Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niliwekwa Huru Kutokana na Minyororo ya Chuki

Niliwekwa Huru Kutokana na Minyororo ya Chuki

Niliwekwa Huru Kutokana na Minyororo ya Chuki

SIMULIZI LA JOSÉ GÓMEZ

NILIZALIWA mnamo Septemba 8, 1964, katika mji mdogo wa Rognac, kusini mwa Ufaransa. Wazazi wangu, babu na nyanya yangu walitoka katika jamii ya Wahamaji ya Andalusia, kutoka Algeria na Morocco, Afrika Kaskazini. Jamii yetu ya Wahamaji ina zoea la kuishi katika jamaa kubwa.

Baba yangu alikuwa mjeuri, na baadhi ya mambo ya zamani sana ninayokumbuka ni wakati alipokuwa akimpiga mama yangu. Baada ya muda, Mama aliamua kumtaliki, jambo lisilo la kawaida katika jamii hiyo ya Wahamaji. Mama alinichukua mimi, ndugu yangu na dada yangu na kutupeleka Ubelgiji, ambapo tuliishi kwa amani kwa miaka minane.

Hata hivyo, mambo yalibadilika. Sisi watoto tulitaka kumwona Baba, kwa hiyo Mama alitupeleka Ufaransa ambapo tuliungana naye tena. Kuishi tena na Baba kuliniletea magumu. Tulipokuwa Ubelgiji tulienda mahali popote na Mama. Lakini kulingana na desturi ya ukoo wa baba yangu, wanaume walipaswa kushirikiana na wanaume tu. Walikuwa na maoni ya kwamba wanaume wana haki zote na wanawake wanapaswa kufanya kazi zote. Kwa mfano, siku moja nilipotaka kumsaidia shangazi yangu kusafisha vyombo baada ya chakula cha mchana, mjomba wangu alidai nilikuwa mwanamume afanyaye ngono na wanaume. Katika familia yake, kusafisha vyombo ni kazi ya wanawake pekee. Hatimaye, maoni hayo yasiyofaa yaliniathiri.

Muda si muda, mama yangu akaanza tena kutendewa jeuri na baba yangu. Mara kadhaa tulipojaribu kumtetea mama, ilibidi mimi na ndugu yangu tutoroke kupitia dirishani ili kuepuka kupigwa ngumi na Baba. Dada yangu alipigwa pia. Kwa hiyo, nilikaa mbali na nyumbani muda mrefu kadiri nilivyoweza. Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 15, sikuwa na mwelekeo wowote maishani.

Hatimaye, nilijulikana kwa sababu ya kuwa na hasira kali yenye jeuri. Nilifurahia kuwachokoza watu. Nyakati nyingine niliwachokoza vijana wenzangu, lakini ni wachache waliothubutu kupigana nami, kwa kuwa mara nyingi nilibeba kisu au mnyororo. Punde nilianza kuiba magari na kuyauza. Nyakati nyingine ningechoma magari na kufurahi kuwaona wazima-moto wakiuzima. Baadaye nilianza kuvunja maduka na maghala ya bidhaa. Nilikamatwa mara kadhaa. Na kila mara nilimwomba Mungu anisaidie!

Naam, niliamini Mungu yuko. Tulipokuwa Ubelgiji nilikuwa nimehudhuria shule ya Kikatoliki. Kwa hiyo nilifahamu kwamba nilikuwa nikifanya makosa. Hata hivyo, imani yangu katika Mungu haikunisukuma nibadili mwenendo wangu. Nilifikiri nilipaswa kuomba tu, na ningesamehewa makosa yangu.

Mnamo mwaka wa 1984, nilihukumiwa kifungo cha miezi 11 gerezani kwa sababu ya kuiba. Nilipelekwa katika Gereza la Baumettes, huko Marseilles. Huko, nilitia alama katika sehemu mbalimbali za mwili wangu. Alama moja ilisema “chuki na kisasi.” Badala ya kubadili mwenendo wangu, niliruhusu gereza liongeze chuki yangu kuelekea mamlaka na jamii kwa ujumla. Nilipoachiliwa, baada ya kutumikia kifungo cha miezi mitatu gerezani, nilikuwa na chuki nyingi zaidi. Halafu, msiba fulani ulibadili maisha yangu.

