Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahakama ya Juu Yatetea Uhuru wa Kusema

Mahakama ya Juu Yatetea Uhuru wa Kusema

Mahakama ya Juu Yatetea Uhuru wa Kusema

JUNI 17, 2002, ilikuwa siku muhimu wakati ambapo Mahakama ya Juu ilichapisha hati yenye uamuzi wake. Mahakama iliamuaje? Vichwa vya habari magazetini vilitangaza uamuzi huo. Gazeti The New York Times lilitangaza hivi: “Mahakama Yaondoa Vizuizi vya Ziara za Mashahidi wa Yehova.” Gazeti The Columbus Dispatch la Ohio lilisema: “Mahakama Kuu Yabatilisha Amri ya Kutaka Kibali.” Gazeti The Plain Dealer la Cleveland, Ohio, lilikuwa na kichwa hiki sahili: “Waombaji Hawahitaji Kibali cha Baraza la Jiji.” Na katika gazeti USA Today, ukurasa unaoambatana na ule wa mhariri ulitangaza hivi: “Uhuru wa Kusema Washinda.”

Maamuzi ya mahakama za chini dhidi ya Mashahidi wa Yehova yalibatilishwa kwa kura ya 8 kwa 1! Hati rasmi yenye uamuzi wa Mahakama ambayo ilikuwa na kurasa 18, iliandikwa na Jaji John Paul Stevens. Kwa mara nyingine tena, uamuzi huo uliunga mkono haki zinazoonyeshwa katika Marekebisho ya Kwanza ambazo zinatetea huduma ya hadharani ya Mashahidi wa Yehova. Katika hati hiyo, Mahakama ilieleza kwamba Mashahidi hawakuomba kibali kwa sababu wanadai kuwa “mamlaka yao ya kuhubiri inatoka katika Maandiko.” Kisha Mahakama ikanukuu ushahidi uliotolewa katika hati ya malalamishi ya Mashahidi: “Kwa maoni yetu, kuomba kibali cha manispaa ili kuhubiri ni kama kumtukana Mungu.”

Hati yenye uamuzi wa Mahakama ilisema: “Kwa zaidi ya miaka 50, Mahakama imeondoa vizuizi vya kwenda nyumba hadi nyumba na kugawanya vijitabu. Haishangazi kwamba kesi nyingi kati ya hizo zilihusu haki za Marekebisho ya Kwanza zilizowasilishwa na Mashahidi wa Yehova, kwani dini yao inawataka waende kuzungumza na watu nyumba hadi nyumba. Kama tulivyoona katika kesi ya Murdock v. Pennsylvania,. . . (1943), Mashahidi wa Yehova wanadai kufuata mfano wa Paulo, kwa kufundisha “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.” Matendo 20:20. Wanafuata kabisa agizo hili la Maandiko, “Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.” Marko 16:15. Kwa kufanya hivyo wanaamini kwamba wanatii amri ya Mungu.’”

Kisha Hati yenye uamuzi ikanukuu tena kesi ya mwaka 1943: “Katika Marekebisho ya Kwanza, shughuli hiyo ya kidini ina umuhimu uleule kama ibada inayofanywa makanisani na mahubiri yanayofanywa na mapadri. Haki zinazohusu shughuli nyingine za kawaida za kidini ambazo zinakubalika zinahusu pia shughuli hiyo.” Hati hiyo pia ilinukuu kesi nyingine ya mwaka 1939 iliyosema: ‘Kuweka mipaka kwa kuwadai watu wapate leseni huzuia ugawanyaji wa vijitabu kwa uhuru na bila vizuizi na kuingilia haki za msingi za kikatiba.’

Kisha Mahakama ikatoa taarifa hii muhimu: “Kesi hizo zinaonyesha kwamba kwa kupinga vizuizi vya uhuru wa kusema Mashahidi wa Yehova hawajapigania haki zao wenyewe tu.” Hati hiyo ilieleza kwamba ‘si Mashahidi tu wanaokabili hatari ya kunyamazishwa na amri kama ile iliyotolewa na wenye mamlaka wa Stratton.’

Hati hiyo iliendelea kusema kwamba amri hiyo “inadharau kanuni zinazotetewa na Marekebisho ya Kwanza na vilevile wazo la kuwa na jamii huru. Ni jambo lenye kuudhi kwamba katika mazungumzo ya kawaida, raia anapaswa kwanza kuifahamisha serikali kuwa angependa kuzungumza na majirani wake kisha apate kibali cha kufanya hivyo. . . . Sheria inayodai watu wapate kibali ili wawe na mazungumzo hayo inakiuka kabisa urithi wetu wa kitaifa na katiba yetu.” Kisha Hati hiyo ikataja “athari kubwa sana za amri hiyo ya kupata kibali.”

