Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Yanayofaa Kuhusu Faragha

Maoni Yanayofaa Kuhusu Faragha

Maoni Yanayofaa Kuhusu Faragha

“MACHO YA BWANA YAKO KILA MAHALI; YAKIMCHUNGUZA MBAYA NA MWEMA.”—MITHALI 15:3.

WATU wengi hawapendi mtu achunguze matendo yao, mawazo yao na yale yaliyo moyoni mwao. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Mungu anaweza kufanya hivyo. Biblia inasema hivi kwenye Waebrania 4:13: “Hakuna kiumbe kisichokuwa dhahiri machoni pake, bali vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.” Je, Mungu anaingilia faragha ya watu kwa kufanya hivyo? La hasha. Kwa nini?

Kwa mfano: Unapoogelea ufuoni, huenda mwokoaji akakutupia jicho daima. Lakini hufikiri kwamba anaingilia faragha yako. Kwa kweli, unahisi ukiwa salama akiwapo. Unajua kwamba ukiwa taabani, atakuja haraka kukusaidia. Vivyo hivyo, mama humwangalia mtoto wake kila wakati. Asipofanya hivyo, watu watamwona kuwa mama asiyejali.

Yehova Mungu vilevile huchunguza mawazo na matendo yetu kwa sababu anatujali sana. Nabii mmoja wa Biblia alisema hivi: “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Lakini, Yehova anajua mawazo na matendo yetu kwa kadiri gani? Tunaweza kufahamu jambo hilo kwa kuchunguza visa fulani vinavyohusu Yesu, Mwana wa Mungu.

Uwezo wa Kusoma Mioyo na Akili

Yesu alipokuwa akila chakula kwenye nyumba ya Farisayo mmoja, mwanamke aliyejulikana kuwa mtenda-dhambi alikuja na kupiga magoti miguuni pa Yesu. Alianza kulia na kutumia nywele zake kupangusa machozi yaliyoanguka kwenye miguu ya Yesu. Simulizi hilo lasema hivi: “Kwa kuona hayo yule Farisayo aliyemwalika akajisemea ndani yake mwenyewe: ‘Mtu huyu, kama angekuwa ni nabii, angejua ni nani na ni wa aina gani mwanamke anayemgusa.’” Jibu la Yesu linaonyesha kwamba alijua hali za mwanamke huyo na pia alijua yale ambayo Farisayo huyo alikuwa amesema “ndani yake mwenyewe.”—Luka 7:36-50.

Pindi nyingine Yesu alikutana na watu waliopinga miujiza yake. Andiko la Mathayo 9:4 linasema hivi: “Yesu, akijua fikira zao, akasema: ‘Kwa nini mnafikiri mambo maovu katika mioyo yenu?’” Yesu hakukisia-kisia tu au kutumia akili kujua mawazo ya wengine.

Tukichunguza simulizi la ufufuo wa Lazaro tutaona kwamba kuna mengi zaidi yaliyohusika. Lazaro, rafiki mkubwa wa Yesu alikuwa mfu kwa muda wa siku nne. Mawazo yake yalikuwa yamepotea, na alikuwa ameanza kuoza. (Zaburi 146:3, 4) Yesu alipoagiza jiwe lililofunika kaburi liondolewe, Martha, dadake Lazaro alisema hivi: “Bwana, kufikia sasa lazima awe anuka.” Hata hivyo, kwa nguvu za Mungu, Yesu alimfufua Lazaro akiwa na kumbukumbu na mawazo yale aliyokuwa nayo kabla hajafa.—Yohana 11:38-44; 12:1, 2.

Uwezo wa Yehova Mungu wa kujua mawazo yetu ya ndani unathibitishwa na maelezo ya Yesu kuhusu sala. Kabla ya kuwafundisha wanafunzi wake ile sala ya mfano, Yesu alisema hivi: “Mungu Baba yenu ajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla nyinyi hamjamwomba.” Yesu alisema hivi pia: “Usalipo ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye katika siri; ndipo Baba yako atazamaye katika siri atakurudishia wewe.”—Mathayo 6:6, 8.

