Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Dhambi Isiyosameheka?

Je, Kuna Dhambi Isiyosameheka?

Maoni ya Biblia

Je, Kuna Dhambi Isiyosameheka?

JE, KUNA adhabu mbaya kuliko kifo? Ndiyo, kifo bila tumaini la ufufuo kwa sababu ya kutenda dhambi isiyosameheka. Yesu alisema kwamba kuna dhambi ambayo ‘haitasamehewa.’—Mathayo 12:31.

Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Mungu yu tayari kusamehe. Tofauti na wanadamu ambao wanaweza kuweka kinyongo na kukosa kuwasamehe wengine, Mungu ‘husamehe kabisa.’ (Isaya 55:7-9) Mungu alihisi uchungu mkali alipomtuma Mwana wake mpendwa duniani ili awe dhabihu ya kupatanisha, au ya kufunika, yenye thamani kubwa sana hivi kwamba inaweza kufuta dhambi zetu.—Yohana 3:16, 17; Matendo 3:19; 1 Yohana 2:1, 2.

Wakati ujao Mungu atafufua wengi ambao walifanya dhambi nzito ambao wamekwisha samehewa kabisa makosa waliyofanya zamani. (Matendo 24:15; Waroma 6:23) Yesu alisema kwamba, watu watasamehewa “kila namna ya dhambi na kufuru,” ila dhambi isiyosameheka. (Mathayo 12:31) Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, ‘Ni kosa gani linaloweza kuwa baya sana hivi kwamba Mungu hawezi kulisamehe?’

Wakati Ambapo Toba Haiwezekani Tena

Onyo la Yesu lilihusu ‘kukufuru dhidi ya roho’ kimakusudi na kwa kupenda. Dhambi ya aina hiyo haiwezi kusamehewa. Yesu aliongeza: “Si katika mfumo huu wa mambo wala katika ule utakaokuja.” (Mathayo 12:31, 32) Watu wanaofanya dhambi hiyo hawatafufuliwa.

Inamaanisha nini kukufuru dhidi ya roho? Tendo hilo huanzia moyoni nalo huonyesha kwamba mtu ana nia mbaya na mwelekeo mwovu. Ni azimio la mtu la kuipinga roho takatifu ya Mungu kimakusudi linalofanya dhambi hiyo iwe nzito kuliko dhambi nyingine. Kwa mfano: Katika sehemu fulani ulimwenguni, kuna mauaji ya aina mbili kulingana na sheria. Kuna mauaji yaliyopangwa kimbele na mauaji ambayo hayakupangwa, na yanaainishwa kwa kutegemea kama kulikuwa na kusudi la kuua au njia ya kuua. Ni mwuaji aliyepanga kuua ndiye anayehukumiwa kifo.

Mtume Paulo alikuwa mkufuru hapo awali lakini alisema: “Nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikuwa asiye na ujuzi.” (1 Timotheo 1:13) Kufanya dhambi dhidi ya roho takatifu kunamaanisha kuipinga kimakusudi. Moyo wa mtu anayefanya dhambi hiyo huwa mwovu sana hivi kwamba hauwezi kubadilika kuwa mzuri.

Yaelekea Paulo alizungumzia dhambi ya aina hiyo alipoandika maneno haya: “Haiwezekani kwa habari ya wale ambao wametiwa nuru mara moja kwa wakati wote, na ambao wameonja zawadi ya bure ya kimbingu, na ambao wamekuwa washiriki wa roho takatifu, na ambao wameonja neno bora la Mungu na nguvu za mfumo wa mambo unaokuja, lakini ambao wameanguka, kuwarudisha tena kwenye toba.” (Waebrania 6:4-6) Mtume huyo alisema hivi pia: “Tukizoea dhambi kwa kusudi baada ya kuwa tumepokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyoachwa kwa ajili ya dhambi.”—Waebrania 10:26.

Mwenendo wa baadhi ya viongozi wa dini wa siku zake ndio uliomfanya Yesu atoe onyo juu ya dhambi isiyosameheka. Lakini hawakutii onyo lake. Badala yake walimwua. Baadaye walipata habari isiyokanushika kwamba roho takatifu ilikuwa imefanya mwujiza. Waliambiwa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa! Ilikuwa wazi kwamba Yesu alikuwa Kristo! Hata hivyo, waliipinga roho takatifu kwa kuwalipa askari Waroma waseme uwongo kuhusu ufufuo wa Yesu.—Mathayo 28:11-15.

Onyo kwa Wakristo wa Kweli

Kwa nini Wakristo wa kweli hutia maanani onyo hilo kuhusu dhambi isiyosameheka? Kwa sababu ijapokuwa tuna ujuzi sahihi juu ya Mungu na utendaji wa roho yake, bado moyo wetu unaweza kubadilika kuwa mwovu hatua kwa hatua. (Waebrania 3:12) Hatupaswi kamwe kufikiri kwamba jambo hilo haliwezi kutupata sisi. Fikiria Yudasi Iskariote. Awali alikuwa mfuasi mwaminifu wa Yesu. Alichaguliwa kuwa mmoja wa wale mitume 12, kwa hiyo, bila shaka alikuwa na sifa nzuri. Lakini wakati fulani alianza kuruhusu mawazo maovu na tamaa zikue, na mwishowe zikamshinda. Katika pindi ambazo alishuhudia miujiza ya ajabu ya Yesu, alikuwa akiiba pesa. Kisha, akamsaliti Mwana wa Mungu kimakusudi ili apate pesa.

Baadhi ya watu waliokuwa Wakristo waaminifu awali wamejitenga na Mungu kimakusudi. Huenda walifanya hivyo kwa sababu ya kuudhika, au kwa sababu ya kiburi au pupa. Sasa wao ni waasi-imani wanaoipinga roho ya Mungu. Wao hupinga kimakusudi kile ambacho wanajua vizuri ni kazi ya roho takatifu. Je, watu hao wamefanya dhambi isiyosameheka? Yehova ndiye Hakimu.—Waroma 14:12.

Badala ya kuwahukumu wengine, ni heri kila mmoja wetu ajiepushe na dhambi za siri ambazo zinaweza kufanya mioyo yetu kuwa migumu hatua kwa hatua. (Waefeso 4:30) Na tunafarijiwa kujua kwamba Yehova atasamehe kabisa hata makosa mazito ambayo tumetenda, iwapo tutatubu.—Isaya 1:18, 19.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Baadhi ya Mafarisayo walifanya dhambi isiyosameheka