Hatari ya Uhalifu

Vipi juu ya yale maoni ya kwamba kibali hicho kinawalinda watu dhidi ya wakora wanaovunja nyumba na wahalifu wengine? Mahakama ilitoa kauli hii: “Ijapokuwa tunakubali kwamba mahangaiko hayo ni ya kweli, kesi zinazotangulia zinaonyesha wazi kwamba tunapaswa kuwa na usawaziko tunapozingatia mahangaiko hayo na vilevile jinsi ambavyo amri zinazotolewa zinavyoathiri haki za Marekebisho ya Kwanza.”

Hati hiyo ya Mahakama iliendelea kusema: “Haielekei kwamba wahalifu watazuiwa wasifike kwenye nyumba za watu na kuzungumza mambo ambayo hayakutajwa katika amri hiyo eti kwa sababu hawana kibali. Wahalifu wanaweza kuomba waonyeshwe njia au kuomba ruhusa ya kutumia simu, . . . au huenda wakapata kibali kwa kutumia jina bandia na waepuke kuadhibiwa.”

Kwa kurejelea maamuzi yaliyofanywa katika miaka ya 1940, Mahakama iliandika hivi: “Maneno yaliyo katika hati za maamuzi za kipindi cha Vita ya Pili ya Ulimwengu ambazo zilizuia washiriki wenzi wa walalamishi [Watch Tower Society] wasishtakiwe kwa mashtaka madogo-madogo, yanaonyesha jinsi Mahakama inavyozingatia haki zinazopatikana katika Marekebisho ya Kwanza ambazo zinahusiana na kesi hii.”

Uamuzi wa mwisho wa Mahakama ulikuwa nini? “Hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Rufaa imebatilishwa, na kesi imerudishwa kwenye mahakama hiyo ili hatua zaidi za kisheria zichukuliwe kupatana na hati hii. Hiyo ndiyo amri ya mahakama.”

Basi, kama ilivyotaarifiwa katika gazeti Chicago Sun-Times, ‘Mahakama Iliunga Mkono Mashahidi wa Yehova,’ kwa kura ya 8 kwa 1.

Vipi Juu ya Wakati Ujao?

Mashahidi wa Yehova katika Kutaniko jirani la Wellsville wameuonaje ushindi huo mbele ya Mahakama ya Juu? Ama kweli, hawana haja ya kujivuna wala kuwaaibisha wakazi wa Stratton kwa sababu ya ushindi wao. Mashahidi hawana kinyongo na wakazi wenye kuheshimika wa kijiji hicho. Gregory Kuhar, Shahidi anayekaa katika eneo hilo, alisema: “Hatukudhamiria kuwa na kesi kama hiyo. Amri ya kijiji ndiyo haikuwa halali. Yale tuliyoyafanya hayakuwa kwa faida yetu tu, bali kwa faida ya watu wote.”

Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba Mashahidi wameepuka kabisa kuwachokoza wanakijiji hao. Shahidi mwingine anayeitwa Gene Koontz alieleza hivi: “Mara yetu ya mwisho kuhubiri Stratton ilikuwa Machi 7, 1998—zaidi ya miaka minne iliyopita.” Aliongeza hivi: “Niliambiwa kwamba ningekamatwa. Katika miaka iliyopita, ripoti nyingi zilionyesha kwamba polisi walitaka kutukamata. Halafu tulipoomba tuonyeshwe hati rasmi yenye amri hiyo, hatukupata majibu.”

Koontz aliongeza hivi: “Tungependa kuwa na uhusiano mwema na majirani wetu. Ikiwa wengine hawataki tuwatembelee, tunaheshimu uamuzi wao. Lakini kuna wengine ambao ni wenye urafiki na wangetaka tuzungumze nao kuhusu Biblia.”

Gregory Kuhar alieleza hivi: “Hatukufuatilia kesi hiyo ili kuwaudhi wenyeji wa Stratton. Tulitaka tu kutetea kisheria uhuru wetu wa kusema kupatana na Katiba.”

Aliendelea kusema: “Muda si muda, tunatarajia kurudi Stratton. Ningependa kuwa wa kwanza kubisha mlango tunaporudi huko. Kwa kupatana na amri ya Kristo, ni lazima turudi.”

