Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kupenda Vitu vya Kimwili?

Inamaanisha Nini Kupenda Vitu vya Kimwili?

Maoni ya Biblia

Inamaanisha Nini Kupenda Vitu vya Kimwili?

WANADAMU wana mwelekeo wa kiasili wa kupenda mambo ya kiroho na uhitaji wa kumwabudu Mungu. Hata hivyo, mwanadamu aliumbwa kutokana na vitu vya kiasili na ana mahitaji ya kimwili na uwezo wa kufurahia vitu vya kimwili. Wakristo fulani wana mali nyingi. Je, hiyo inamaanisha kwamba wanapenda mali na hawathamini mambo ya kiroho? Kwa upande mwingine, je, inamaanisha kwamba wale ambao ni maskini hawawezi kuwa na mwelekeo wa kupenda vitu vya kimwili, lakini wana mwelekeo wa kupenda mambo ya kiroho tu?

Ama kweli utakubali kwamba kupenda vitu vya kimwili kunatia ndani mengi zaidi ya kuwa na mali nyingi. Hebu ona mifano ifuatayo ya Biblia inayoonyesha maana ya kupenda vitu vya kimwili na jinsi kunavyoweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho.

Matajiri na Watu Mashuhuri

Baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu katika nyakati za Biblia walikuwa matajiri na watu mashuhuri. Kwa mfano, Abrahamu “alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu.” (Mwanzo 13:2) Ayubu alikuwa “mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki” kwa kuwa alimiliki mifugo wengi na watumishi wengi sana. (Ayubu 1:3) Wafalme wa Israeli, kama Daudi na Solomoni walikuwa na mali nyingi sana.—1 Mambo ya Nyakati 29:1-5; 2 Mambo ya Nyakati 1:11, 12; Mhubiri 2:4-9.

Kulikuwa na Wakristo matajiri katika karne ya kwanza. (1 Timotheo 6:17) Lidia anatajwa kuwa “muuzaji wa rangi ya zambarau, wa jiji la Thiatira na mwabudu wa Mungu.” (Matendo 16:14) Rangi ya zambarau na mavazi yaliyotiwa rangi hiyo yalitumiwa na watu wenye vyeo au matajiri. Kwa hiyo, yaelekea Lidia alikuwa na mali nyingi.

Kwa upande mwingine, waabudu fulani wa Yehova katika nyakati za Biblia walikuwa maskini hohehahe. Misiba ya kiasili, mikasa, na vifo vya wapendwa wao vilifanya familia nyingine kuwa maskini. (Mhubiri 9:11, 12) Ni lazima wale waliokuwa maskini waliumia sana kuwaona wale wengine wakiwa na mali nyingi! Hata hivyo, ingekuwa kosa kama wangewahukumu matajiri kuwa walipenda vitu vya kimwili au kukata maneno kwamba wale waliokuwa maskini walimtumikia Mungu kikamili zaidi. Kwa nini? Hebu ona kinachomfanya mtu apende vitu vya kimwili.

Kupenda Fedha

Kamusi moja inasema kwamba kupenda vitu vya kimwili ni “kukazia fikira au kujiingiza sana katika vitu vya kimwili badala ya mambo ya kiakili na ya kiroho.” Kwa hiyo, kupenda vitu vya kimwili kunatokana na mambo tunayotamani, tunayotanguliza, na kuzingatia maishani. Jambo hilo linaonyeshwa na mifano miwili ifuatayo ya Biblia.

Baruku, aliyekuwa mwandishi wa nabii Yeremia, alipewa shauri kali na Yehova. Huenda alikuwa maskini kwa sababu ya hali za Yerusalemu na kwa kushirikiana na Yeremia ambaye hakupendwa na watu wengi. Hata hivyo, Yehova alimwambia hivi: “Je, unajitafutia mambo makuu? Usiyatafute.” Huenda Baruku alianza kupenda vitu vya kimwili na kukazia fikira mali au ufanisi wa watu wengine. Yehova alimkumbusha Baruku kwamba Angemwokoa wakati wa uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa unakaribia lakini Hangeokoa mali zake.—Yeremia 45:4, 5.

Yesu alitoa mfano wa mtu aliyekuwa anazingatia sana mambo ya kimwili. Mtu huyo alikaza fikira zake kwenye mali badala ya kuzitumia kuongeza utumishi wake kwa Mungu. Tajiri huyo alisema: “Hakika nitabomoa ghala zangu na kujenga zilizo kubwa zaidi, . . . nami hakika nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi, wewe una vitu vyema vingi vilivyolimbikwa kwa miaka mingi; starehe, kula, kunywa, jifurahishe mwenyewe.’” Kisha Yesu akasema: “Lakini Mungu akamwambia, ‘Wewe mwenye kukosa akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Ni nani, basi, atakayepaswa kuwa na vitu ulivyoviweka akiba?’ Hivyo ndivyo huwa kwa mtu ajilimbikiaye hazina mwenyewe lakini si tajiri kuelekea Mungu.”—Luka 12:16-21.

Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo mawili? Yanatusaidia kutambua kwamba mtu anakuwa mwenye kupenda vitu vya kimwili, si kwa sababu ya mali alizo nazo, bali kwa sababu ya kuziona kuwa muhimu sana. Mtume Paulo alisema: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Matatizo hutokea mtu anapoazimia kuwa tajiri na kupenda vitu vya kimwili.

Tunahitaji Kujichunguza

Wakristo wote, wawe matajiri au maskini, wanapaswa kujihadhari wasinaswe na mtego wa kupenda vitu vya kimwili. Nguvu za mali ni zenye udanganyifu na zinaweza kumwangamiza mtu kiroho. (Mathayo 13:22) Bila kujua, tunaweza kuacha kukazia uangalifu mambo ya kiroho na kuanza kutilia maanani mambo ya kimwili, na hilo linaweza kuleta matokeo yenye kusikitisha.—Mithali 28:20; Mhubiri 5:10.

Kwa hiyo, Wakristo wanapaswa kuchunguza mambo wanayotanguliza maishani. Iwe sisi ni maskini au matajiri, ikiwa tunazingatia mambo ya kiroho, tutajitahidi kufuata shauri la Paulo la kuweka tumaini letu “si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.”—1 Timotheo 6:17-19.