Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

“Wazazi ndio wanaoweza hasa kuwalinda watoto wao wasitumie dawa za kulevya. Wanapaswa kuweka mfano mzuri kwa watoto wao na kuwafundisha.”—DONNA SHALALA, KATIBU WA WIZARA YA AFYA NA HUDUMA ZA JAMII YA MAREKANI.

HIVYO, wewe mzazi ndiwe mwenye daraka la kuwalinda watoto wako dhidi ya dawa za kulevya. Lakini inasikitisha kwamba si wazazi wote wanaotambua kwamba wana daraka muhimu. “Baba alikuwa na shughuli nyakati zote,” asema Ireneu, kijana mmoja Mbrazili. “Alikuwa akizungumza nasi kifupi tu. Hatukupata ushauri wowote kuhusu dawa za kulevya.”

Kwa upande mwingine, fikiria yale ambayo kijana mwingine Mbrazili anayeitwa Alecxandros anakumbuka: “Vipindi vya televisheni vilipoonyesha watumiaji sugu wa dawa za kulevya, babangu aliniita mimi na ndugu zangu sebuleni ili tuwatazame. Alituonyesha jinsi watu hao walivyokuwa katika hali mbaya kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya. Nyakati nyingine alitumia nafasi hiyo kutuuliza iwapo tumewahi kuwaona vijana ambao wanatumia dawa za kulevya shuleni. Kwa njia hiyo, alituonya kuhusu hatari za kutumia dawa za kulevya.”

Je, umezungumza na watoto wako kuhusu hatari za kutumia dawa za kulevya? Ili ufanye hivyo, huenda ukahitaji kufahamu hatari hizo. Wazazi Wakristo wanaweza kuwasaidia watoto wao waelewe kwamba wakitumia dawa za kulevya watahatarisha hali yao ya kiroho. Biblia hutusihi tudumishe miili yetu ikiwa safi kutokana na uchafu wa kimwili na wa kiroho. (2 Wakorintho 7:1) Kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na watoto wako ni njia bora ya kuwalinda. *

“Rafiki wa Karibu”

Ni muhimu pia uwe na uhusiano wa karibu pamoja na watoto wako. Yehova ni “rafiki wa karibu” wa watoto wake walioko duniani. (Yeremia 3:4, NW) Je, wewe ni rafiki wa karibu wa mtoto wako? Je, wewe humsikiliza mtoto wako kwa makini? Je, mtoto wako anaweza kukueleza matatizo yake bila kuogopa? Je, wewe humchambua-chambua bila kumpongeza? Tenga wakati ili umjue mtoto wako vizuri. Je, ana marafiki? Je, unawajua? Biblia inaonya hivi: “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Usiogope kuweka sheria thabiti au kutoa nidhamu kwa upendo. Biblia inasema: “Mpe nidhamu mwanao naye hatakupa wasiwasi; yeye ataufurahisha moyo wako.”—Mithali 29:17, Biblia Habari Njema.

Zaidi ya hayo, usipuuze hatari ambazo zinamkabili mtoto wako. Huenda wazazi wengine wakafikiri kwamba kwa kuwa watoto wao wanaishi katika familia inayoheshimiwa basi hawatajiingiza katika dawa za kulevya. Lakini, Dakt. José Henrique Silveira anaeleza hivi: “Muuzaji wa dawa za kulevya hutaka kuwa rafiki ya watoto wa watu wanaoheshimiwa kwa kuwa anajua kwamba atapata faida kubwa.” Naam, kijana anayeheshimika akianza kutumia dawa za kulevya, mara nyingi vijana wengine humwiga.

Kwa hiyo, ona mambo kwa njia inayofaa. Jitahidi kufahamu dalili za mwanzo-mwanzo za kutumia dawa za kulevya. Kwa mfano, je, mtoto wako ameanza kujitenga, kushuka moyo, kuwa mkatili, au asiyetaka kukubali maoni ya wengine? Je, amejitenga na marafiki wake wa zamani au washiriki wa familia bila sababu? Ikiwa ndivyo, huenda una sababu ya kuhangaika.

Kwa kusikitisha, licha ya wazazi kufanya jitihada nyingi, vijana wengine huanza kutumia dawa za kulevya baada ya kuchochewa sana na vijana wenzao. Unapaswa kufanya nini mtoto wako akitumbukia katika hali hiyo?

Namna Gani Kijana Wako Akitumia Dawa za Kulevya?

Ireneu anasema hivi: “Miezi kadhaa ilipita kabla ya wazazi wangu kugundua kwamba ndugu yangu anatumia dawa za kulevya. Kwanza walishikwa na wasiwasi kwa sababu hawakufikiri kwamba hata mtoto wao mmoja angekuwa mtumiaji sugu wa dawa za kulevya. Babangu alidhani kwamba njia bora ya kushughulikia jambo hilo ni kumwadhibu ndugu yangu vikali.”

