Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Mwisho wa Juma!

Furahia Mwisho wa Juma!

Furahia Mwisho wa Juma!

KARIBU kila mtu hutazamia wakati huo, na ufikapo huwa wakati muhimu katika juma. Watu wengine husafiri wakati huo, wengine hucheza, wengine huabudu, na wengine hukaa nyumbani na kulala.

Tunazungumzia mwisho wa juma. Huko Amerika na Ulaya, mwisho wa juma huanza Ijumaa na kuendelea hadi Jumapili. Lakini wazo hilo la mwisho wa juma lilianzia wapi? Iwapo unaishi mahali ambapo watu hufanya kazi kwa siku tano kila juma, unawezaje kutumia mwisho wa juma vizuri?

Mwanzoni Ilikuwa Siku ya Kustarehe

Sheria za Sabato ambazo taifa la Israeli lilipewa miaka karibu 3,500 iliyopita zilisema hivi: “Kazi itafanywa siku sita; lakini siku ya saba ni Sabato ya kustarehe kabisa, takatifu kwa BWANA; kila mtu atakayefanya kazi yo yote katika siku ya Sabato, hakika yake atauawa.” (Kutoka 31:15) Sabato pia ilikuwa siku ambayo wazazi Waisraeli walishughulikia mahitaji ya kiroho ya familia zao.

Sabato ya Kiyahudi ilianza Ijumaa baada ya jua kushuka hadi Jumamosi baada ya jua kushuka. Hata hivyo, kitabu The World Book Encyclopedia kinasema kwamba watu waliodai kuwa Wakristo “waliifanya Jumapili kuwa siku maalumu ya kuabudu, kwa sababu waliamini Yesu alifufuka siku hiyo. Kufikia karne ya nne W.K., kanisa na serikali ziliikubali rasmi kuwa siku ya kustarehe huko Ulaya.”

Ni hivi majuzi tu ambapo muda wa kustarehe uliongezwa kuwa zaidi ya siku moja. Jambo hilo lilianzia Uingereza katika miaka ya 1870, wakati ambapo saa za kazi zilimalizika Jumamosi mchana. Jumamosi alasiri na Jumapili ulikuwa wakati wa mwisho wa juma. Jumamosi alasiri washiriki wa familia walikula pamoja na baadaye, kulingana na gazeti Atlantic Monthly, “walienda kuoga kupatana na desturi yao ya kila juma katika bafu la umma.”

Huko Marekani, mwisho wa juma uliongezwa hata zaidi na kuwa siku mbili za kutoenda kazini. Kulingana na gazeti moja, mnamo mwaka wa 1908, kampuni moja huko New England ilianzisha mpango wa kufanya kazi kwa siku tano kwa juma. Mpango huo ulikubaliwa na wafanyakazi Wayahudi na “Wakristo,” kwa sababu kila kikundi kilikuwa na siku moja ya kustarehe—Jumamosi kwa Wayahudi na Jumapili kwa “Wakristo.” Watu wengi waliupenda mpango huo wa kufanya kazi siku tano kwa juma. Mtengenezaji wa magari Henry Ford aliuunga mkono kwa kuwa aliona ungewachochea watu wengi wanunue magari ya kwenda tafrija za familia wakati wa mwisho wa juma.

Umepanga Kufanya Nini Mwisho wa Juma?

Mwisho wa juma wenye siku mbili umekuwa jambo la kawaida leo katika Ulaya na Amerika. Kwa hiyo, ikiwa unaishi katika maeneo hayo, si ajabu kuulizwa na wafanyakazi wenzako swali hili juma linapokaribia kumalizika: “Umepanga kufanya nini mwisho wa juma?” Swali hilo humfanya mtu afikirie mambo mengi ya kusisimua.

Kwa kuwa umekuwa ukifanya kazi ya mwajiri wako juma zima, mwisho wa juma hukupatia nafasi ya kufanya mambo unayotaka. Unaweza kutumia wakati huo kufanya mambo mengine tofauti na yale ambayo wewe hufanya kila siku. Unaweza kupata pumziko unalohitaji au kuwa pamoja na wapendwa wako. Au huenda ukatembelea madukani, jambo ambalo wengi hupenda kufanya. Brigitte anayeishi Ujerumani asema: “Mimi hufurahia sana kutembelea madukani.”