Faida za Kujua Kwamba Mungu Anatuona

Je, kujua kwamba Mungu anachunguza mioyo yote na anatambua “mawazo yote ya fikira” kunatuzuia au kutunyima uhuru wetu? (1 Mambo ya Nyakati 28:9) La, kujua kwamba hatuwezi kumficha Mungu jambo lolote kunaweza kutusaidia sana kufanya yaliyo mema.

Elizabeth, aliyetajwa katika makala ya kwanza, anasema kwamba yeye hawi mnyofu kwa sababu anachunguzwa kwa kamera kazini. Badala yake, anasema: “Kujua kwamba Yehova anaona mwenendo wangu hunichochea kuwa mnyofu kila wakati, hata nisipokuwa kazini.”

Jim pia ana maoni kama hayo. Yeye hufanya kazi katika kiwanda ambamo wafanyakazi huiba sana. Hata hivyo, Jim hawezi kumwibia mwajiri wake. Anasema hivi: “Ni kweli kwamba ninaweza kuiba mali ya kampuni bila kukamatwa, lakini uhusiano wangu na Mungu ni muhimu sana na ninajua kwamba anaona kila jambo ninalofanya.”

Kujua kwamba Mungu anaona matendo yetu yote, pamoja na kutaka sana kuwa na uhusiano mzuri naye, kunaweza kumchochea mtu afanye mabadiliko makubwa maishani mwake. Kwa mfano, Doug alilelewa katika familia ya Kikristo lakini alipuuza wazo la kwamba Mungu anaweza kuona matendo yake yote. Hivyo aliishi maisha maradufu. Alihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na familia yao lakini baadaye akiwa pamoja na rafiki zake alitumia dawa za kulevya. Alipenda sana kuendesha pikipiki hata akajiunga na genge la waendesha pikipiki wenye jeuri. Doug alifanya uhalifu mbaya sana ili apendwe na rafikize.

Baada ya miaka kadhaa, Doug alianza tena kujifunza Biblia. Alianza kumwona Yehova kuwa mtu halisi awezaye kuona matendo ya watu, na matendo hayo yanaweza kumfurahisha au kumhuzunisha. Doug alichochewa kuanza kuishi kupatana na viwango vya juu vya maadili vya Mungu. Ijapokuwa genge hilo lilimpiga vibaya mtu yeyote aliyejitenga nalo, Doug alihudhuria mkutano wa genge hilo na kutangaza mbele ya washiriki wake wote kwamba amejitenga. Anakumbuka: “Niliposimama ili kuongea nao, moyo wangu ulikuwa ukidunda-dunda. Nilihisi kama Danieli alipokuwa katika pango la simba. Lakini nilisali kimoyomoyo kwa Yehova kisha nikaeleza kwa utulivu sababu zangu za kujitenga nao. Nilipomaliza, wote walinisalimu na kunitakia heri isipokuwa mmoja wao tu. Niliona andiko la Isaya 41:13 likitimia kuhusiana nami: ‘Mimi, BWANA, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia.’” Doug anahisi kwamba Yehova alimpa nguvu alizohitaji ili kubadili maisha yake.

Maoni Yanayofaa

Ni upumbavu kufikiri kwamba tunaweza kumficha Mungu mambo fulani. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mpumbavu amesema moyoni, hakuna Mungu.” (Zaburi 14:1) Kama makala zilizotangulia zilivyoonyesha, wanadamu wamebuni kamera zinazoweza kumtambua mtu fulani hususa katikati ya umati. Wamebuni vifaa vya kunasa mazungumzo ambavyo vinaweza kutambua sauti ya mtu fulani kati ya maelfu ya sauti za watu wanaopiga simu. Basi, hapana shaka yoyote kwamba Muumba wa ubongo wa mwanadamu anaweza kuchunguza fikira za mtu yeyote, wakati wowote Anapotaka kufanya hivyo.

Ingawa Muumba wetu ana haki ya kujua mambo tunayofanya faraghani, wanadamu hawana haki ya kufanya hivyo. Mtume Petro anawahimiza hivi watu wote wanaotaka kumpendeza Mungu: “Acheni mmoja wenu asiteseke akiwa . . . mtenda-maovu au akiwa mjishughulishaji katika mambo ya watu wengine.” (1 Petro 4:15) Mtume Paulo pia anatuonya tusijiingize “katika mambo ya watu wengine.”—1 Timotheo 5:13.

