Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tatizo Hilo Linaenea?

Kwa Nini Tatizo Hilo Linaenea?

Kwa Nini Tatizo Hilo Linaenea?

JE, WAJUA kwamba biashara haramu ya kuwauza wanadamu ni uhalifu wa tatu kwa ukubwa ulimwenguni, baada ya ulanguzi wa dawa za kulevya na uuzaji wa silaha? Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa linasema kwamba kuna ukahaba wa kila aina unaoongezeka kwa kasi sana.

Katika nchi moja ya Amerika ya Latini, Tume Maalumu ya Uchunguzi iliripoti kwamba kuna zaidi ya wasichana wadogo makahaba 500,000, licha ya kwamba ukahaba si halali.

Katika nchi nyingine, kuna watoto makahaba 300,000 hivi mitaani, hasa katika maeneo yenye ulanguzi wa dawa za kulevya.

Imeripotiwa kwamba wasichana wapatao milioni moja katika nchi za Asia hutumiwa kama makahaba na kutendewa kama watumwa. Nchi nyingine ni vituo vikuu vya ngono na ukahaba wa watoto.

Kwa sababu ya kuenea sana kwa magonjwa yanayoambukizwa kingono, kama vile UKIMWI, wateja huwa tayari kulipa pesa nyingi zaidi ili wafanye ngono na watoto ambao wanadhaniwa kuwa mabikira na ambao huenda hawajaambukizwa. “Tatizo hilo linazidi kuongezeka kwa sababu hofu ya UKIMWI inawafanya wanaume watafute wasichana na wavulana wenye umri mdogo zaidi,” aeleza Luíza Nagib Eluf wa Wizara ya Sheria nchini Brazili. Alisema: “Kuwatumia wasichana na wavulana wadogo vibaya kingono ni tatizo kubwa sana la kijamii linalowakabili wanawake maskini nchini Brazili.”

Umaskini na Ukahaba wa Watoto

Ukahaba wa watoto husitawi katika maeneo yenye umaskini na taabu. Afisa mmoja wa serikali alisema kwamba ukahaba na utumwa wa watoto nchini mwao “unahusiana moja kwa moja na kuvunjika kwa familia na kunasababishwa na taabu na njaa.” Wazazi fulani wanadai kwamba waliwauza watoto wao kuwa makahaba kwa sababu ya umaskini. Watoto wa mitaani hufanya ukahaba kwa sababu wanaona ndiyo njia pekee ya kujiruzuku.

Gazeti la O Estado de S. Paulo linaeleza kwamba msichana anayeshirikiana na genge la mitaani huenda mwishowe akawa kahaba. Huenda akalazimika kuiba na kufanya ukahaba mara kwa mara ili apate chakula. Hatimaye anakuwa kahaba kabisa.

Nyakati nyingine vijana hupelekwa nchi nyingine kufanya kazi ya ukahaba. “Mara nyingi makahaba wahamiaji hutuma pesa nyingi kwa familia zao ambazo zinaishi katika nchi maskini sana za Asia na Afrika,” charipoti kichapo UNESCO Sources. “Nchi hizo zinaendeleza ukahaba kwa sababu watalii kutoka nchi tajiri huja tu kufanya ngono na vijana na watoto makahaba.”

Gazeti la Time linaripoti hivi kuhusu hatari zinazowakabili watoto wa mitaani walio makahaba katika jiji moja la Amerika ya Latini: “Baadhi ya makahaba hao wana umri wa miaka 12 tu. Kwa kawaida watoto hao wanaotoka kwenye familia zilizovunjika, hulala mahali popote wakati wa mchana, na kurandaranda kwenye madisko usiku wakitafuta mabaharia wa kufanya ngono nao.”

Msichana mdogo kahaba aliyelewa dawa za kulevya hutendewa unyama ambao kwa kawaida hangekubali kamwe. Kwa mfano, gazeti la Veja linasema kwamba polisi waligundua kaseti 92 za video zilizorekodiwa na daktari mmoja, zinazoonyesha zaidi ya wanawake 50 wakiteswa kinyama baadhi yao wakiwa wasichana wadogo.

Licha ya matukio hayo yenye kushtua, kijana mmoja kahaba alisema: “Siwezi kamwe kupata kazi yoyote ya kuajiriwa inayoweza kutosheleza mahitaji yangu kwa sababu sina ujuzi wowote wa kazi. Familia yangu inajua kazi ninayofanya, na sitaki kuacha maisha haya. Mwili ni wangu, nami nautumia kama nipendavyo.”

Hata hivyo, wasichana hawa hawakukusudia kamwe kuwa makahaba. Mfanyakazi mmoja wa huduma za jamii anasema kwamba makahaba wengi watoto “wangependa kuolewa” na wanatamani kupata mchumba anayewafaa kabisa. Ingawa kuna hali ngumu zilizowaingiza katika maisha ya ukahaba, mchunguzi mmoja anadai hivi: “Jambo lenye kusikitisha zaidi ni kwamba wengi wao walibakwa wakiwa nyumbani kwao.”

Je, Ukahaba wa Watoto Utakoma?

Hata hivyo, kuna tumaini kwa watoto hao wanaoteseka. Kuna makahaba wenye umri mbalimbali ambao wameacha maisha hayo. (Ona sanduku “Watu Wanaweza Kubadilika,” kwenye ukurasa wa 7.) Neno la Mungu, Biblia, limesaidia mamilioni ya watu kotekote ulimwenguni kuwa majirani wema na washiriki waaminifu wa familia. Twasoma hivi kuhusu watu ambao hapo awali walikuwa waasherati, wazinzi, wezi, wenye pupa, na walevi: “Baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.

