Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yajaribiwa Ulaya Wakati wa Wanazi

Imani Yajaribiwa Ulaya Wakati wa Wanazi

Imani Yajaribiwa Ulaya Wakati wa Wanazi

SIMULIZI LA ANTON LETONJA

Mnamo Machi 12, 1938, majeshi ya Hitler yaliingia nchini Austria. Redio zilicheza nyimbo zilizoambatana na matembezi ya wanajeshi na kutangaza siasa. Watu walijawa na hisia za kizalendo nchini kwetu, Austria.

HITLER alipoanza kutawala, watu walikuwa na matumaini makubwa nchini Austria. Wengi walitumaini kuwa “Utawala wa Miaka Elfu Moja” wa Hitler ungemaliza matatizo ya umaskini na ukosefu wa kazi. Msisimuko huo uliwafanya hata makasisi Wakatoliki kumpigia Hitler saluti.

Ingawa nilikuwa kijana mwenye umri wa miaka 19 tu, sikupumbazwa na ahadi za Hitler. Sikuamini kwamba serikali yoyote ya wanadamu ingeweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu.

Kujifunza Kweli za Biblia

Nilizaliwa mnamo Aprili 19, 1919, huko Donawitz, Austria, nikiwa mtoto wa tatu na wa mwisho katika familia yetu. Baba alikuwa mchimbaji wa makaa ya mawe mwenye bidii. Mnamo mwaka wa 1923, alitupeleka hadi Ufaransa, ambako alipata kazi katika mji wenye madini wa Liévin. Kwa sababu alipenda siasa, yeye hakuamini dini, lakini Mama alikuwa Mkatoliki shupavu. Mama alitufundisha sisi watoto kuwa na imani katika Mungu, na alisali pamoja nasi kila usiku. Baada ya muda, Baba alimkataza Mama kwenda kanisani kwa sababu ya kutoamini dini.

Mwishoni mwa miaka ya 1920, tulikutana na kijana Myugoslavia, Vinzenz Platajs, ambaye tulimwita Vinko. Yeye aliwasiliana na Wanafunzi wa Biblia. Wakati huo Mashahidi wa Yehova walijulikana kwa jina hilo. Muda mfupi baadaye, Mwanafunzi mmoja wa Biblia alianza kutembelea familia yetu. Kwa kuwa Baba alimzuia Mama kwenda kanisani, Mama alimuuliza Vinko kama ilifaa kumwabudu Mungu nyumbani. Vinko alimwonyesha andiko la Matendo 17:24, linalosema kwamba Mungu “hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono,” na akamwelezea kwamba nyumbani ni mahali panapofaa kumwabudu Mungu. Alipendezwa na akaanza kuhudhuria mikutano katika nyumba za Wanafunzi wa Biblia.

Baba alimtaka Mama akomeshe “upuuzi huo.” Ili atutenganishe na Wanafunzi wa Biblia, alituagiza tuhudhurie Misa kila Jumapili! Mama alipokataa katakata kuhudhuria, Baba alitaka niwe mtumishi wa kanisa. Ingawa aliheshimu uamuzi wa Baba kuhusu jambo hilo, Mama aliendelea kukazia kanuni za Biblia moyoni na akilini mwangu na kunipeleka kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia.

Katika mwaka wa 1928, Vinko na dada yangu, Josephine—au Pepi, kama tulivyomwita—walionyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Baadaye walioana. Mwaka uliofuata binti yao, Fini, alizaliwa huko Liévin. Miaka mitatu baadaye walikubaliwa kuingia katika utumishi wa wakati wote nchini Yugoslavia, ambako kazi ya Mashahidi ilikuwa imewekewa vikazo. Ingawa walipata magumu mengi, shangwe na bidii yao katika utumishi wa Yehova iliendelea bila kufifia. Mfano wao ulinichochea nitamani kuwa mtumishi wa wakati wote.