Niliazimia Kulipiza Kisasi

Mgogoro ulitokea kati ya jamaa yetu na jamaa nyingine ya Wahamaji. Ili kusuluhisha tatizo hilo, mimi na wajomba wangu tuliamua kupigana na jamaa hiyo. Sote tulijihami kwa silaha. Bishano lilipotokea, mjomba wangu Pierre na binamu ya baba yangu walipigwa risasi na kuuawa. Nilipandwa na hasira, nikasimama barabarani nikipiga mayowe kwa hasira kali huku nimeshika bunduki mkononi. Hatimaye, mjomba wangu mmoja alininyang’anya bunduki niliyokuwa nayo.

Kifo cha Mjomba Pierre, ambaye nilimwona kama baba yangu, kiliniletea majonzi mengi. Niliomboleza kulingana na desturi za jamii ya Wahamaji. Kwa siku nyingi sikunyolewa wala kula nyama. Nilikataa kutazama televisheni au kusikiliza muziki. Niliapa kulipiza kifo cha mjomba wangu, lakini watu wa ukoo walinizuia kupata bunduki.

Mnamo Agosti 1984, nilijiunga na jeshi. Nilipokuwa na umri wa miaka 20, nilijiandikisha katika kikosi cha kudumisha amani cha Umoja wa Mataifa huko Lebanoni. Nilikuwa tayari kuua au kuuawa. Pia nilivuta bangi sana. Zaidi ya kunifanya nihisi vizuri, bangi ilinifanya nione hakuna kitu ambacho kingeweza kunidhuru.

Kwa kuwa ilikuwa rahisi kupata silaha huko Lebanoni, niliamua kupeleka silaha Ufaransa ili nitimize mpango wangu wa kulipiza kisasi kifo cha mjomba wangu. Nilinunua bastola mbili na risasi kutoka kwa wakazi wa huko. Nilitenganisha sehemu mbalimbali za bastola hizo, nikazificha ndani ya redio mbili, na kuzituma nyumbani.

Yaliposalia majuma mawili tu kabla ya utumishi wetu wa kijeshi kumalizika, niliondoka kambini bila ruhusa pamoja na wenzangu watatu. Tuliporudi kambini, tulitiwa gerezani. Nilipokuwa gerezani, nilipandwa na hasira nikamshambulia mlinzi mmoja. Singeweza kustahimili dharau kutoka kwa mtu asiye wa jamii ya Wahamaji. Siku iliyofuata, nilipigana tena, mara hiyo na afisa wa kijeshi. Kwa muda uliobaki wa utumishi wangu wa kijeshi, nilipelekwa katika Gereza la Montluc, huko Lyons.

Napata Uhuru Gerezani

Siku yangu ya kwanza katika Gereza la Montluc, kijana mmoja mwenye kuvutia alinisalimia kwa uchangamfu. Nilifahamu baadaye kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova na kwamba alitiwa gerezani pamoja na washiriki wenzake kwa sababu walikataa kupigana. Jambo hilo lilinitatanisha. Nilitaka kujua zaidi.

Nilipata kujua kwamba Mashahidi wa Yehova wanampenda Mungu kikweli, na nilivutiwa na maadili yao bora. Bado, nilikuwa na maswali mengi. Hasa, nilitaka kujua kama wafu wanaweza kuwasiliana na watu walio hai kupitia ndoto, jambo ambalo watu wengi wa jamii ya Wahamaji wanaamini. Shahidi mmoja kwa jina Jean-Paul alijitolea kunifundisha Biblia, akitumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. *

Nilimaliza kusoma kitabu hicho kwa usiku mmoja, na moyo wangu uliguswa na mambo niliyosoma. Nikiwa gerezani bado, nilipata uhuru wa kweli! Hatimaye nilipoachiliwa, nilisafiri nyumbani kwa gari-moshi, huku nikibeba mfuko uliojaa vichapo vya Biblia.

Nilienda kuwatafuta Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme katika mji wa Martigues. Niliendelea kujifunza Biblia kwa msaada wa kijana kwa jina Eric, aliyekuwa katika utumishi wa wakati wote. Baada ya siku chache, niliacha kuvuta sigara, na pia nikaachana na marafiki zangu wahalifu. Niliazimia kutenda kupatana na andiko la Mithali 27:11 linalosema: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu, ili nipate kumjibu anilaumuye.” Nilimpata Baba mwenye upendo, Yehova, ambaye nilitaka kumpendeza.