Leo, kama ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, kuna watu ambao wanabadili maisha yao na kuwa watu wazuri. Hata hivyo, jitihada zinahitajiwa ili kukomesha tabia ya kuwatumia wengine kingono. Serikali na mashirika fulani yanajitahidi kukomesha watalii wanaofanya ukahaba na ukahaba wa watoto. Lakini kwa kweli, wanadamu hawawezi kukomesha taabu na umaskini. Watungaji wa sheria hawawezi kuzuia mawazo na mielekeo inayosababisha ukosefu wa maadili.

Ufalme wa Mungu ndio utakaotatua matatizo hayo yote wala si jitihada za wanadamu. Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Mara nyingi umaskini huchangia ukahaba wa watoto

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Matokeo Mabaya Sana

Daisy alikuwa na umri wa miaka sita tu alipobakwa na ndugu yake. Kwa sababu hiyo, akaishi na kaka yake hadi alipofikia umri wa miaka 14, kisha akaanza kufanya kazi kwenye klabu ya usiku. Baada ya siku chache, Daisy akawa mgonjwa. Alipopata nafuu, wasimamizi wa klabu hiyo walimwambia alipe pesa walizomdai, hivyo akaamua kuwa kahaba. Mwaka mmoja hivi baadaye, hakuwa amelipa deni hilo, na ilionekana kwamba hangeweza kamwe kukamilisha deni hilo. Hata hivyo, baharia mmoja alimlipia deni lililobaki, na kumpeleka hadi jiji jingine ambako alitendewa kama mtumwa. Daisy alimwacha mwanamume huyo na baadaye akaishi na mwanamume mwingine kwa miaka mitatu halafu wakafunga ndoa. Alijaribu kujiua mara tatu kwa sababu ya matatizo mengi mazito katika ndoa yao.

Hatimaye, yeye na mumewe wakaanza kujifunza Biblia. Lakini Daisy alijiona hafai kuwa Shahidi wa Yehova. Alipoonyeshwa kwenye Biblia kwamba Yehova Mungu anakubali watu wanaofanya mabadiliko yanayofaa, alijiweka wakfu kwake. Daisy alijitahidi sana kufanya mambo yanayofaa, lakini alihisi kwamba hayatoshi na hivyo alishuka moyo pindi kwa pindi. Ingawa hivyo inatia moyo kwamba amekubali kusaidiwa ili awe na usawaziko na kushinda hisia za majuto zinazomsumbua kwa sababu ya kubakwa na maisha yake ya ukahaba alipokuwa mtoto.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Watu Wanaweza Kubadilika

Yesu Kristo alipokuwa duniani, aliwahurumia watu wenye dhambi, waliotaabika. Alijua kwamba makahaba wangeweza kubadilika haidhuru umri wao. Yesu hata aliwaambia hivi viongozi wa kidini: “Kwa kweli nawaambia nyinyi kwamba wakusanya-kodi na makahaba wanaenda mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 21:31) Ijapokuwa watu hao wenye mioyo inayofaa walidharauliwa kwa sababu ya namna yao ya maisha, walisamehewa walipotia imani katika Mwana wa Mungu. Watenda-dhambi wenye kutubu walikuwa tayari kuacha maisha yao ya ukahaba ili wapokee baraka za Ufalme wa Mungu. Kisha, waliishi kupatana na kanuni za Mungu za uadilifu. Leo pia, watu wa kila namna wanakubali kweli ya Neno la Mungu halafu wanabadili maisha yao.

Fikiria mambo yaliyompata Maria, Carina, na Estela, waliotajwa kwenye makala ya kwanza. Mbali na kukinza shinikizo la mama yake la kumtaka aendelee kufanya ukahaba, Maria alijikakamua sana kuacha kutumia dawa za kulevya. Anasema hivi: “Nilitumia dawa za kulevya ili nitulize hisia za kujiona sifai kwa sababu ya kuishi maisha ya ukahaba.” Maria anaeleza jinsi alivyokaribishwa na kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova: “Nilivutiwa na upendo ambao nilionyeshwa na washiriki wa kutaniko. Wote—watoto kwa watu wazima—walinitendea kwa heshima. Niliona kwamba waume ni waaminifu kwa wake zao. Nimefurahi sana kukubaliwa kama rafiki yao.”

Alipokuwa na umri wa miaka 17, Carina alitembelewa na Mashahidi wa Yehova. Alianza kujifunza Biblia, ingawa aliendelea na kazi yake ya ukahaba kwa muda fulani. Hatua kwa hatua, alianza kuthamini kweli za Biblia. Akaamua kuhamia mji mmoja wa mbali, na huko akawa Shahidi wa Yehova.

Estela, ambaye alikuwa kahaba na mlevi wa kupindukia alipokuwa mtoto, alianza kupendezwa na Biblia. Hata hivyo, alikata shauri kwamba Mungu hawezi kamwe kumsamehe. Lakini, punde si punde, alifahamu kwamba Yehova Mungu huwasamehe watu wanaotubu. Sasa Estela akiwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo aliyefunga ndoa na mama mwenye watoto watatu, anasema hivi: “Nina furaha na ninamshukuru sana Yehova kwa sababu aliniokoa kutoka kwenye maisha hayo machafu na amenikaribisha katika tengenezo lake safi.”

Masimulizi hayo yanaunga mkono maneno ya Biblia ya kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mara nyingi watoto makahaba hutumia dawa za kulevya

[Picha katika ukurasa wa 5]

© Jan Banning/Panos Pictures, 1997