Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!

Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!

Kuwatumia Watoto Vibaya Kutakoma Hivi Karibuni!

“KATIKA Azimio la Watu Wote la Haki za Binadamu, Umoja wa Mataifa ulitangaza kwamba watoto wana haki ya kutunzwa vyema na kusaidiwa,” ndivyo unavyosema utangulizi wa Mkataba wa Haki za Mtoto. Utangulizi huo unasema hivi pia kuhusu umuhimu wa familia: “Mtoto anahitaji kukua katika mazingira ya kifamilia yenye furaha, upendo, na amani ili utu wake usitawi kikamilifu na kwa njia inayofaa.” Hata hivyo, kusudi hilo halijatimizwa.

Haitoshi tu kuzungumza kuhusu ulimwengu bora unaowafaa watoto. Maadili yanazidi kuzorota, na watu wengi wanaliona kuwa jambo la kawaida. Utekelezaji wa sheria hauwezi kudhibiti pupa na ukosefu wa maadili ulioenea kotekote. Mara nyingi wazazi huendeleza mambo maovu badala ya kuwapenda na kuwalinda watoto wao. Basi kwa nini tutarajie kwamba ukahaba wa watoto utakoma?

Ijapokuwa ulimwengu huu mwovu umeshindwa kuhakikisha kwamba watoto wote wanaonyeshwa upendo nyumbani na wana wakati ujao salama, hivi karibuni Muumba wetu atakomesha kila namna ya uovu na ukosefu wa maadili kingono, kutia ndani ukahaba wa watoto. Karibuni, Yehova Mungu ataushangaza ulimwengu kwa kuingilia mambo ya wanadamu akitumia Ufalme wake. Mungu atawahukumu watu wote wanaowatumia wengine vibaya na kuwashawishi kutenda maovu. Wale tu wanaowapenda wanadamu wenzao ndio watakaookoka na kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.

Hebu wazia furaha itakayokuwapo wakati watoto na watu wazima watakapoishi bila kuvunjiwa heshima na kutumiwa vibaya kingono! Hata madhara ya kihisia-moyo na ya kimwili yanayotokana na kutumiwa vibaya na kutendewa jeuri yatatokomea kabisa. Wale waliotendewa vibaya kingono wataweza kuishi bila kumbukumbu mbaya au madhara ya mambo yaliyowapata. “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.

Wakati huo, hakuna mtoto atakayeteswa au kutumiwa vibaya kingono. Mambo kama vile furaha, upendo, na hali ya kuelewana hayatakuwa ndoto tu. Andiko la Isaya 11:9 linatangaza hivi kuhusu wenyeji wa ulimwengu mpya wa Mungu: “Hawatadhuru wala hawataharibu.”

Kwa kweli, kutakuwa na shangwe iliyoje wakati umaskini, matumizi ya dawa za kulevya, familia zenye huzuni, na maadili maovu yatakuwa yametoweka kabisa! Kutakuwa na amani, uadilifu, na usalama kotekote. “Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”—Isaya 32:18.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kuwatunza Watoto Kunaweza Kuzuia Familia Isivunjike

● “Wazazi wangu walinitia moyo kusoma kwa bidii shuleni na kujifunza ustadi fulani. Hawakujaribu kunilazimisha nifuate mapendezi yao, lakini walinisaidia kuchagua shule zilizokuwa na mitaala niliyotaka.”—Tais.

● “Mimi na dada yangu tuliandamana na mama yetu tulipoenda kununua bidhaa. Mbali na kutusaidia kutumia pesa vizuri, alitusaidia pia kutonunua mavazi yasiyo ya kiasi au yanayoonyesha uchi.”—Bianca.

● “Tulipoenda kwenye karamu, sikuzote wazazi wangu waliniuliza ni nani wangehudhuria, ni muziki wa aina gani ungechezwa, na wakati ambapo karamu ingeanza na kumalizika. Tulihudhuria karamu nyingi pamoja tukiwa familia.”—Priscila.

● “Nilipokuwa mtoto mchanga na tineja, nilizungumza kwa uhuru sana na wazazi wangu. Mwanashule mwenzangu aligundua jambo hilo akasema hivi: ‘Ninavutiwa sana kuona ukizungumza jambo lolote kwa uhuru na wazazi wako. Mimi hata sijihisi huru kuzungumza na mama yangu, kwa kawaida mimi huwauliza watu wengine mambo nisiyojua.’”—Samara.

● “Nilifurahia miaka yangu ya utineja. Niliwatumaini watu na niliangua kicheko daima. Nilistarehe sana nikiwa na rafiki zangu na tulipiga gumzo pamoja. Wazazi wangu walijua kwamba huo ni utu wangu, na hawakujaribu kunilazimisha kubadili utu wangu. Lakini kwa fadhili walinisaidia kutambua kwamba nilihitaji kuwa mwangalifu na kujiendesha kwa adabu nikiwa na watu wa jinsia tofauti.”—Tais.

● “Kama vijana wengine wengi, nilipendezwa mno na watu wa jinsia tofauti. Baba yangu aliniwekea umri ambao ningeweza kuanza kutafuta mchumba. Badala ya kuudhika, nilitambua kwamba wazazi wangu walinijali na walitaka kunilinda nisiumie wakati ujao.”—Bianca.

● “Niliona ndoa kuwa kifungo kizuri sana, hasa kwa sababu ya mfano mzuri wa wazazi wangu. Daima walikuwa na uhusiano mzuri na walidumisha mawasiliano mazuri. Ninakumbuka wakati nilipokuwa nikichumbiwa, mama yangu alinipa mashauri kuhusu jinsi ya kutenda katika hali fulani na alinieleza jinsi ambavyo jambo hilo lingeathiri ndoa yangu.”—Priscila.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, hakuna mtoto atakayetendewa vibaya kamwe