Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku za Wageni Zilizovutia Wengi

Siku za Wageni Zilizovutia Wengi

Siku za Wageni Zilizovutia Wengi

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI UJERUMANI

“ILIKUWA siku nzuri ajabu!” “Asanteni kwa ukarimu wenu na maonyesho yenye kupendeza. Tulihisi tumekaribishwa.” Kwa nini wageni wengi walitoa maelezo hayo ya uthamini? Walikuwa wamealikwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani. Kwa muda wa siku tatu, kuanzia Ijumaa, Mei 24, hadi Jumapili, Mei 26, 2002, wageni walikaribishwa kujiunga na wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya 1,000 kuadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwa ofisi ya Ujerumani huko Selters-Taunus.

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yaliyo karibu na ofisi ya tawi yalifanya kampeni kabambe ya kuwaalika watu. Majuma mawili kabla ya sherehe hiyo kubwa, zaidi ya mialiko 100,000 ilitawanywa kwa watu binafsi au ikaachwa nyumbani mwao. Walitumia pia redio na matangazo marefu magazetini. Watu ambao huleta bidhaa kwenye ofisi ya tawi na maafisa wengine walialikwa kibinafsi. Zaidi ya watu 7,000 walikubali kuja—wengi hawakuwa Mashahidi.

Wageni walitembezwa katika matbaa, mahali pa kujalidi vitabu, idara ya upakiaji, mahali pa kurekebisha vitu, dobi, na sehemu za jengo la usimamizi. Maonyesho fulani yalionyesha vile Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani walivyofuata kanuni za Biblia kwa uthabiti wakati wa utawala wa Nazi na wa Kikomunisti. Onyesho moja la Biblia lililokuwa na zaidi ya vitu 700 lilikazia matumizi ya jina la Mungu, Yehova. Haiwezekani kutaja maelezo yote ya uthamini yaliyotolewa na watu, lakini yafuatayo ni baadhi ya maelezo hayo.

“Kila mtu ni mwenye urafiki. Kila kitu ni safi na nadhifu. Kuna upatano kati ya watu na mazingira. Tunatumaini kwamba mtatuambukiza urafiki wenu.”—Wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa.

“Asanteni sana kwa chakula kitamu na kwa kutushughulikia kwa njia nzuri, yenye urafiki. Tulikifurahia sana, na tungependa kurudi tena. Watu wa hapa ni wazuri kwelikweli!”—Maelezo yalioandikwa katika kitabu cha wageni na kikundi cha wanafunzi wa chuo cha ufundi wa glasi.

“Asanteni sana kwa kutukaribisha kwa uchangamfu kwenye ofisi yenu. Tulifurahia sana matembezi hayo. Tunawapongeza wale wanaofanya kazi katika dobi. Hatujawahi kamwe kuona mahali pengine palipo safi na nadhifu hivyo.”—Barua-pepe kutoka kwa mwakilishi wa kampuni inayouza sabuni na vifaa vya dobi.

Eva aliyewatembeza wageni alisema: “Katika kila kikundi nilichotembeza, mtu fulani alisema hivi kuhusu vyumba vya makazi: ‘He! tunaenda kuleta mizigo yetu. Tuko tayari kuhamia hapa!’”

Mwanamke fulani aliyekuwa katika kiti cha magurudumu alikuwa akitazama michoro ya majengo ya ofisi, alipoulizwa na mfanyakazi mmoja wa kujitolea kama alihitaji msaada. Alijibu “la!” Alisema kwamba tayari alikuwa ndani ya jengo hilo kwa muda wa saa tano na hangeweza kuketi wima tena. Kwa kawaida huwa hatoki kitandani, na wakati huo alikuwa na maumivu makali. Hata hivyo, alisema: “Naweza kulala nirudipo nyumbani, lakini hii ni sherehe inayofanywa mara moja tu!” Aliongeza kusema: “Kila kitu kinavutia sana na ndiyo sababu nataka kuona vyote!”

Georg, mwenye umri wa miaka mitano hivi aliulizwa ni nini kilichompendeza zaidi. Kwa kuwa alipendezwa na mashine ya kuchapa, alijibu hivi: “Nilipendezwa na makaratasi yaliyoviringwa! Wao huyaweka makaratasi hayo upande mmoja halafu magazeti hutokea upande wa pili. Hilo ni jambo lenye kuvutia mno!”