Uchunguzi unaonyesha kwamba watu wengi wanapenda kupumzika wakati hawaendi kazini. Watu wanaopendelea kukaa nyumbani wakati wa mwisho wa juma wanaweza kufanya mambo mengi mbalimbali: kutunza maua, kukusanya stempu, kusikiliza muziki, kutazama video, kupika, kuandika barua, kusoma, kushona, kucheza, kuchora, na kadhalika. Wengine wanapenda kufanya mambo ambayo huwaruhusu kuwa pamoja na watoto na wenzi wao wa ndoa, kama vile kucheza. *

Je, Biblia inakataza kutumia wakati kufanya mambo yanayoonekana kuwa si ya muhimu sana? La. Solomoni aliandika hivi: “Heri konzi moja [“la pumziko,” NW] pamoja na utulivu, kuliko konzi mbili [“za kazi ngumu,” NW] pamoja na taabu; na kujilisha upepo.” (Mhubiri 4:6) Mambo kama vile kucheza, kupumzika, na kustarehe ni muhimu katika maisha ya Mkristo maadamu yanafanywa kwa usawaziko.

Kupita Kiasi

Kwa upande mwingine, hata jambo zuri huenda lisifae au hata likaleta madhara likifanywa kupita kiasi. Kwa mfano mazoezi ya mwili yana faida fulani. (1 Timotheo 4:8) Lakini kuna watu ambao hujishughulisha na michezo kupita kiasi mwishoni mwa juma. Wengine hutumia wakati na pesa nyingi kufanya mazoezi na kununua vifaa vya michezo ili wasishindwe kamwe kwenye michezo.

Watu ambao hawafanyi mazoezi kwa ukawaida wanaweza kupata madhara ya afya wanapolazimisha miili yao kufanya mazoezi kupita kiasi. Gazeti moja linaripoti kuhusu watu wa umri wa makamo “ambao hupenda sana kucheza mwishoni mwa juma” ili kurudia ujana wao, lakini badala yake hujeruhiwa, miguu yao huteguka, huumia na kuchubuka. Wengine hucheza michezo hatari ambayo inaweza kuumiza na hata kuua, ijapokuwa wanadai eti inawasisimua. * Kwa hiyo, shauri la Biblia linalowatia watu moyo wawe na “kiasi” linafaa kabisa. (Tito 2:2) Mazoezi yanapaswa kuburudisha wala si kuchosha au kuhatarisha.

Hivyo watu fulani hupendelea kufanya mazoezi ya kiasi. Kwa mfano, watu wengi sana nchini Ujerumani hupenda kutembea na kukwea milima. Watu wengi huko Ulaya hupenda kutembea huku wakipima wakati wanaotumia. Wao hutembea kupitia njia za mashambani kwa muda uliowekwa. Hiyo ni njia nzuri ya kufanya mazoezi, na wakati huohuo kutazama mandhari yenye kupendeza! Pia ni jambo ambalo familia nzima inaweza kufurahia.

Kupangia Mambo Mengi Mno

Wakati mwingine watu hupangia mambo mengi sana mwishoni mwa juma, na hivyo huwa hawayafurahii. Badala ya kuwa wameburudika juma linalofuata, wao huwa wachovu sana. Kulingana na gazeti la Ujerumani Focus, asilimia 27 ya watu waliohojiwa katika uchunguzi mmoja walisema kuwa wao hujikuta wakifanya mambo haraka-haraka na hivyo kuchoka sana.

Gazeti Time liliandika hivi: “Kupumzika ndio siri ya kupata matokeo mazuri kazini.” Yesu Kristo pia alijua umuhimu wa kupata pumziko na kustarehe. Kwenye Marko 6:31 yeye aliwaambia wanafunzi wake hivi: “‘Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.’ Kwa maana kulikuwa na wengi wakija na kwenda, nao hawakuwa hata na wasaa wa kula mlo.” Kwa hiyo, hata ingawa unapata nafasi ya kufanya mazoezi, kutembelea madukani, na kufanya mambo mengine, bado unaweza kuburudishwa zaidi ukipanga wakati wa kusoma unapostarehe, kupumzika, au kulala. Hata hivyo, kuna jambo jingine ambalo linaweza kukuburudisha hata zaidi mwishoni mwa juma.

