Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inafaa Nitazame Video za Muziki?

Je, Inafaa Nitazame Video za Muziki?

Vijana Huuliza . . .

Je, Inafaa Nitazame Video za Muziki?

“Video za muziki ni nzuri sana. Nyingine ni kama sinema fupi. Ninapenda matukio yanayoonyeshwa katika video hizo, na jinsi watu wanavyocheza dansi.”—Casey.

“Video hizo zinamwezesha mtu kujua muziki mpya ambao umetolewa karibuni. Zinakuwezesha kusikiliza muziki tofauti, mbali na vile vibao 40 vya kawaida. Pia, watu hupenda kuzungumza kuhusu mambo wanayoona katika video za muziki.”—Josh.

“Ninapenda habari zinazoonyeshwa katika video hizo—kama vile jina la mwimbaji, jinsi alivyovalia, na anavyotenda. Mambo hayo yote hunisaidia kujua maana ya wimbo.”—Kimberly.

“Mimi hutaka kuona vibao vipya ambavyo vimetolewa na bendi ninayoipenda. Ninapenda madoido yanayoonyeshwa katika video hizo. Na video nyingine huchekesha. Lakini mtu anapaswa kujihadhari.”—Sam.

HUENDA wewe pia unapenda kutazama video za muziki. Video hizo zilipoanza kuonyeshwa mara ya kwanza kwenye televisheni, hazikuwa na madoido mengi. Lakini video hizo zilipokuwa maarufu na zikauzwa sana, ziliongezwa madoido mengi ya kisanaa na ya kitekinolojia. Leo, video hizo zinatumiwa sana katika fani ya muziki na vijana wanazipenda sana. Katika nchi nyingine, vituo fulani vya televisheni huonyesha video za muziki peke yake!

Lakini kwa nini vijana wengine, kama vile Sam, aliyenukuliwa hapo juu, wanasema kwamba mtu anapaswa kujihadhari? Je, video fulani za muziki zinaweza kukuathiri—labda kuchafua akili yako na kupotosha maadili yako na hata kuharibu uhusiano wako na Muumba wako? Huenda mtu akasema kwamba haziwezi kukuathiri sana hivyo. Lakini hebu fikiria jambo hili, Tuseme ungeenda kuogelea ziwani au baharini, kisha uone ishara zinazoonya kwamba ni hatari kuogelea hapo, je, lingekuwa jambo la hekima kupuuza maonyo hayo? La hasha. Basi, itafaa uzingatie maonyo fulani kuhusu video za muziki.

Hatari

Unapaswa kutambua kwamba yale unayoona na kusikia yanaweza kukuathiri! Biblia inatuambia kwamba muziki ulimsaidia Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, kutuliza hisia zake. (1 Samweli 16:14-23) Je, muziki unaweza kuwa na athari mbaya? Kitabu kinachoitwa Rock and Roll—Its History and Stylistic Development kinasema hivi: “Mtu hawezi kusema kwamba muziki unamwathiri nyakati fulani na kwamba nyakati nyingine haumwathiri. Iwapo tunakubali kwamba muziki wa roki umewaathiri watu kwa njia nzuri (kwani huo ndio ukweli), tunapaswa pia kukubali kwamba umewaathiri vibaya (kwani huo ndio ukweli). Mtu anayesema kwa majivuno hivi, ‘Ah, mimi husikiliza muziki bila kuathiriwa nao,’ ni mpumbavu kabisa au hafahamu mambo hata kidogo.”

Biblia huonyesha mara nyingi jinsi macho yanavyoathiri fikira na hisia zetu. (Mithali 27:20; 1 Yohana 2:16) Kwa hiyo, watengenezaji wa video za muziki wanapotia madoido yenye kuvutia macho, wao hufanya muziki huo uwaathiri wasikilizaji hata zaidi. Mara nyingi wao hutumia vivutio gani?

Kulingana na uchunguzi mmoja, asilimia 57 hivi ya video za muziki wa roki huonyesha jeuri. Karibu asilimia 76 ya video hizo huonyesha matendo mbalimbali ya ngono. Na uchunguzi mwingine uliofanywa hivi majuzi ulionyesha kwamba asilimia 75 ya video zinazosimulia visa fulani zinaonyesha pia mambo fulani yanayohusiana na ngono, na zaidi ya asilimia 50 ya video hizo zilionyesha jeuri, hasa kuwaelekea wanawake. Basi, je, si inawezekana video hizo zikuathiri? Gazeti moja linasema kwamba “uchunguzi mbalimbali umeonyesha kuwa kutazama video za muziki kwaweza kuwashawishi vijana kufanya ngono wakiwa wachanga au kujihusisha katika matendo mengine hatari ya kingono.” Hakuna shaka kwamba video za muziki zinazidi kuwa chafu kwani wanamuziki wanajaribu kutokeza muziki wenye kushtua zaidi ili kuwapita wanamuziki wengine wa sasa na wa zamani.

