwamba mwangaza huo haukusonga? Labda hungeathiriwa na kikundi. Naam, tunapaswa kujiamini. Lakini kujiamini kunahusisha nini, nasi tunawezaje kusitawisha hali hiyo?

Mfanye Yehova Kuwa Tumaini Lako

Huenda umesikia habari nyingi kuhusu kusitawisha hali ya kujiamini. Lakini kuna maoni mbalimbali kuhusu jinsi unavyoweza kusitawisha hali hiyo na kiwango cha kujiamini unachopaswa kufikia. Biblia inatoa shauri hili la busara: “Naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu.” (Waroma 12:3) Tafsiri nyingine ya mstari huo inasema hivi: “Ninamwambia kila mmoja wenu asijikadirie zaidi kuliko alivyo kikweli, lakini ajikadirie kwa kiasi.”—Charles B. Williams.

‘Ukikadiria kwa kiasi’ jinsi ‘ulivyo kikweli’ hutajitutumua wala kujivuna. Badala yake, ukiwa na maoni hayo yanayofaa utakuwa na uhakika katika uwezo wako halisi wa kufikiri, kuelewa mambo, na kufanya maamuzi ya busara. Muumba wako alikupa ‘nguvu za kufikiri,’ na hiyo ni zawadi kubwa sana. (Waroma 12:1) Kukumbuka jambo hilo kutakusaidia usikubali watu wengine wakuamulie mambo. Hata hivyo, kuna jambo jingine ambalo linaweza kukusaidia hata zaidi.

Mfalme Daudi aliongozwa na Mungu kuandika hivi: “Ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, tumaini langu tokea ujana wangu.” (Zaburi 71:5) Naam, Daudi alimfanya Baba yake wa mbinguni kuwa tumaini lake tangu ujanani. Alikuwa “kijana tu”—labda hata tineja—wakati lile jitu la Ufilisti Goliathi lilipotaka kupigana uso kwa uso na askari mmoja tu wa Israeli. Maaskari waliogopa. (1 Samweli 17:11, 33) Huenda walitiana woga. Hapana shaka kwamba walizungumza kwa hofu kuhusu ukubwa na ushujaa wa Goliathi na kusema kwamba mtu mwenye kichaa ndiye tu angepigana naye. Daudi hakuathiriwa na maoni hayo. Kwa nini?

Ona maneno ambayo Daudi alimwambia Goliathi: “Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.” (1 Samweli 17:45) Daudi alifahamu ukubwa wa Goliathi, nguvu zake, na silaha alizotumia. Lakini alijua jambo jingine kwa uhakika sawa na alivyofahamu kwamba kuna anga juu yake. Alijua kwamba Goliathi hakuwa kitu kwa kulinganishwa na Yehova Mungu. Ikiwa Yehova alikuwa upande wa Daudi, ya nini amwogope Goliathi? Imani hiyo katika Mungu ilimfanya Daudi ajihisi salama. Hata ikiwa angeshawishiwa na watu kwa njia yoyote ile, yeye hangeyumbayumba.

Je, unamwamini Yehova hivyo? Yeye hajabadilika tangu wakati wa Daudi. (Malaki 3:6; Yakobo 1:17) Kadiri unavyojifunza juu yake, ndivyo utakavyoamini yote anayokuambia katika Neno lake. (Yohana 17:17) Katika Neno lake utapata viwango thabiti na vyenye kutegemeka ambavyo vitakuongoza maishani na kukusaidia kuepuka kuathiriwa na vijana wenzako. Zaidi ya kumfanya Yehova kuwa tumaini lako, kuna jambo jingine unaloweza kufanya.

Chagua Washauri Wazuri

Neno la Mungu hukazia uhitaji wa kutafuta mwongozo mzuri. Mithali 1:5 inasema hivi, kulingana na Biblia Habari Njema: “Mwenye busara apate mwongozo.” Wazazi wako, wanaokujali sana, wanaweza kukupa mwongozo. Indira anakubali jambo hilo. Anasema hivi: “Niko katika kweli kwa sababu wazazi wangu sikuzote walinisaidia kwa kutumia Maandiko na kunifanya nimwone Yehova akiwa halisi maishani mwangu.” Vijana wengi wanakubaliana naye pia.

Ikiwa wewe ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo, basi unaweza kupata utegemezo mzuri kutoka kwa waangalizi waliowekwa rasmi, au wazee, na pia Wakristo wengine waliokomaa. Kijana aitwaye Nadia anasema hivi: “Niliwaheshimu sana wazee wa kutaniko letu. Nakumbuka mwangalizi-msimamizi alitoa hotuba moja iliyotayarishwa hasa kwa ajili ya vijana. Baada ya mkutano huo mimi na rafiki yangu tulikuwa na furaha sana kwa sababu alizungumzia mambo ambayo tulikuwa tukikabiliana nayo.”

Uvutano unaofaa wa marika unaweza kukusaidia pia kuepuka kuathiriwa na vijana wenzako. Ukichagua marafiki wako kwa hekima, wanaweza kukusaidia kushikilia miradi mizuri na viwango vinavyofaa. Tunawezaje kuchagua marafiki wanaofaa? Kumbuka shauri hili: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Nadia alijitahidi kuchagua marafiki wenye hekima shuleni—waamini wenzake, ambao walifuata kanuni zilezile za maadili alizofuata. Anakumbuka hivi: “Wakati wavulana shuleni walipokuja ‘kuzungumza’ nasi, sisi vijana Mashahidi tulitegemezana.” Marafiki wazuri wanaweza kutusaidia kuwa na sifa bora. Jitihada ya kuchagua marafiki wa aina hiyo si ya bure.

Basi, uwe na hakika kwamba ukimfanya Yehova awe tumaini lako, ukitafuta mwongozo kutoka kwa Wakristo wakomavu, na kuchagua marafiki wako kwa hekima, unaweza kuepuka kuathiriwa na vijana wenzako. Ama kwa hakika, unaweza kuwasaidia marafiki wako kubaki katika barabara ya uhai kama wewe.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona makala “Je, Vijana Wenzako Wanaweza Kukuathiri Sana?” katika toleo la Amkeni! la Novemba 22, 2002.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

Tafuta marafiki wazuri, wanaompenda Mungu na viwango vyake kama wewe

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.”—1 Wakorintho 15:33

“Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima.” —Mithali 13:20