Katika nchi fulani, raia wengi ‘hujishughulisha’ na kujiingiza sana “katika mambo ya watu wengine” kwa kupiga picha na kurekodi mambo ya faraghani kwa kutumia video au kanda ndogo za kunasa sauti. Kwa mfano, nchini Japan, mkimbiaji wa masafa marefu Naoko Takahashi, aliyeshinda medali ya dhahabu katika Mashindano ya Olimpiki huko Sydney, aligundua hivi majuzi kwamba kamera ndogo ilikuwa imefichwa katika bafu lake na ilikuwa ikimpiga picha bila yeye kujua. Video ilitayarishwa, na maelfu ya nakala za video hiyo zimeuzwa kinyume cha sheria.

Zoea la kutumia tekinolojia ya kisasa kuiba vitambulisho au kufanya ulaghai kwa kutumia habari za kibinafsi za watu wengine limeenea pia. Ni jambo la busara kuchukua hatua za kulinda habari zako za kibinafsi ili zisiwafikie watu wasiofaa. * Biblia inasema: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mithali 22:3.

Matendo ya Siri—Hukumu ya Hadharani

Inaelekea kwamba serikali zitazidi kuwachunguza kwa makini zaidi raia wake kadiri uhalifu, jeuri na ugaidi unavyozidi kuongezeka. Hata hivyo, hivi karibuni, kamera na vifaa vya kunasa mazungumzo ya watu faraghani havitahitajiwa tena. Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni, Yehova Mungu atawahukumu wanadamu wote kulingana na matendo waliyofanya hadharani na faraghani.—Ayubu 34:21, 22.

Kuanzia wakati huo na kuendelea, dunia haitakuwa na jeuri, chuki, na uhalifu ambao umewasumbua wanadamu kwa miaka mingi. Itawezekanaje? Mbali na kwamba Yehova atawajua vyema watu wote watakaokuwa wakiishi wakati huo, wao pia watamjua Yehova vyema. Maneno ya nabii Isaya yatatimia: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Ona sanduku lenye kichwa “Jihadhari!”

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Kujua kwamba hatuwezi kumficha Mungu jambo lolote kunaweza kutusaidia sana kufanya yaliyo mema

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Jihadhari!

HABARI ZA SIRI NA VITUO VYA INTERNET VYA WANAOTAFUTA KAZI: Watu wanaotafuta kazi kwa kuweka maelezo ya elimu na uzoefu wao wa kazi kwenye Internet hukabili hatari ya habari zao kusambaa kwa wengine. Habari hizo zinaweza kuhifadhiwa kwa miaka mingi kwenye Internet na zinaweza hata kutumiwa na wezi wa vitambulisho. Vituo fulani vya kutangaza kazi huomba habari za kibinafsi za watu wanaotafuta kazi kama vile, jina, anwani, umri, na ujuzi wa kazi na kisha husambaza habari hizo kwa watu wengine kama vile watangazaji wa bidhaa.

HABARI ZA SIRI NA SIMU ZA MKONONI: Hivi sasa hakuna njia ya bei nafuu ya kutunza habari za siri za watu wanaotumia simu za mkononi. Ni salama zaidi kutumia simu ya kawaida ikiwa mnazungumzia jambo la siri. Hakikisha kwamba wewe na mtu unayezungumza naye mnatumia simu za kawaida. Ujumbe kutoka kwa simu nyingi za mkononi unaweza kunaswa na redio, simu nyingine za mkononi, au hata na mashine zinazopima mpigo wa moyo wa watoto wachanga. Ukinunua bidhaa kwa kupiga simu na kutaja nambari yako ya kadi ya mkopo na tarehe yake ya mwisho, habari hizo zinaweza kuibiwa na kutumiwa vibaya na walaghai. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 32 Habari hii imetolewa kwenye kituo cha Internet cha shirika la Privacy Rights Clearinghouse.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Hakuna mtu anayeona kwamba mwokoaji anaingilia faragha yake anapomtupia jicho daima

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kujua kwamba Mungu anaona matendo yetu kulimchochea Doug afanye mabadiliko maishani mwake