Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kutumiaje Uhuru Wetu wa Kuamua?

Tunapaswa Kutumiaje Uhuru Wetu wa Kuamua?

Maoni ya Biblia

Tunapaswa Kutumiaje Uhuru Wetu wa Kuamua?

MUNGU aliwapa wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, uwezo wa kufanya maamuzi yao wenyewe. Alimpa Adamu daraka la kutunza bustani ya Edeni na pia kazi ya kuwapa wanyama majina. (Mwanzo 2:15, 19) Na jambo la maana zaidi ni kwamba Adamu na Hawa wangeweza kuamua ikiwa watamwabudu Mungu au la.—Mwanzo 2:17, 18.

Tangu wakati huo, wanadamu wamefanya maamuzi mengi sana. Mengi ya maamuzi hayo yamekuwa mazuri, mengine hayakufaa, na mengine yamekuwa maovu kabisa. Baadhi ya maamuzi mabaya ya wanadamu yamesababisha misiba. Hata hivyo, Mungu hajawahi kamwe kuingilia haki yetu ya kufanya maamuzi. Akiwa Baba mwenye upendo, Mungu ametupatia Biblia kutusaidia kufanya maamuzi mazuri. Anatuonya pia kuhusu matokeo ya kufanya maamuzi yasiyofaa. Biblia inasema kwamba tutavuna tunalopanda.—Wagalatia 6:7.

Maamuzi ya Mtu Binafsi

Mungu hutueleza waziwazi matakwa yake kuhusu mambo fulani na kutupa mwongozo hususa. Hata hivyo, Biblia haiweki sheria za kutuongoza katika kila kitu tunachofanya maishani. Badala yake, ina kanuni zinazowaruhusu watu kuwa na mapendezi tofauti-tofauti. Kwa mfano, ona kile ambacho Biblia inasema kuhusu tafrija.

Maandiko yanamtaja Yehova kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Neno lake linasema kwamba kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kucheza.” (Mhubiri 3:1, 4) Biblia inatuambia kwamba Mfalme Daudi alicheza muziki ili kuwaburudisha wengine. (1 Samweli 16:16-18, 23) Yesu alihudhuria arusi, na hata akabadilisha maji kuwa divai.—Yohana 2:1-10.

Hata hivyo, Biblia inatoa onyo hili linalofaa: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) “Kufanya mzaha wenye aibu” na mambo yasiyo ya adili humchukiza Mungu na yanaweza kuharibu uhusiano wetu naye. (Waefeso 5:3-5) Matatizo makubwa yanaweza kutokea ikiwa hakuna mtu wa kudhibiti unywaji wa pombe kwenye sherehe. (Mithali 23:29-35; Isaya 5:11, 12) Yehova Mungu huchukia jeuri.—Mithali 3:31; Mithali 6:16, 17.

Mistari hiyo inatusaidia tuwe na maoni kama ya Mungu kuhusu tafrija. Wakristo wanapofanya maamuzi, wao huchunguza maoni ya Biblia. Bila shaka, kila mmoja wetu atapata matokeo mazuri au mabaya ya maamuzi anayofanya.—Wagalatia 6:7-10.

Pia, Wakristo wanatiwa moyo kufanya maamuzi ya hekima kupatana na kanuni za Biblia zinazohusu mavazi, ndoa, kulea watoto, na shughuli za kibiashara. Hiyo inatia ndani mambo ambayo hayatajwi waziwazi katika Maandiko. Hata hivyo, kanuni zinazopatikana katika Biblia zinawasaidia kufanya maamuzi kupatana na dhamiri. (Waroma 2:14, 15) Kanuni inayofuata inahusu maamuzi yote yanayofanywa na Wakristo mmoja-mmoja: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

Basi kuhusu habari hiyo, inafaa tuzingatie pia ile kanuni ya ‘kushughulika na mambo yetu wenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Wakristo wanaweza kuchagua mambo tofauti-tofauti ambayo hayapingani na mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, maamuzi ya Mkristo mmoja yanaweza kutofautiana na maamuzi ya Mkristo mwingine. Mungu hapendi kuwaona watumishi wake wakihukumiana. (Yakobo 4:11, 12) Biblia inatoa ushauri huu wenye hekima: “Acheni mmoja wenu asiteseke . . . akiwa mjishughulishaji katika mambo ya watu wengine.”—1 Petro 4:15.

Uamuzi wa Kumtumikia Mungu

Biblia inakazia faida za kumtii Mungu. Hata hivyo, Mungu hawalazimishi watu wamwabudu. Badala yake, anawaalika wanadamu aliowaumba, wawe waabudu wake. Kwa mfano, Biblia inasema hivi: “Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za BWANA aliyetuumba.”—Zaburi 95:6.

Waisraeli wa kale walipewa mwaliko kama huo. Zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, wakati taifa la Israeli lenye mamilioni ya watu liliposimama mbele ya Mlima Sinai, Mungu alianzisha ibada ya kweli iliyotegemea Sheria ya Musa. Walipaswa kuamua ikiwa watamtumikia Mungu au la. Waliamuaje? Wote walisema hivi kwa umoja: “Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda, [“tuko tayari kuyatenda,” NW] nasi tutatii.” (Kutoka 24:7) Wao wenyewe ndio walioamua kumwabudu Yehova.

Katika karne ya kwanza, Yesu alianzisha kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:17; 24:14) Hakumlazimisha mtu yeyote kufanya kazi hiyo. Badala yake, aliwaalika watu kwa fadhili, akisema: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ (Marko 2:14; 10:21) Wengi walikubali mwaliko huo na wakaanza kuhubiri pamoja naye. (Luka 10:1-9) Baada ya muda, watu kadhaa waliamua kuacha kuwa wanafunzi wa Yesu. Yudasi aliamua kumsaliti. (Yohana 6:66; Matendo 1:25) Baadaye, watu wengi walifuata mwelekezo wa mitume na wakawa wanafunzi, si kwa sababu walitishwa kuuawa bali kwa hiari yao. Walikuwa na “mwelekeo ufaao” na hivyo “wakawa waamini.” (Matendo 13:48; 17:34) Leo pia, Wakristo wa kweli hutii Neno la Mungu na kufuata mafundisho ya Yesu kwa hiari.

Ni wazi kwamba Mungu anataka tutumie uwezo wetu wa kuchagua. Yeye pia hutoa mwongozo katika Biblia unaotusaidia kufanya maamuzi ya hekima. (Zaburi 25:12) Kila Mkristo anapaswa kuchunguza kanuni za Mungu kwa makini anapofanya maamuzi. Tukifanya hivyo, tutakuwa tunamtolea Mungu ‘utumishi mtakatifu tukitumia nguvu zetu za kufikiri kuzuri.’—Waroma 12:1.