Kesi ya “Watchtower v. Village of Stratton” imekuwa na matokeo makubwa. Baada ya kupata habari kuhusu uamuzi wa Mahakama ya Juu, maafisa kadhaa wa manispaa huko Marekani walitambua kwamba sheria fulani katika maeneo yao hazistahili tena kutumiwa kuzuia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova. Kufikia sasa, vizuizi vya kuhubiri nyumba hadi nyumba vimeondolewa katika maeneo 90 hivi ya Marekani.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

“MASHAHIDI WA YEHOVA WASHINDA TENA”

Charles C. Haynes, msomi mkuu na mkurugenzi wa miradi ya elimu kwenye Kituo cha Marekebisho ya Kwanza, aliandika maneno hayo kwenye kituo cha Internet cha Freedom Forum chini ya kichwa “Uhuru wa Imani.” Haynes aliendelea kusema: “Juma lililopita [Mashahidi] walishinda kesi ya 48 katika Mahakama ya Juu. Kesi hizo zimeongeza umaana wa haki za Marekebisho ya Kwanza kwa Wamarekani wote.” Alionya hivi: “Kumbukeni jambo hili: Ikiwa serikali inaweza kuzuia uhuru wa dini moja, inaweza kuzuia uhuru wa dini yoyote ile—au dini zote. . . . Bila shaka, watu wana haki ya kutosikiliza—na kufunga mlango. Lakini serikali haipaswi kuwa na mamlaka ya kuamua ni nani anayeruhusiwa kubisha mlango. Kwa hiyo natoa hongera kwa Mahakama ya Juu.”

Haynes amalizia hivi: “Sote tunapaswa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova. Haidhuru ni mara ngapi wanatukanwa, wanafukuzwa mjini, au kupigwa, wao huendelea kupigania uhuru wao wa dini (na wetu pia). Na wanaposhinda, sote tunashinda.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10, 11]

TAARIFA ZA MAGAZETI KUHUSU UAMUZI WA MAHAKAMA YA JUU

“Mahakama Yaunga Mkono Mashahidi wa Yehova; Kibali Hakihitajiki Katika Huduma ya Nyumba Hadi Nyumba

Mashahidi wa Yehova wameamini sikuzote kwamba Mungu anawaunga mkono katika kazi yao ya kutembelea watu nyumbani. Sasa Mahakama ya Juu imewaunga mkono pia.” —Chicago Sun-Times, Juni 18, 2002.

“Uhuru wa Kusema Washinda

Mashahidi wa Yehova watakapokuja mlangoni pako, unaweza kuwashukuru. Kwa sababu ya kujitoa kwa ujasiri kwa kanuni za dini yao, huenda dini hiyo isiyo ya kawaida ambayo ina washiriki milioni 1 hivi [huku Marekani] imefanya mengi kuliko kikundi kingine chochote kuwawezesha Wamarekani mmoja-mmoja wawe na uhuru wa kusema. . . .

“Mashahidi wamezoea kwenda kwenye mahakama ya juu. Kwa zaidi ya miaka 65, wamefaulu kupambana na uonevu wa walio wengi kupitia kesi zaidi ya 24.” —USA TODAY, Juni 18, 2002.

“Kwenda Nyumba Hadi Nyumba Kwatangazwa Kuwa Haki ya Kikatiba. Uamuzi Huo Ni Ushindi kwa Mashahidi wa Yehova

Mnamo Jumatatu Mahakama ya Juu ya Marekani iliamua kwamba wanasiasa, makundi ya kidini, Maskauti wa Kike na wengine wana haki ya kikatiba ya kwenda nyumba hadi nyumba kuendeleza harakati zao bila kuhitaji kwanza kupata kibali kutoka kwa maafisa wa mtaa.”—San Francisco Chronicle, Juni 18, 2002.

“Mahakama ya Juu Yasema: Mashahidi wa Yehova na Maskauti wa Kike Hawawezi Kuzuiwa Kubisha Milango

WASHINGTON—Leo Mahakama ya Juu iliamua kwamba Katiba inalinda haki ya mishonari, wanasiasa na wengine kuwatembelea watu bila kuhitaji kwanza kupata kibali kutoka kwa mamlaka ya mtaa. . . .

“Kupitia kura 8 kwa 1, mahakama ilisema kwamba haki ya uhuru wa kusema iliyo katika Marekebisho ya Kwanza inatia ndani haki ya kuwapelekea watu ujumbe mlangoni pao.”—Star Tribune, Minneapolis, Juni 18, 2002.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Jaji Stevens

[Hisani]

Stevens: Collection, The Supreme Court Historical Society/Joseph Bailey