Ugumu wa Kubadilika

Haikuwa rahisi kwangu kufuata kanuni za Kikristo. Kwa mfano, nilianza tena kutumia dawa za kulevya kwa majuma kadhaa. Lakini, tatizo kubwa zaidi lilikuwa kushinda tamaa ya kulipiza kisasi. Ingawa Eric hakujua, nilibeba bunduki nyakati zote na bado nilikuwa nikipanga kulipiza kifo cha mjomba wangu. Niliwatafuta watu hao usiku kucha.

Nilipomwambia Eric jambo hilo, alinieleza kwamba singeweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu ikiwa ningeendelea kubeba silaha na kutafuta kulipiza kisasi. Nilihitaji kufanya uamuzi. Nilitafakari kwa uzito shauri la mtume Paulo katika Waroma 12:19: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi.” Jambo hilo, pamoja na sala, lilinisaidia kudhibiti hisia zangu. (Zaburi 55:22) Hatimaye, nilitupilia mbali silaha zangu. Mnamo Desemba 26, 1986, baada ya kujifunza Biblia kwa mwaka mmoja, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa katika maji.

Jamaa Yangu Yaitikia Vizuri

Mabadiliko niliyofanya katika mwenendo wangu yaliwatia moyo wazazi wangu wajifunze Biblia. Walioana tena, na mama yangu akabatizwa mnamo Julai 1989. Hatimaye, baadhi ya washiriki wengine wa jamaa yetu walikubali ujumbe wa Biblia na wakawa Mashahidi wa Yehova.

Mnamo Agosti 1988, niliamua kuwa mhudumu wa wakati wote. Halafu, nilimpenda dada mmoja katika kutaniko letu kwa jina Katia. Tulifunga ndoa katika Juni 10, 1989. Haikuwa rahisi katika mwaka wa kwanza wa ndoa yetu, kwa sababu bado nilihitaji kubadili maoni fulani niliyokuwa nayo kuelekea wanawake. Ilikuwa vigumu kwangu kutumia maneno ya 1 Petro 3:7, ambapo waume wanatiwa moyo kuwaheshimu wake zao. Nilihitaji kusali mara nyingi ili nipate nguvu ya kushinda kiburi changu na kubadili kufikiri kwangu. Mambo yaliboreka hatua kwa hatua.

Bado ninasononeshwa na kifo cha mjomba wangu, na nyakati nyingine mimi hushindwa kujizuia nisilie ninapomfikiria. Mimi hung’ang’ana na hisia zenye uchungu ninapokumbuka jinsi alivyouawa. Kwa miaka mingi, hata baada ya kubatizwa, niliogopa kukutana ghafula na washiriki wa jamaa tuliyokuwa na kisasi nayo. Ingekuwaje kama wangenishambulia? Ningetendaje? Je, ningetawaliwa na utu wangu wa zamani?

Siku moja nilitoa hotuba ya watu wote katika kutaniko jirani. Huko nilimwona Pepa, ambaye anatoka kwenye jamaa ya watu waliomuua mjomba wangu. Kwa hakika, utu wangu wa Kikristo ulijaribiwa sana. Lakini sikufuata hisia zangu. Baadaye, Pepa alipobatizwa, nilimkumbatia na kumpongeza kwa kufanya uamuzi wa kumtumikia Yehova. Licha ya mambo yote yaliyotendeka, nilimkubali kama dada yangu wa kiroho.

Mimi humshukuru Yehova kila siku kwa kuniweka huru kutokana na minyororo ya chuki. Ningekuwa wapi leo iwapo Yehova hangenionyesha rehema? Kwa sababu yake, ninaweza kufurahia maisha ya familia yenye furaha. Pia nina tumaini la wakati ujao, la ulimwengu mpya usio na chuki wala jeuri. Ndiyo, nina kila sababu ya kutumaini ahadi hii ya Mungu: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”—Mika 4:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Nikiwa katika vikosi vya amani vya Umoja wa Mataifa huko Lebanon, mwaka wa 1985

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na Katia na wana wangu wawili, Timeo na Pierre