Shahidi mmoja alishangazwa na mume wake. Mume huyo, ambaye si Shahidi alikuwa amehudhuria mkutano mmoja tu wa Kikristo na alikubali kutembelea ofisi ya tawi Jumamosi. Jumapili mke wake aliporudi nyumbani kutoka mikutano ya kutaniko, alimkuta mumewe akiwa nadhifu na tayari kutoka. Mke wake alimuuliza “Unataka kufanya nini?” Alijibu: “Sikuona kila kitu jana. Kwa hiyo ukiwa tayari tutaenda Selters. Ninataka kwenda kuona vizuri.”

Kwenye maonyesho ya Biblia, mwanamke mmoja mzee aliyekuwa nadhifu, aliomba kutumia simu huku akionekana mwenye wasiwasi, kwa sababu alitaka kupiga simu ya dharura. Mume wake hufanya kazi ya kujalidi vitabu, hasa vile vya zamani. Yeye na mumewe hukutana kwa kawaida na watu wengine wanaopenda vitabu, mmoja ambaye ni kasisi Mprotestanti anayependa kukusanya Biblia. Mwanamke huyo alitaka sana kumpigia simu kasisi huyo. Kwa sababu hakumpata nyumbani, alimwachia ujumbe huu kwenye mashine ya kujibu simu: “Uje hapa leo ukiweza. Nina hakika hujawahi kuona kitu kama hiki. Usikose kuja kukiona!”

Wenzi fulani pamoja na mtoto wao walikuwa wamekuja kutoka mji jirani wa Limburg. Hawakuwa wamesikia kuhusu Mashahidi wa Yehova hadi walipokuta mwaliko nyumbani mwao. Waliamua kuja ili wajionee ofisi hiyo kubwa ya Selters. Marlon na Leila, ambao ni wafanyakazi wa kujitolea katika ofisi ya tawi ya Ujerumani, walikutana na wenzi hao na kuwaeleza mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova na jinsi watu wanavyoishi katika ofisi hiyo. Familia hiyo ilivutiwa sana hivi kwamba wazazi wakaomba mtu fulani ajifunze Biblia pamoja na watoto wao kwa ukawaida.

“Ilikuwa siku ya kufurahisha sana na yenye kupendeza. Ingawa niliona mashine ya kuchapa tu, nilivutiwa sana. Nyinyi ni watu wazuri sana, wenye urafiki. Mimi napenda watu kama nyinyi.”—Stefanie (mwenye umri wa miaka 12), maelezo katika kitabu cha wageni.

Mwanamke mmoja anayeishi katika kijiji kilicho karibu alisema: “Kuna jambo ninalotaka kuwaambia. Mimi ni Mwislamu, lakini sikuzote nimetaka kuja kuona ofisi yenu. Nyinyi nyote ni watu wa kupendeza na watulivu. Mnatufanya sisi [wageni] tuhisi tumekaribishwa hapa Ujerumani. Mnapendezwa na watu. Hongera! Kesho nitarudi hapa nikiwa na mume wangu.” Yeye aliandika hivi katika kitabu cha wageni: “Hii ilikuwa siku kubwa! Ni kana kwamba niko katika Paradiso.”

Dereva wa kigari kimoja kilichowasafirisha wageni kati ya maegesho na milangoni, alimsikia abiria mmoja akimwambia mwenzake: “Ni wenye urafiki sana! Sikujua kamwe kazi inayofanywa hapa. Sasa nimejua kazi wanayofanya. Ona jinsi wanavyojiendesha vizuri. Dini yao ndiyo inayowafundisha kuwa watu wazuri hivyo.”

Saa mbili baada ya sherehe kumalizika, mtu mmoja alitembea huku na huku uani mbele ya jengo la usimamizi. Alikuwa akiwaza na kuwazua na kutikisa kichwa chake akitazama nyuma kwenye jengo hilo. Kisha akamwambia mfanyakazi mmoja wa kujitolea hivi: “Ni wazi kwamba kila kitu kilifanywa kwa upendo. Mimi si Shahidi wa Yehova, lakini nawatakia baraka za Yehova.”

Shahidi mmoja aliandika hivi: “Kupitia barua hii fupi ninawashukuru kutoka moyoni mwangu. Mlijitahidi sana kufanya siku hizi za wageni kuwa zenye kufurahisha kabisa. . . . Kwa ujumla, mlionyesha jinsi wanadamu wote watakavyoishi pamoja kwa umoja wakati ujao! . . . Siku hizo za wageni zilimletea Mungu wetu Yehova utukufu.”—Sandra.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Vigari vilivyowasafirisha wazee, walemavu, au waliochoka tu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Maonyesho ya njia za kuhubiri zilizotumiwa zamani

[Picha katika ukurasa wa 23]

Karibuni nyote

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mfanyakazi wa kujitolea anaeleza kwa njia rahisi matumizi ya tekinolojia

[Picha katika ukurasa wa 24]

Maonyesho ya Biblia