Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kuiba Mtihani?

Kuna Ubaya Gani Kuiba Mtihani?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Ubaya Gani Kuiba Mtihani?

“Kila mtu anajua kwamba ni vibaya kuiba mtihani, lakini ni rahisi kufanya hivyo.”—Jimmy, mwenye umri wa miaka 17.

JE, UMEWAHI kushawishiwa kuitupia jicho karatasi ya mwanafunzi mwenzako mnapofanya mtihani? Vijana wengine pia hushawishiwa kufanya hivyo. Jenna, ambaye yuko katika kidato cha nne, anaeleza jinsi ambavyo wanafunzi wengi katika darasa lake huiba mitihani bila wasiwasi: “Wao hujisifu wanapofanya hivyo,” yeye asema. “Usipoiba mtihani wanakuona kuwa mtu wa kiajabu!”

Katika uchunguzi mmoja uliofanywa Marekani, asilimia 80 ya vijana wanaopata maksi za juu katika madarasa yao walikubali kwamba wao huiba mitihani, na asilimia 95 kati yao hawakugunduliwa kamwe. Baada ya kuwahoji wanafunzi zaidi ya 20,000 wa shule za sekondari, Taasisi ya Maadili ya Josephson ilikata kauli hii: “Unyofu na uaminifu unapungua zaidi na zaidi.” Walimu wanashangazwa na jinsi ambavyo tatizo la kuiba mtihani limeenea sana! Hata Gary J. Niels, ambaye ni msimamizi wa shule, alisema: “Ni vijana wachache sana ambao hawaibi mtihani.”

Wazazi wengi wanataka watoto wao wafanye kazi za shule kwa njia inayofaa. Hata hivyo, vijana wengi hukosa uaminifu wanapoiba mtihani. Ni njia zipi mpya wanazotumia? Kwa nini vijana wengine huiba mtihani? Kwa nini unapaswa kuepuka zoea hilo?

Kutumia Tekinolojia Kuiba Mtihani

Siku hizi, watu hutumia mbinu nyingi za udanganyifu kuiba mitihani. Ama kwa hakika, zile mbinu za udanganyifu kama vile kuiba kazi ya mwanafunzi mwenzako au kutumia karatasi zenye majibu si kitu zinapolinganishwa na mbinu za kisasa za kitekinolojia. Mbinu hizo zinatia ndani kutumia bipa zinazopokea majibu ya maswali ya mtihani kutoka kwa watu walio mbali; mashine za kupiga hesabu zilizoingizwa habari kuhusu mtihani; kamera ndogo zinazofichwa katika nguo ambazo zinatumiwa kutuma maswali kwa watu walio mbali ili watoe majibu; vifaa vinavyopeleka ujumbe kwa wanafunzi wengine darasani kwa kutumia mnururisho; na hata vituo vya Internet vyenye karatasi za mitihani za karibu masomo yote!

Walimu wanajaribu kukomesha zoea hilo baya la kuiba mtihani, lakini wana kibarua kigumu. Kwani, si wanafunzi wote—au walimu wote—wanaoelewa maana ya kuiba mtihani. Kwa mfano, wanafunzi wanapofanya mradi fulani wakiwa kikundi, si rahisi kubainisha iwapo wameshirikiana kwa uaminifu au wameibiana. Isitoshe, wanafunzi wengine katika kikundi hicho wanaweza kuwaachia wengine kazi yote. Yuji, ambaye ni mwanafunzi katika chuo kimoja cha mafunzo, anasema: “Wanafunzi wengine ni wavivu sana—hawafanyi kazi yoyote!” Anaongeza hivi: “Kisha wote wanapata maksi zilezile. Nafikiri kufanya hivyo ni kuiba mtihani pia!”

Kwa Nini Wao Huiba Mtihani?

Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba sababu kuu inayowafanya wanafunzi wengi waibe mtihani ni kukosa kujitayarisha. Wanafunzi wengine huona kwamba inawabidi waibe mtihani kwa sababu ya mashindano makali shuleni baina ya wanafunzi au kwa sababu ya matarajio makubwa ya wazazi wao. Sam, mwenye umri wa miaka 13, anasema hivi: “Wazazi wangu wanahangaikia maksi tu. Wao huniuliza: ‘Ulipata maksi ngapi katika hesabu? Ulipata maksi ngapi katika mtihani wa Kiingereza?’ Mimi huchukia maswali hayo!”

Wengine huiba mtihani kwa sababu ya kushinikizwa sana wapate maksi za juu. Kitabu kinachoitwa The Private Life of the American Teenager kinasema: “Mfumo ambao unawashinikiza watu kufanikiwa badala ya kupata uradhi kutokana na kujifunza una kasoro. Nyakati nyingine wao hutafuta mafanikio kwa udanganyifu.” Wanafunzi wengi wanakubali kauli hiyo. Kwani, hakuna mtu yeyote anayetaka kuanguka mtihani wowote ule, sembuse mtihani wa mwisho. “Watu fulani huwa na wasiwasi mwingi kwamba wataanguka,” asema Jimmy, mwanafunzi wa shule ya sekondari. “Hata ikiwa wanajua majibu, wataiba mtihani ili wawe na uhakika kwamba majibu yao yako sawa.”

Kwa kuwa watu wengi wako tayari kutumia udanganyifu, kuiba mtihani kwaweza kuonekana kuwa jambo linalofaa. Na nyakati nyingine kwaweza kuonekana kuwa jambo lenye faida. Greg, mwenye umri wa miaka 17, anasema: “Jana nilimwona kijana mmoja akiiba mtihani darasani. Tuliporudishiwa karatasi za mtihani leo, alipata maksi nyingi kunishinda.” Wengi wanaathiriwa na vijana wenzao ambao wanaiba mtihani. Yuji anasema: “Wanafunzi fulani husema kwamba ‘ikiwa wengine wanaiba mtihani, basi ni lazima nifanye hivyo pia.’” Lakini je, ni lazima?

Zoea la Kujidanganya

Hebu linganisha zoea la kuiba mtihani na wizi. Je, kuiba ni kuzuri eti kwa sababu watu wengi wanaiba? Huenda ukajibu la—hasa ikiwa pesa zako ndizo zinazoibwa! Mtu anapoiba mtihani anapata sifa asiyostahili—labda hata anaathiri matokeo ya wale ambao ni waaminifu. (Waefeso 4:28) Tommy, ambaye alimaliza shule ya sekondari hivi karibuni, anasema: “Haifai kufanya hivyo.” Kisha anaongeza: “Mtu anapoiba mtihani ni kana kwamba anasema anafahamu somo lile, na kumbe halijui. Kwa hiyo anasema uwongo.” Maoni ya Biblia kuhusu jambo hilo yanaonyeshwa wazi katika Wakolosai 3:9: “Msiwe mkiambiana uwongo.”

Kuiba mtihani kwaweza kuwa zoea lisiloweza kukomeshwa kwa urahisi. Jenna anasema: “Wale wanaoiba mtihani huona kwamba hawahitaji kusoma ili wapite, kwa hiyo wanategemea sana kuiba mtihani. Halafu wanapojitegemea, hawawezi kufanikiwa maishani.”

Kanuni iliyoandikwa kwenye Wagalatia 6:7 inaamsha fikira: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” Matokeo ya kuiba mtihani shuleni yanatia ndani kusumbuliwa na dhamiri, kutoaminiwa na marafiki wako, na kudumaza akili kwa sababu ya kutosoma. Kama vile kansa inavyoweza kuenea na kufisha, kuzoea udanganyifu kunaweza kuenea katika shughuli nyingine maishani na kuharibu mahusiano yaliyo muhimu kwako. Ama kwa hakika, zoea hilo litaathiri uhusiano wako na Mungu, ambaye anachukia udanganyifu.—Mithali 11:1.

