Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Wakristo Wawe Maskini?

Je, Ni Lazima Wakristo Wawe Maskini?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Lazima Wakristo Wawe Maskini?

WAKATI mmoja Yesu alimwambia mtawala fulani kijana aliyekuwa tajiri aende auze mali zake na kuwagawia maskini. Simulizi hilo lasema kwamba mwanamume huyo alihuzunishwa na usemi wa Yesu na akaenda zake akiwa ametiwa kihoro, “kwa maana alikuwa na miliki nyingi.” Halafu Yesu akawaambia wanafunzi wake hivi: “Jinsi litakavyokuwa jambo gumu kwa wale wenye fedha kuingia katika ufalme wa Mungu!” Kisha Yesu akasema: “Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko kwa mtu tajiri kupata kuingia katika ufalme wa Mungu.”—Marko 10:21-23; Mathayo 19:24.

Yesu alimaanisha nini? Kwamba utajiri na ibada ya kweli havipatani hata kidogo? Je, Wakristo wanapaswa kuhisi wakiwa na hatia ikiwa wana pesa? Je, Mungu huwataka waishi maisha ya kujinyima sana yasiyo na raha yoyote?

Mungu Huwakaribisha “Watu wa Namna Zote”

Nyakati za kale, Mungu hakutaka Waisraeli waishi maisha ya umaskini. Fikiria hili: Waisraeli walipoingia nchi ambayo Mungu alikuwa amewapa, walilima na kufanya biashara ili kutimiza mahitaji yao na ya wapendwa wao. Mambo kama vile hali za kiuchumi, hali ya hewa, afya, au ustadi wa mtu wa kufanya biashara ungeamua iwapo angefanikiwa au la. Sheria ya Musa iliwataka Waisraeli wamhurumie yeyote aliyeteseka kwa sababu za kiuchumi au aliyekuwa maskini. (Mambo ya Walawi 25:35-40) Kwa upande mwingine, watu fulani walikuwa matajiri. Boazi, mwanamume mwenye imani na mwaminifu ambaye alikuja kuwa babu ya Yesu Kristo, hutajwa kuwa “mtu mkuu mwenye mali.”—Ruthu 2:1.

Ilikuwa hivyo pia wakati wa Yesu. Alipokuwa akizungumza na mwanamume tajiri aliyetajwa mwanzoni, Yesu hakuwa na nia ya kuwatia moyo watu waishi maisha ya kujinyima yasiyo na raha yoyote. Badala yake, alikuwa akifundisha somo la maana. Kwa maoni ya wanadamu, huenda likaonekana kuwa jambo gumu kwa matajiri kunyenyekea na kukubali njia ya Mungu ya wokovu. Hata hivyo, Yesu alisema: “Kwa wanadamu hilo haliwezekani, bali kwa Mungu mambo yote yawezekana.”—Mathayo 19:26.

Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza liliwakaribisha “watu wa namna zote.” (1 Timotheo 2:4) Baadhi ya watu hao walikuwa matajiri, wengine waliweza kujitosheleza maishani, na wengi walikuwa maskini. Wengine walikuwa wamekusanya mali kabla ya kuwa Wakristo. Baadaye hali ziliporuhusu, wengine walifanya biashara kwa hekima na wakapata mali.

Vivyo hivyo, udugu wetu wa Kikristo leo unatia ndani watu wenye hali tofauti-tofauti kiuchumi. Wote hujitahidi kufuata mwongozo wa Biblia kuhusu mambo ya kifedha, kwa sababu kupenda mali kunaweza kumwathiri mtu yeyote. Somo ambalo Yesu alifundisha kuhusu yule mtawala kijana aliyekuwa tajiri huwatahadharisha Wakristo wote kuhusu jinsi ambavyo pesa na mali zinavyoweza kumdhibiti mtu.—Marko 4:19.

Onyo kwa Matajiri

Ingawa Biblia hailaumu kuwa na mali, inalaumu kupenda fedha. Mwandishi wa Biblia Paulo alisema hivi: “Kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote.” Alisema kwamba kwa kupuuza mambo ya kiroho kwa sababu ya kutamani utajiri, “wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Kwa kupendeza, Paulo aliwapa matajiri maagizo hususa. Alisema: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo uliopo wasiwe wenye kunia ya juu, na waweke tumaini lao, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.” (1 Timotheo 6:17) Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba matajiri wanakabili hatari ya kuwa na kiburi na kujiona wakiwa bora kuliko watu wengine. Pia, huenda wakashawishiwa kufikiri kwamba mali zinaweza kuwapa usalama wa kweli—jambo ambalo ni Mungu pekee anayeweza kutoa kwa ukamili.

Wakristo matajiri wanaweza kujilinda na hatari hizo kwa kuwa “matajiri katika kazi zilizo bora.” Kazi hizo zinatia ndani kuwa “wakarimu, tayari kushiriki,” kwa kuwasaidia wale wenye uhitaji. (1 Timotheo 6:18) Wakristo—matajiri kwa maskini—wanaweza kutumia baadhi ya mali zao kueneza habari njema za Ufalme wa Mungu, ambalo ndilo jambo la maana zaidi kwa Wakristo wa kweli leo. Roho hiyo ya ukarimu huonyesha mtazamo unaofaa kuelekea mali za kimwili, na humpendeza Yehova Mungu na Yesu Kristo, ambao hupenda watoaji wachangamfu.—Mathayo 24:14; Luka 16:9; 2 Wakorintho 9:7.

Mambo Yaliyo ya Maana Zaidi

Ni wazi kwamba si lazima Wakristo wawe maskini. Lakini, hawapaswi ‘kuazimia kuwa matajiri.’ (1 Timotheo 6:9) Wao hufanya kazi kwa bidii ili waweze kujitosheleza maishani. Ikitegemea hali fulani-fulani na uchumi wa mahali wanapoishi, jitihada zao zitafanikiwa kwa njia tofauti-tofauti.—Mhubiri 11:6.

Haidhuru hali zao za kifedha, Wakristo wanapaswa kujitahidi “kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Kwa kutanguliza mambo ya kiroho, Wakristo ‘hujiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.’—1 Timotheo 6:19.