Ukuzi wa Kiroho

Kwa kusikitisha, wazazi wetu walitalikiana katika mwaka wa 1932 kwa sababu ya kutoelewana. Tulirudi Austria pamoja na Mama, lakini ndugu yangu mkubwa, Wilhelm (Willi), alibaki Ufaransa. Baada ya hapo, hatukuonana mara nyingi na Baba. Aliendelea kutupinga hadi alipokufa.

Niliishi na mama yangu katika kijiji cha Gamlitz, Austria. Yeye alinifundisha kwa ukawaida akitumia vichapo vya Biblia, kwa kuwa hakuna kutaniko lililokuwa karibu. Mara mbili kila mwezi, Eduard Wohinz aliendesha baiskeli umbali wa karibu kilometa mia moja hadi Graz ili kututembelea na kututia moyo!

Hitler alipoanza kutawala kwa ukatili katika mwaka wa 1938, Ndugu Wohinz alikamatwa. Tulihuzunika kusikia kwamba aliuawa kwa kupuliziwa gesi yenye sumu katika taasisi moja huko Linz. Imani yake yenye nguvu ilituchochea kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

Matukio Mabaya ya Mwaka wa 1938

Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku nchini Austria katika mwaka wa 1935. Majeshi ya Hitler yaliingia Austria katika mwaka wa 1938, na huduma yetu ikawa hatari sana. Majirani walijua kwamba mimi na mama yangu tulikuwa Mashahidi wa Yehova, hivyo tuliamua kutofanya mambo hadharani. Hata nilianza kulala ghalani usiku ili Wanazi wasiweze kunikamata kwa urahisi.

Mapema katika mwaka wa 1938, nilimaliza elimu yangu ya msingi na kuanza kufanya kazi katika kiwanda cha kuoka mikate. Kwa sababu nilikataa kusema “Asifiwe Hitler” au kuwa mwanachama wa kikundi cha Vijana wa Hitler, nilifutwa kazi. Hata hivyo, nilitamani hata zaidi kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa katika maji.

Mimi na mama yangu tulibatizwa katika Aprili 8, 1938. Usiku mmoja, tulikusanyika katika chumba kimoja msituni tukiwa na watu wengine saba. Baada ya hotuba ya ubatizo, tulitembea kupitia kijia chembamba hadi kwenye dimbwi, mmoja baada ya mwingine, kila baada ya dakika kumi. Sote tulibatizwa katika hori lililojengwa kwa mawe.

Katika Aprili 10, 1938, kura bandia ya kuamua Austria ijiunge na Ujerumani ilipigwa. Mwito uliosema “Hitler Juu!” ulibandikwa kila mahali nchini. Mimi na mama yangu hatukuhitajika kupiga kura kwa sababu hatukuwa raia wa taifa lolote, kwa sababu tulikuwa tumeishi Ufaransa kwa muda mrefu. Jambo hilo liliniokoa baadaye. Franz Ganster, kutoka Klagenfurt kusini mwa Austria, alituletea magazeti ya Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida. Kwa hiyo tuliimarishwa kiroho na Neno la Mungu kabla ya Vita ya Pili ya Ulimwengu kupamba moto.

Ndugu Yangu, Willi

Willi, aliyekuwa mkubwa wangu kwa miaka minne, hakuwa amewasiliana nasi kwa zaidi ya miaka tisa tangu tulipotoka Ufaransa. Ingawa Mama alikuwa amemfundisha Biblia tangu ujana, alikuwa amepumbazwa aamini kwamba sera ya kisiasa ya Hitler ingeleta mafanikio wakati ujao. Katika Mei 1940, mahakama moja ya Ufaransa ilimhukumia Willi kifungo cha miaka miwili kwa sababu ya makosa aliyofanya alipokuwa Mnazi. Muda mfupi baadaye, aliachiliwa wakati majeshi ya Ujerumani yalipovamia Ufaransa. Wakati huo, alitutumia kadi akiwa Paris. Tulifurahi kujua kwamba alikuwa hai, lakini tulishangaa kusikia mambo aliyokuwa ameshawishwa kuamini!