Wale wanaotegemea udanganyifu wanajidanganya. (Mithali 12:19) Matendo yao yanawafanya kuwa sawa na wale viongozi wafisadi katika jiji la kale la Yerusalemu ambao walisema hivi: “Tumefanya maneno ya uongo kuwa kimbilio letu, tumejificha chini ya maneno yasiyo kweli.” (Isaya 28:15) Hata hivyo, mdanganyifu hawezi kumficha Mungu matendo yake.—Waebrania 4:13.

Usiibe Mtihani!

Mara nyingi vijana hutumia jitihada nyingi na akili nyingi kuiba mtihani—jitihada ambazo wangetumia vizuri kupata elimu bora bila udanganyifu. Abby, mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Ikiwa wangejitahidi sana kujifunza kama vile wanavyojitahidi kuiba mtihani, wangepata maksi za juu sana.”

Ama kweli, unaweza kushawishiwa sana uibe mtihani. Lakini unapaswa kuepuka mtego huo wa kimaadili! (Mithali 2:10-15) Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwanza, kumbuka kwa nini unaenda shule. Unaenda shule kujifunza. Ni kweli kwamba huenda usione faida za kujifunza mambo mengi kwa kuwa huenda usiyatumie kamwe maishani. Lakini mtu anapoepuka kujifunza kwa kuiba mtihani, anazuia ukuzi wa uwezo wake wa kujifunza mambo mapya na kutumia ujuzi maishani. Ni lazima mtu ajitahidi sana ili apate ufahamu wa kweli. Biblia inasema: “Inunue kweli, wala usiiuze; naam, hekima, na mafundisho, na ufahamu.” (Mithali 23:23) Naam, unapaswa kusoma kwa bidii na kujitayarisha kwa ajili ya mitihani. Jimmy anasema: “Unahitaji kusoma kwa bidii kabla ya mtihani.” Kisha anaongeza: “Ukifanya hivyo utakuwa na uhakika kwamba unayajua majibu.”

Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda usijue majibu yote, na huenda ukapata maksi za chini. Hata hivyo, usipovunja kanuni zako, huenda ukatambua mambo unayohitaji kutenda ili kufanya maendeleo.—Mithali 21:5.

Yuji, ambaye alinukuliwa hapo awali, ni Shahidi wa Yehova. Anaeleza kile anachofanya wakati wanafunzi wenzake darasani wanapomshinikiza awasaidie kuiba mtihani: “Kwanza, mimi huwaambia kwamba mimi ni Shahidi.” Kisha anaongeza: “Hilo limenisaidia sana kwani wanajua kwamba Mashahidi wa Yehova ni wanyofu. Mtu anapoomba nimwambie jibu wakati wa mtihani, mimi hukataa. Halafu baadaye ninamweleza sababu ya kukataa.”

Yuji anakubali taarifa hii ambayo mtume Paulo aliwaandikia Waebrania: “Twataka kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Ukifuata viwango vya juu vya unyofu na kuepuka kuiba mtihani, maksi zako za juu zitakuwa za kweli. Ukifanya hivyo, utawapa wazazi wako zawadi ya pekee sana, yaani, utawaonyesha kwamba wewe ni Mkristo mwaminifu. (3 Yohana 4) Isitoshe, utakuwa na dhamiri safi na utapata shangwe kwa sababu ya kuufurahisha moyo wa Yehova Mungu.—Mithali 27:11.

Basi, hata watu wengi kadiri gani wakiiba mtihani, epuka zoea hilo! Ukifanya hivyo, utadumisha uhusiano mwema pamoja na wengine na, zaidi ya yote, pamoja na Mungu wa kweli, Yehova.—Zaburi 11:7; 31:5.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Mara nyingi mtu anayeiba mtihani hatambui kwamba yeye ni mwizi

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Mara nyingi, kuiba mtihani humwongoza mtu kwenye matendo mengine makubwa ya udanganyifu

[Blabu katika ukurasa wa 15]

Mtu anayeiba mtihani hawezi kumficha Mungu matendo yake

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ukijifunza vya kutosha kabla ya mtihani utakuwa na uhakika