Mzazi anapogundua kwamba mtoto wake anatumia dawa za kulevya, huenda kwanza akakasirika, akakata tamaa, na kuhisi kwamba ameshindwa kutimiza daraka lake. Hata hivyo, hati moja iliyochapishwa na Wizara ya Elimu ya Marekani inashauri hivi: “Usiwe na wasiwasi! Usijilaumu. Jambo muhimu zaidi wakati huo ni kutulia [na] kufahamu kinachoendelea. . . . Matumizi ya dawa za kulevya yanaweza kuzuiwa. Mtumiaji sugu wa dawa za kulevya anaweza kutibiwa.”

Naam, uwe mwenye fadhili na thabiti ili hali isiwe mbaya zaidi. Ukikasirika kupita kiasi au kukata tamaa huenda mtoto wako asifaulu kuacha zoea hilo. Pia, ungependa mtoto wako awe mtu mzima mwenye kuwajibika ambaye anaweza kujifanyia maamuzi. Kwa hiyo, tenga wakati wa kutosha ili uongee waziwazi na kijana wako na kumsaidia aone faida za kuacha kutumia dawa za kulevya. Jaribu kujua mawazo ya mtoto wako mpotovu, na uwe tayari kumsikiliza.—Mithali 20:5.

Ireneu anasema hivi pia: “Baadaye, wazazi wangu walishughulikia hali hiyo kwa njia tofauti na wakaanza kumshauri ndugu yangu, wakamwekea sheria kuhusu mahali alipoenda, na wakabadili saa za masomo yake ili asikutane na wanashule walewale kila siku. Walianza kumsaidia awe na marafiki wanaofaa na wakamhangaikia yeye na vilevile sisi wengine katika familia.”

Hebu ona jinsi wazazi wengine walivyofanikiwa kukomesha tatizo hilo walipogundua kwamba watoto wao wanatumia dawa za kulevya.

Wazazi Waliofanikiwa Kukomesha Tatizo Hilo

“Hilo ndilo tatizo baya zaidi ambalo tumewahi kukumbwa nalo,” asema mwanamume mmoja anayeitwa Marcelo, anayeishi huko São Paulo, Brazili. “Mimi na mke wangu hatukuwa tumegundua kwamba mwenendo wa wana wetu wawili umebadilika. Mara kwa mara, walienda kula kwenye mikahawa pamoja na vijana wengine ambao tulidhani tunawajua vizuri. Tulivunjika moyo sana rafiki yetu alipotuambia kwamba wavulana wetu wawili wanavuta bangi. Hata hivyo, tulipowauliza, walikubali jambo hilo mara moja.”

Marcelo alishughulikaje na wanawe? “Mimi na mke wangu hatungeweza kuficha hisia zetu,” yeye asema. “Lakini, ijapokuwa tulishutumu zoea lao la kutumia dawa za kulevya, hatukuwaona kuwa watu wasiofaa kitu. Tuliazimia kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea tutawasaidia wana wetu kuacha kutumia dawa za kulevya. Tuliongea nao waziwazi kuhusu nia yetu, na wote wawili walikubali masharti tuliyowawekea. Walipaswa kwenda shuleni kama kawaida na vilevile kufanya kazi. Hatukuwaruhusu tena waende kwenye tafrija peke yao. Kila siku tulionyesha kwamba tunawapenda, bali si wakati wa pindi za pekee tu. Kwa kuwa mimi ni mjenzi, nilienda kufanya kazi pamoja nao mara nyingi. Tulifurahia kuwa pamoja, tukatumia wakati mwingi zaidi kuzungumzia mambo ya wakati ujao na kuwaambia kwamba wanapaswa kuweka miradi inayofaa.” Hivyo, Marcelo na mke wake walifanikiwa kuwasaidia wana wao waache kutumia dawa za kulevya.

Fikiria pia kisa cha baba mwingine Mbrazili. Mwanaye, Roberto, akumbuka: “Babangu alipogundua kwamba ndugu yangu alikuwa anatumia dawa za kulevya, yeye hakumchambua vikali au kumtia nidhamu, badala yake alimtendea kwa urafiki naye alimsaidia kujieleza waziwazi. Alijitahidi kuwajua marafiki wa ndugu yangu na mahali ambapo walipenda kwenda, na akamsaidia ndugu yangu kuelewa kwamba hakuna haja ya kutumia dawa za kulevya wala kushirikiana na marafiki wa aina hiyo. Baba alimwambia kwamba hataki kamwe kujinyima usingizi akimtafuta.” Mama yake wa kambo alimuunga mkono baba yake alipokuwa akimsaidia kijana huyo mwenye matatizo. Wote wawili walikubaliana kwamba walipaswa kuchukua hatua mara moja na kumsaidia kuacha tatizo hilo akiwa nyumbani.—Ona sanduku “Kutafuta Msaada.”