Wakati wa vita, Willi alipata nafasi ya kututembelea mara nyingi kwa sababu alikuwa na uhusiano mzuri na kikosi cha SS (Schutzstaffel, walinzi wa Hitler). Alivutiwa sana na mafanikio ya kijeshi ya Hitler. Kila nilipojaribu kumkumbusha kuhusu tumaini letu linalotegemea Biblia alisema: “Huo ni upuuzi! Ona vile Hitler ameshambulia ghafula. Hivi karibuni Wajerumani watatawala ulimwengu mzima!”

Mnamo Februari 1942, alipokuja nyumbani likizoni, nilimpatia kitabu Enemies, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Nilishangazwa sana alipokisoma chote mara hiyo. Alianza kutambua kwamba utawala wa Hitler haungeweza kufanikiwa na alikuwa anaunga mkono mfumo mkatili. Aliazimia kurekebisha makosa yake.

Msimamo wa Willi Katika Kweli ya Biblia

Willi alipotutembelea mwezi uliofuata, alikuwa amebadilika sana. Alisema: “Anton, nilikuwa nimepotea!”

Nilimwambia, “Willi, laiti ungalijua hivyo mapema.”

“La,” akajibu, “sijachelewa sana! Biblia inasema ‘ufanye unalopaswa kufanya maadamu u hai,’ ninamshukuru Mungu kwa sababu ningali hai!”—Mhubiri 9:10.

“Na sasa utafanya nini?” nilimwuliza.

“Sitaendelea kutumika jeshini,” alinijibu. “Nitavunja uhusiano wangu na Wanazi ili nione jinsi itakavyokuwa.”

Mara moja akaenda Zagreb, Yugoslavia, kumtembelea tena dada yangu, Pepi. Baada ya kuhudhuria kwa muda mikutano iliyokuwa imepigwa marufuku ya Mashahidi, alibatizwa kisiri. Hatimaye, mwana mpotevu alirejea!—Luka 15:11-24.

Ili aepuke Wanazi huko Ufaransa, Willi alijaribu kuingia Uswisi. Lakini akakamatwa na polisi wa jeshi la Ujerumani. Alipelekwa mahakamani huko Berlin, na mnamo Julai 27, 1942, alihukumiwa kifo kwa sababu ya kutoroka. Niliruhusiwa kumtembelea katika Gereza la Kijeshi la Berlin-Tegel. Nilielekezwa kwenye chumba kidogo, na baada ya muda mfupi Willi aliingia akiwa amefunganishwa na mlinzi kwa mnyororo. Machozi yalinitoka nilipomwona katika hali hiyo. Hatukuruhusiwa kukumbatiana na tulipewa dakika 20 tu za kuagana.

Willi aliponiona nikitoa machozi aliniuliza: “Anton, kwa nini unalia? Unapaswa kufurahi! Ninamshukuru Yehova sana kwa kunisaidia niipate kweli tena! Iwapo ningekufa nikipigana kwa ajili ya Hitler, singekuwa na tumaini. Lakini nikifa kwa ajili ya Yehova, nina hakika nitafufuliwa na tutaonana tena!”

Katika barua aliyoandika ili kutuaga, Willi alisema: “Mungu wetu mpendwa, ninayemtumikia, hunipa kila kitu ninachohitaji na atanitegemeza hadi mwisho, ili niweze kuvumilia na kushinda. Ninasema tena, mwe na hakika kwamba sijutii jambo lolote na nimedumu nikiwa imara katika Bwana!”

Willi aliuawa katika Gereza la Brandenburg, karibu na Berlin, siku iliyofuata, Septemba 2, 1942. Alikuwa na umri wa miaka 27. Maisha yake yalionyesha ukweli wa maneno ya Wafilipi 4:13: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”

Vinko Ni Mwaminifu Hadi Kifo

Jeshi la Ujerumani lilifika Yugoslavia katika mwaka wa 1941, na kuwalazimu Pepi na mumewe, Vinko, na binti yao mwenye umri wa miaka 12, Fini, kurudi nyumbani Austria. Wakati huo Mashahidi wengi nchini Austria walikuwa gerezani au kwenye kambi za mateso. Kwa kuwa hawakuwa raia wa taifa lolote—hawakuwa raia wa Ujerumani—walipewa kazi ngumu katika shamba moja huko kusini mwa Austria, karibu na nyumbani kwetu.

