Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Habari Kamili

Pata Habari Kamili

Pata Habari Kamili

Ni vigumu kupata habari kamili kuhusu masuala mbalimbali. Serikali na mashirika husema kweli nusu-nusu. Mara nyingi vyombo vya habari huahidi kuripoti kwa usahihi, lakini havitimizi ahadi hizo. Madaktari hawaelezi athari za dawa wanazopendekeza kikamili. Je, kuna njia ya kupata habari za kuaminika?

Wakati Internet ilipobuniwa, watu wengi waliiona kuwa njia ya kupata habari zenye kutegemeka kutoka ulimwenguni pote. Jambo hilo linawezekana tu iwapo unajua kituo cha Internet kilicho na habari fulani. “Uzuri wa Internet ni kwamba inaweza kuwaelimisha watu wengi sana haraka kuliko chombo kingine cha habari. Hasara yake ni kwamba inaweza kuwapumbaza watu upesi kuliko vyombo vingine vya habari,” yasema tahariri katika gazeti The New York Times.

Tahariri hiyo iliendelea kusema: “Internet inavutia watu kwa sababu ni ya ‘kitekinolojia,’ hivyo, wale wasio na elimu huiamini sana. Hawajui kwamba Internet, ni kama bomba la maji machafu: ni chombo cha kielektroni kinachopitisha habari zisizothibitishwa na zisizochunguzwa.” Kwa kusikitisha, kama vile mwandishi huyo alivyokiri, hakuna programu yoyote ya kuondoa upuuzi huo.

Mtu yeyote anaweza kuweka habari zozote kwenye Internet, au kuziandika katika gazeti au kitabu. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia utambuzi na kuwa na ufahamu ili tusiamini tu habari zote tunazosoma. Wale wanaotaka kupata habari sahihi lazima wathibitishe kwamba chanzo chake kinategemeka. Huenda hilo likachukua wakati. Lakini tunapopata habari kamili, tunaweza kufikiri vizuri, kufanya maamuzi mazuri na kuwa na uhakika na mambo tunayoamua.