Mtaalamu mmoja katika fani ya elimu alisema: “Watu wengi husema kwamba muziki wanaosikiliza na kuona kwenye video za muziki si tofauti na muziki wa vizazi vilivyopita . . . Lakini yaonekana kwamba wanamuziki wengi wa sasa hutumia maneno machafu na yenye kuchukiza ili muziki wao ununuliwe sana.” Na gazeti la Chicago linasema hivi kuwahusu watazamaji wa kituo fulani cha televisheni kinachoonyesha video za muziki: “Kila wakati wanaonyeshwa picha nyingi chafu.”

Gazeti la Chicago linazungumza pia kuhusu video moja ya muziki ambayo inaonyesha “kijana mmoja akiwa ameketi kwenye kaunta mkahawani na kuegemeza kichwa chake nyuma sana. Anapata jeraha kubwa jekundu shingoni, kisha kichwa chake kinaanguka.” Yasemekana kwamba video nyingine ilionyesha mwanamume mmoja akivua nguo hatua kwa hatua kisha akaondoa nyama yake na misuli yake pia. Mambo mengine yanayotisha sana yalionyeshwa pia.

Huenda wengine wakapuuza mambo hayo, wakisema kwamba video zilizofafanuliwa hapo juu zimepita kiasi na kwamba video nyingi si mbaya sana. Huenda wengine hata wakasema kwamba hawadhani video za muziki zinachukiza. Lakini, je, inawezekana kwamba watu hao hawachukizwi nazo kwa sababu wameziona mara nyingi sana? Casey, yule kijana aliyenukuliwa mwanzoni, anakubali hivi: “Usipoweka mipaka kuhusu yale unayotazama, utazoea kutazama mambo uliyoyachukia hapo awali. Bila kutambua, utajikuta ukitaka kutazama mambo yenye kuchukiza hata zaidi na kukubali haraka mambo uliyoyachukia hapo zamani.”

Ni nini kinachoweza kutokea? Huenda uwezo wako wa kufanya maamuzi mazuri ukadhoofika sana. Kwa kuwa akili zetu zinaweza kuathiriwa kwa urahisi, Biblia inatuhimiza ‘tulinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.’ (Mithali 3:21, NW; 5:2) Unaweza pia kuharibu urafiki wako pamoja na Yehova Mungu. Ama kweli, urafiki huo ndio kitu chenye thamani sana kwako. Basi, unapaswa kulinda urafiki huo kwa kujitahidi kuepuka burudani yoyote isiyofaa. Jinsi gani?

Jilinde

Kwanza, tafadhali kubali kwamba ni vibaya kutazama sinema zinazoonyesha mambo ambayo Biblia inapinga waziwazi. (Zaburi 11:5; Wagalatia 5:19-21; Ufunuo 21:8) Video inapoonyesha mambo ‘yasiyowafaa watu watakatifu,’ unapaswa kuacha kuitazama mara moja. (Waefeso 5:3, 4) Ni kweli kwamba kubadili kituo—au kuzima televisheni—si rahisi ikiwa video inasisimua. Basi huenda ukahitaji kusali kama mtunga-zaburi, ambaye aliandika hivi: “Unigeuze macho yangu nisitazame visivyofaa.”—Zaburi 119:37.

Huenda ukaepuka kutazama video zinazochukiza, kama zile tulizozungumzia awali. Hata hivyo, video nyingine hazionyeshi mambo machafu waziwazi. Video hizo zinaweza kuonyesha mambo ya ngono kifupi tu. Maneno na picha za video hizo zinaweza kuchanganywa kwa ustadi ili kufundisha wazo fulani lisilopatana na kanuni za Mungu bila kusema au kuonyesha jambo lolote chafu. Isitoshe, dhamiri yako ikikusumbua hata kidogo kwa sababu ulitazama video fulani, huenda video hiyo haikuwa nzuri au haikupatana na kanuni za Kikristo. Basi, unawezaje kuamua kile utakachotazama na kile ambacho hutatazama iwapo video haionyeshi mambo machafu waziwazi?

Ama kwa hakika, ikiwa unataka kutazama video za muziki, unapaswa kuzungumza na wazazi wako kwani wao ndio wana daraka la kuamua yale unayotazama. (Waefeso 6:1, 2) Lakini wazazi wako wakikuruhusu utazame video za muziki, hupaswi kufuata tu maoni yako mwenyewe. Andiko la Waebrania 5:14 linatutia moyo ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu’ ili “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa.” Nguvu zetu za ufahamu zinazoezwa kwa kujifunza kanuni za Biblia, ambazo zinatuwezesha kutofautisha yaliyo mema na yaliyo mabaya machoni pa Yehova. Ukitafakari kanuni hizo za Biblia, utaweza kutambua mambo yanayoweza kuhatarisha hali yako ya kiroho hata kama hakuna sheria hususa ya Biblia ya kukuongoza.

Basi, ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kukuongoza kwa habari ya kutazama video za muziki? Hilo litazungumziwa katika makala ya wakati ujao.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Mtu anayesema kwa majivuno hivi, ‘Ah, mimi husikiliza muziki bila kuathiriwa nao,’ ni mpumbavu kabisa au hafahamu mambo hata kidogo”

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, kweli unaweza kutazama kitu kisichofaa na usiathiriwe nacho?