Baadaye, mnamo Agosti 26, 1943, Vinko alikamatwa na polisi wa Gestapo (polisi wa siri wa Nazi). Fini alipojaribu kumuaga baba yake, mkuu wa polisi alimpiga kwa nguvu nyingi na kumwangusha upande wa pili wa chumba. Vinko alihojiwa mara kwa mara na kupigwa vibaya na polisi wa Gestapo, kisha akapelekwa katika Gereza la Stadelheim huko Munich.

Mnamo Oktoba 6, 1943, nilikamatwa na polisi nikiwa kazini, na kupelekwa katika Gereza la Stadelheim, ambako Vinko alikuwa. Kwa kuwa nilijua Kifaransa vizuri, nilitumiwa kuwatafsiria wafungwa wa kivita wa Ufaransa. Nilipata nafasi ya kuzungumza na Vinko nilipokuwa nikitembea humo gerezani.

Hatimaye Vinko alihukumiwa kifo. Alishtakiwa kwa kuwapelekea Mashahidi vichapo vya Biblia na kuwapatia msaada wa kifedha wanawake Mashahidi ambao waume zao walikuwa katika kambi za mateso. Alihamishwa hadi gereza lilelile ambamo Willi aliuawa karibu na Berlin na kukatwa kichwa katika Oktoba 9, 1944.

Pindi ya mwisho ambayo Vinko alikutana na familia yake ilikuwa yenye kuvunja moyo. Alikuwa amefungwa kwa minyororo na kupigwa vibaya, na ilikuwa vigumu kwake kuwakumbatia kwa sababu ya minyororo. Fini alikuwa mwenye umri wa miaka 14 alipomwona baba yake kwa mara ya mwisho. Bado anakumbuka maneno yake ya mwisho: “Fini, mtunze mama yako!”

Baada ya kifo cha baba yake, Fini alichukuliwa kutoka kwa mama yake na akapelekwa kwa familia ya Wanazi ambayo ilitaka “kumrekebisha.” Mara kwa mara alipigwa vibaya. Majeshi ya Urusi yalipoingia Austria, familia hiyo ya Wajerumani iliyokuwa imemtesa sana ilipigwa risasi. Ilionwa kuwa familia katili sana ya Wanazi.

Dada yangu aliendelea na utumishi wa wakati wote baada ya vita. Alitumika pamoja na mume wake wa pili, Hans Förster, katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Uswisi hadi kifo chake katika mwaka wa 1998. Fini amefuata kielelezo cha wazazi wake na sasa anaendelea kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova, nchini Uswisi.

Kuwa Huru Hatimaye!

Mapema katika mwaka wa 1945, gereza letu huko Munich lilikuwa mojawapo ya majengo yaliyopigwa bomu. Jiji likawa magofu. Nilikuwa nimekaa gerezani kwa miezi 18 wakati wa kusikizwa kwa kesi yangu ulipofika. Ilikuwa majuma mawili tu kabla ya vita kumalizika rasmi katika Mei 8, 1945. Wakati wa kesi, niliulizwa hivi: “Je, utakubali kuingia jeshini?”

Nami nikajibu: “Mfungwa haruhusiwi kuvaa yunifomu wala kusema ‘Asifiwe Hitler.’” Nilipoulizwa kama nilikuwa tayari kutumika katika jeshi la Ujerumani, nilisema: “Tafadhali nipeni karatasi za kujiandikisha, halafu nitawajulisha uamuzi wangu!”

Siku chache baadaye, vita ilimalizika, na nikaambiwa kwamba nilikuwa huru. Muda mfupi baadaye, nilihamia eneo la Graz, ambamo kutaniko dogo la Mashahidi 35 lilianzishwa. Leo kuna makutaniko manane katika eneo la Graz.

