Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zawadi Zinazotufanya Tuwe Viumbe wa Kipekee

Zawadi Zinazotufanya Tuwe Viumbe wa Kipekee

Zawadi Zinazotufanya Tuwe Viumbe wa Kipekee

‘Wanasayansi huchunguza viumbe kwa sababu wanapendezwa nao, na wanapendezwa nao kwa sababu wanavutia.’—JULES-HENRI POINCARÉ, MWANASAYANSI MFARANSA ALIYE PIA MTAALAMU WA HESABU (1854-1912).

POINCARÉ alipendezwa sana na umaridadi wa viumbe na hasa ule utaratibu na upatano “wa hali ya juu” ambao huwavutia wanasayansi. Lakini si wanasayansi tu wanaofurahia umaridadi na upatano unaotuzunguka. Karibu miaka 3,000 iliyopita, mtunga-zaburi Daudi alivutiwa sana na uumbaji, hasa jinsi ambavyo mwanadamu ameumbwa. Alisali hivi: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.”—Zaburi 139:14.

Ni wanadamu pekee wanaoweza kuchochewa kumtukuza Mungu jinsi hiyo. Hata mnyama mwenye akili nyingi zaidi hawezi kufanya hivyo. Lakini, hatupendezwi tu na yale tunayoona katika uumbaji. Tangu zamani, watu wenye kufikiri wameuliza hivi: Viumbe hao wa ajabu walitoka wapi? Kwa nini waliumbwa? Kusudi letu maishani ni nini? Hatuwezi kujibu maswali hayo kwa kutumia sayansi au kwa kufuata maoni yetu. Lakini Biblia, ambayo imeandikwa kwa uongozi wa Mungu, inatoa majibu yenye kuridhisha kwelikweli.—2 Petro 1:20, 21.

Kitabu hicho kitakatifu cha kale kinasema kwamba tuna sifa za kipekee kwa sababu tuliumbwa “kwa mfano wa Mungu,” yaani, tunaweza kuiga (ingawaje kwa kadiri fulani) sifa za Muumba wetu. (Mwanzo 1:27) Kwa hiyo, ingawa hatuna macho kama ya tai, tunaweza kutumia hekima kufanya maamuzi mazuri kuhusu wakati ujao. Huenda uwezo wetu wa kusikia ukawa duni sana ukilinganishwa na ule wa popo, lakini sisi hupendezwa na mazungumzo, muziki, na sauti tamu za viumbe. Na ingawa hatuna dira mwilini mwetu, tunaweza kupata mwelekezo bora maishani kwa kuchunguza Neno la Mungu, Biblia Takatifu.—Mithali 3:5, 6.

Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, ni sisi tu tulio na uhitaji wa kiroho. Yesu alisema hivi: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Je, wewe hujilisha matamko hayo yenye kuburudisha kwa kusoma Biblia kwa ukawaida?

Tukisitawisha sifa za kiroho kwa kutumia Neno la Mungu, tunaweza kufahamu mambo mengi zaidi ya yale ambayo hisi zetu zinatuwezesha kutambua. Kwa njia gani? Sifa hizo hujenga imani yetu. Tukiwa na imani thabiti inayotegemea Biblia, tunaweza “kumwona” Mungu asiyeonekana, kama alivyofanya Musa. Pia tunaweza kujua yale ambayo Mungu anakusudia kufanya wakati ujao.—Waebrania 11:1, 27.

Wakati Ujao Mzuri kwa Wale “Wanaomwona” Mungu

Biblia inasema kwamba Muumba, Yehova Mungu, anaipenda dunia na viumbe wote waliomo, na hasa wanadamu wenye kumhofu. Kwa hiyo, ameahidi kuwaharibu waovu wote, kutia ndani wale “wanaoiangamiza dunia” kwa pupa. (Ufunuo 11:18; Zaburi 37:10, 11; 2 Wathesalonike 1:8) Kisha, atawapa wale wanaompenda na kumtii uhai wa milele. Isitoshe, watu hao watasaidia kuigeuza dunia yote iwe paradiso yenye viumbe wengi. Hilo ni taraja lililoje!—Luka 23:43.

Hebu wazia mambo utakayoweza kufanya na kuvumbua utakapoishi milele ukiwa na afya bora! Mwanasayansi mmoja aliandika hivi: “Dunia itaendelea kuwa na viumbe wa aina mbalimbali, walio maridadi na wenye kustaajabisha.” Biblia inasema hivi: “Kila kitu [Mungu] amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.”—Mhubiri 3:11.

Unawezaje kuwa miongoni mwa wale watakaoishi katika Paradiso inayotajwa katika Biblia? Kwa kujifunza kuhusu kusudi la Mungu sasa na kutenda kupatana na yale unayojifunza. Yesu alisema hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tumia hisi zako kumthamini Muumba wako zaidi

[Picha katika ukurasa wa 11]

Unaweza kumjua Muumba wako vizuri zaidi kwa kusoma Biblia