Usikate Tamaa!

Kulea watoto katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo’ kwaweza kuwa jambo gumu na lenye kuchosha. (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, usipuuze kamwe mahitaji yako ya kihisia na ya kiroho. (Mathayo 5:3) Maneno haya ya Mithali 24:10 ni ya kweli kabisa: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Unaweza kupata nguvu nyingi kwa kushirikiana na Wakristo wa kweli. Unapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, unaweza kutegemezwa na kutiwa moyo.—Waebrania 10:24, 25.

Ama kweli, njia bora ya kulinda familia yako kutokana na dawa za kulevya ni kuwafundisha kuwa na imani katika Mungu. Ni wazi kwamba Mungu hawachagulii vijana njia watakayofuata maishani. Lakini anawapa mashauri mazuri. Kulingana na Zaburi 32:8, Mungu anasema hivi: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.” Mungu ni Baba wa kimbingu mwenye upendo anayetaka kuwalinda vijana wasipatwe na madhara ya kihisia, ya kimwili, na ya kiroho. (Mithali 2:10-12) Uwe na hakika kwamba Mungu pia atawasaidia na kuwaunga mkono wazazi wanaotaka sana kuwalea watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4.

Hata hivyo, nyakati nyingine mtu anapowalea watoto katika ulimwengu wa leo anaweza kuhisi amelemewa sana. Je, kuna matumaini yoyote ya kupata msaada?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Mashahidi wa Yehova wamechapisha habari zinazoweza kuwasaidia wazazi kuzungumzia hatari za dawa za kulevya pamoja na watoto wao. Kwa mfano, ona sura ya 33 na 34 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Matumizi ya dawa za kulevya yanaweza kuzuiwa. Mtumiaji sugu wa dawa za kulevya anaweza kutibiwa.”—WIZARA YA ELIMU YA MAREKANI

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Kutafuta Msaada

Huenda wazazi fulani wakaamua kwamba watoto wao wamwone daktari ili wasaidiwe kuacha kutumia dawa za kulevya. Wazazi wanapaswa kujifanyia uamuzi kuhusu matibabu wanayotaka. Hata hivyo, kwa kuwa kliniki tofauti-tofauti hutoa utunzaji kwa viwango mbalimbali, inafaa wazazi wachunguze mambo kinaganaga kabla ya kuchagua matibabu fulani. Kulingana na mtaalamu wa magonjwa ya akili anayeitwa Arthur Guerra de Andrade, ambaye ni profesa kwenye Chuo Kikuu cha São Paulo huko Brazili, ni asilimia 30 tu ya watu wanaotibiwa kwenye kliniki ndio huacha kuwa watumiaji sugu wa dawa za kulevya. Kwa hiyo, wazazi wanapaswa kuhangaikia sana maendeleo ya watoto wao, hata ikiwa madaktari wanahusishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Msaada kwa Wale Wanaojaribu Kuacha Kutumia Dawa za Kulevya

Je, wewe ni kijana ambaye anajaribu kuacha kutumia dawa za kulevya? Ikiwa ndivyo, utaona kwamba kusoma Biblia na kutumia yale unayosoma kwaweza kukusaidia unapojitahidi kuacha zoea hilo. Unaweza kufaidika sana kwa kusoma kitabu cha Zaburi kwa kuwa kinazungumzia maumivu makali ya moyoni ambayo huenda ukawa nayo sasa. Unaweza kupata msaada kwa kusali kwa Mungu kwa unyofu na kumweleza waziwazi hisia zako za ndani. (Wafilipi 4:6, 7) Utaanza kutambua kwamba anakujali sana na kwamba anataka ufanikiwe. Lakini, kwa kuwa Mungu hamlazimishi mtu kufanya jambo lolote, ni muhimu wewe mwenyewe uazimie kuacha kutumia dawa za kulevya. Mtunga-zaburi Daudi, aliyetegemezwa na Mungu mara nyingi, alisema hivi: “Nalimngoja BWANA kwa saburi, akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, toka udongo wa utelezi; akaisimamisha miguu yangu mwambani, akaziimarisha hatua zangu.” (Zaburi 40:1, 2) Leo, Mungu anawategemeza kwa njia hiyohiyo wale wanaotaka kurekebisha maisha yao na kumtumikia.

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Babangu alituonya kuhusu hatari za kutumia dawa za kulevya”—Alecxandros

[Picha katika ukurasa wa 8]

Tenga wakati ili kuwaonya watoto wako kuhusu hatari za kimwili na za kiroho za kutumia dawa za kulevya

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wajue marafiki wa watoto wako

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ukishughulikia hali ngumu kwa utulivu unaweza kuzuia mambo yasiwe mabaya zaidi