Msaidizi Mpendwa

Muda mfupi baada ya vita, nilikutana na Helene Dunst, mwalimu kijana wa shule ambaye awali alikuwa mwanachama wa chama cha Nazi. Alikuwa amekatishwa tamaa kabisa na utawala wa Wanazi. Mara ya kwanza nilipozungumza naye, aliuliza: “Mbona ni nyinyi pekee mnaojua kwamba jina la Mungu ni Yehova na wengine hawajui?”

“Kwa sababu watu wengi hawasomi Biblia,” nikamjibu. Kisha nikamwonyesha jina la Mungu katika Biblia.

Halafu akasema: “Iwapo Biblia inasema kwamba jina la Mungu ni Yehova, basi twapaswa kumwambia kila mtu jambo hilo!” Helene alianza kuhubiri kweli za Biblia na mwaka mmoja baadaye akaonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Tulioana katika Juni 5, 1948.

Katika Aprili 1, 1953, tulianza utumishi wa wakati wote. Baadaye tulialikwa kwenye darasa la 31 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, karibu na South Lansing, New York. Tulifurahia ushirika mchangamfu pamoja na wanafunzi wenzetu kutoka nchi 64.

Baada ya kuhitimu tulitumwa tena nchini Austria. Kwa muda wa miaka michache tulifanya kazi ya kutembelea makutaniko na kuyaimarisha kiroho. Halafu tulialikwa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Luxembourg. Kisha tuliombwa kwenda katika ofisi ya tawi ya Austria, huko Vienna. Tulipokuwa huko, mnamo mwaka wa 1972, tulianza kujifunza lugha ya Serbo-Croatian ili tuweze kuwahubiria Wayugoslavia wengi waliofanya kazi huko Vienna. Sasa kuna makutaniko manane ya lugha ya Serbo-Croatian hapa Vienna yenye watu kutoka karibu pembe zote za Ulaya!

Helene alikufa mnamo Agosti 27, 2001. Alikuwa rafiki na msaidizi mwenye kutegemeka na mwenye thamani katika ile miaka 53 ya ndoa yetu yenye furaha. Sasa ninatumaini ufufuo hata zaidi.

Naridhika na Upendo wa Mungu

Licha ya kupata misiba mingi, bado ninaridhika na kazi yangu katika ofisi ya tawi ya Austria. Hivi majuzi nimefurahia pendeleo la kusimulia mambo yaliyonipata zamani katika maonyesho yenye kichwa “Wahasiriwa wa Utawala wa Nazi Waliosahauliwa.” Tangu mwaka wa 1997 maonyesho hayo yamefanywa katika majiji na miji 70 nchini Austria. Watu walioachiliwa kutoka kwenye magereza na kambi za kazi ngumu za Wanazi ambao walijionea kwa macho yaliyotukia wamepata nafasi ya kusimulia jinsi Wakristo wa kweli walivyodhihirisha imani na ujasiri waliponyanyaswa na Wanazi.

Naona ni pendeleo kwamba niliwajua waaminifu hao. Walionyesha waziwazi ukweli wa andiko la Waroma 8:38, 39: “Wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

[Picha katika ukurasa wa 17]

Familia yetu katika mwaka wa 1930 (kushoto hadi kulia): mimi, Pepi, Baba, Willi, Mama, na Vinko

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ndugu yangu, Willi, muda mfupi kabla hajauawa

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mimi na Vinko tulitiwa katika Gereza la Stadelheim kwa muda huko Munich

[Picha katika ukurasa wa 19]

Binti ya Vinko, Fini, aliwekwa chini ya uangalizi wa familia katili ya Wanazi; bado ni mwaminifu hata leo

[Picha katika ukurasa wa 20]

Helene alikuwa mwandamani wangu mzuri sana kwa muda wa miaka 53 ya ndoa yetu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikizungumza katika maonyesho ya “Wahasiriwa wa Utawala wa Nazi Waliosahauliwa”