Mahitaji ya Kiroho

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Kusudi moja la kustarehe siku ya Sabato lilikuwa kuwaruhusu watu kushughulikia mahitaji yao ya kiroho. Je, miisho ya juma inaweza kutumiwa kwa kusudi hilo leo? Mikutano mingi ya Mashahidi wa Yehova hufanywa Jumamosi au Jumapili. Wao pia hufanya makusanyiko yao mwishoni mwa juma. Mara nyingi, Mashahidi wengi wa Yehova huwatembelea majirani wao nyumba kwa nyumba mwishoni mwa juma ili kuzungumza nao kuhusu Biblia.

Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wana kazi, makao, na familia za kutunza kama watu wengine. Kwa hiyo, wao pamoja na familia zao hupangia jinsi watakavyotumia wakati wao wa ziada. Hata hivyo, wao hutanguliza mambo ya kiroho. Je, hiyo huwachosha? Fikiria mifano ifuatayo.

Kabla hawajawa Mashahidi, wenzi wa ndoa wanaoitwa Jürgen na Doris walitumia mwisho wa juma kufanya mazoezi kwenye ukumbi wa michezo. Melle na Helena waliutumia kutembelea maonyesho ya sanaa. Helmut naye alifurahia kutazama uumbaji. Silvia alitumia mwisho wa juma kucheza dansi. Tangu watu hao wawe Mashahidi wa Yehova, utendaji wao wa mwisho wa juma umebadilika sana.

Jürgen na Doris wanaeleza hivi: “Mambo tuliyofanya wakati ambapo hatukuwa kazini yalitupumzisha, lakini hayakufanya maisha yetu yawe na kusudi. Kwa kuwa sasa tunawasaidia watu wengine wajifunze Biblia, maisha yetu na ya wale tunaofundisha yana kusudi.” Vipi kuhusu Melle na Helena? “Biblia ina mwongozo bora zaidi wa maisha, na kuzungumza na watu kuihusu huleta furaha nyingi.” Kwa nini Helmut ana shangwe nyingi zaidi? Anasema: “Ninajua kwamba Yehova anathamini yale ninayotimiza katika huduma.” Naye Silvia anasema hivi: “Ninapohubiri, mimi hukutana na watu wengi na kuwa na mazungumzo yenye kupendeza pamoja nao, na hayo ni mambo ninayofurahia.”

Tafadhali zungumza na Mashahidi wa Yehova watakapokutembelea. Ukizungumza kifupi na mmoja wao hilo linaweza kukufungulia njia ya kupata kusudi maishani, si mwishoni mwa juma tu bali hata kila siku ya juma!

Haidhuru unapenda kufanya nini unapokuwa na muda wa ziada, fanya mwisho wa juma uwe wenye kujenga na kufurahisha. Iwapo unasema Kichaga, “Chihio misho wo juma.” Ikiwa unazungumza Kilingala, basi, “Natombeli yo poso elamu.” Iwapo unajua Kikuyu, twakutakia “Wikendi njega.” Popote unapoishi na lolote unalofanya furahia mwisho wa juma!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kwa habari zaidi kuhusu hatari za kucheza michezo fulani ya elektroni, ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nicheze Michezo ya Kompyuta au ya Vidio?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 22, 1996 na mfululizo unaosema “Je, Michezo ya Kompyuta Ina Ubaya Wowote?” katika toleo la Desemba 22, 2002.

^ fu. 16 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Michezo ya Kusisimua—Je! Niijasirie?” katika toleo la Julai 8, 1994, na “Kwa Nini Watu Husisimuliwa na Michezo Hatari?” katika toleo la Oktoba 8, 2002.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Ili ufurahie mwisho wa juma ni lazima usawazishe pumziko, tafrija, na mambo ya kiroho