Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Uhalifu wa Kikatili”

“Uhalifu wa Kikatili”

“Uhalifu wa Kikatili”

MARIA * alianza kufanya ukahaba akiwa mtoto mwenye umri wa miaka 14. Mama yake ndiye aliyemlazimisha kuishi maisha haya yenye kuchukiza sana. Alimwambia kwamba wanaume wangevutiwa sana na urembo wake, na angepata pesa nyingi. Wakati wa jioni, Maria alipelekwa na mamaye kwenye hoteli moja yenye vyumba vya kulala ambako walikutana na wanaume. Kila usiku, Maria alifanya ngono na wanaume watatu au wanne ambao walimlipa mamaye aliyekuwa karibu.

Carina mwenye umri wa miaka 13, anayeishi karibu na Maria, alilazimishwa pia kuwa kahaba. Kama wazazi wengine wengi waliokuza miwa katika eneo lao, wazazi wa Carina walimwingiza katika kazi ya ukahaba ili awaletee pesa zaidi za matumizi. Kwingineko, Estela aliacha shule akiwa mtoto mdogo asiyejua kusoma wala kuandika, akaanza kufanya kazi ya ukahaba mitaani. Naye Daisy alikuwa na umri wa miaka sita hivi alipobakwa na nduguye—tangu hapo alibakwa mara nyingi. Alianza ukahaba akiwa na umri wa miaka 14.

Katika sehemu nyingi ulimwenguni, tatizo la watoto makahaba limeenea kwa njia yenye kutisha sana. Matokeo yanasikitisha. Mara nyingi watoto wanaofanya ukahaba kwa ukawaida au pindi fulani-fulani, hufanya pia uhalifu na kutumia dawa za kulevya. Wengi wao hukata tamaa na kujihisi hawafai wanapoona kwamba hakuna tumaini la kuacha maisha hayo yenye taabu.

Watu mashuhuri wanatambua matokeo mabaya sana ya ukahaba wa watoto. Aliyekuwa rais wa Brazili Fernando Henrique Cardoso alisema hivi waziwazi: “Ukahaba wa watoto ni uhalifu wa kikatili.” Maelezo haya mazito kuhusu ukahaba wa watoto yalichapishwa katika gazeti moja la Brazili: “Nchi ambazo zimekubali ukahaba kuwa jambo la kawaida, na ambazo zinauendeleza kwa sababu ya [pesa], zinakabili matokeo mabaya ya zoea hilo kila siku. Faida yoyote ya kifedha ambayo huenda ikapatikana haiwezi kamwe kulinganishwa na misiba inayompata mtu binafsi, familia na jamii kutokana na zoea hilo.”

Hata hivyo, ukahaba wa watoto unaenea licha ya kwamba watu fulani wanajitahidi sana kukomesha tatizo hilo. Ni nini kinachosababisha hali hiyo yenye kusikitisha? Kwa nini watu wengi hukubali au hata kuendeleza uhalifu huo?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa katika mfululizo huu wa makala.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

“Ukahaba wa watoto ni uhalifu wa kikatili.”—ALIYEKUWA RAIS WA BRAZILI FERNANDO HENRIQUE CARDOSO

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Matendo yote ya kuwatumia watu wengine vibaya kingono yanavunja heshima ya binadamu, na hivyo yanakiuka haki za msingi za binadamu, haidhuru umri, jinsia, jamii, kabila au tabaka la mtu anayetendewa hivyo.”—UNESCO SOURCES