Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Nywele Nilithamini sana makala yenye kichwa “Je, Nywele Zako Zinakuhangaisha?” (Agosti 8, 2002) Nimekuwa nikifanya kazi ya kutengeneza nywele kwa miaka 14. Sisi hufanya tu kama vile mlivyodokeza kuhusu kuchana nywele zinazoanguka. Mimi hufurahi sana kuona jinsi mnavyoandika kwa ustadi.

K. K., Japan

Mimi ni mpenzi wa Amkeni!, na ninataka kuwashukuru kwa makala hiyo. Nywele zangu zilianza kuota mvi nilipobalehe. Nilipokaribia umri wa miaka 20, mtu angeweza kuona mvi zangu hata akiwa mbali. Jambo hilo lilinihangaisha sana. Makala hiyo ilinisaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu sura yangu huku nikijitahidi kusitawisha sifa za kiroho.

E. J., Nigeria

Upendo Unaopumbaza Asanteni kwa sehemu inayosema kuhusu “Upendo Unaopumbaza” katika makala “Kuutazama Ulimwengu.” (Agosti 8, 2002) Makala hiyo ilinisaidia kutambua kwamba hata upendo wa kupumbaza ukidumu kwa muda fulani, huo si msingi imara wa ndoa yenye furaha. Mashauri kama hayo yanaweza kumsaidia mtu aepuke kufanya mambo ya kipumbavu!

P. L., Urusi

Karamu ya Luau Nilifurahia kusoma makala yenu yenye kichwa “Twende Kwenye Karamu Nchini Hawaii.” (Juni 8, 2002) Miaka michache iliyopita nilihudhuria karamu nchini Hawaii. Nilihisi kwamba karamu hiyo ilikuwa na mambo ya kidini na ushirikina. Hata ingawa siku hizi karamu hizo hazihusishi mambo ya kidini au ya ushirikina, je, kweli zinatofautiana na sherehe nyingine zenye asili ya kipagani ambazo zinaonwa kuwa pindi za furaha katika tamaduni nyingi za kisasa?

L. F., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Kama vile kielezi cha chini kwenye ukurasa wa 24 kinavyosema, inawezekana kwamba hapo zamani karamu ya “luau” ilihusiana na dini ya uwongo, lakini siku hizi neno hilo linamaanisha tu karamu inayofanywa nchini Hawaii. Karamu yoyote inayoitwa “luau” huenda ikawafaa au isiwafae Wakristo. Kama ilivyo katika mambo mengine, Wakristo wanapaswa kufanya uamuzi ambao utawawezesha kubaki wakiwa na dhamiri njema mbele za Yehova Mungu.—1 Timotheo 1:5, 19; ona pia gazeti la Amkeni!” la Januari 8, 2000, ukurasa 26-27.

Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua.” (Julai 22, 2002) Ninahisi kwamba makala hiyo iliandikwa kwa ajili yangu. Ingawa sina tatizo hilo, mimi na mume wangu hatuna watoto na nimekuwa nikipambana na mshuko wa moyo na mfadhaiko kwa mwaka mmoja na nusu. Kila wakati nilijihisi mchovu na kuchanganyikiwa, na nilikuwa nikishindwa kuamua hata mambo madogo. Niliogopa kuwa karibu na watu. Hata singeweza kuenda dukani bila kuandamana na mume wangu. Nimeanza kupata nafuu, na ninaendelea kutumia dawa. Makala hiyo imenionyesha kwamba ninaweza kufanya mengi zaidi. Mume wangu amesoma makala hiyo pia, na ameona jinsi anavyoweza kunisaidia.

J. R., Marekani

Ninashukuru sana kwa makala iliyohusu kushuka moyo baada ya kujifungua! Baada ya kujifungua mtoto wangu wa tatu madaktari waliniambia kwamba nilikuwa nimeshuka moyo sana. Kabla ya wakati huo, nilidhani ningerukwa na akili. Ulikuwa wakati mgumu sana kwangu na kwa familia yangu. Nimekuwa nikitumia mitishamba na vitamini na kufanya mazoezi kwa ukawaida, na hilo limenisaidia sana kukabiliana na hali hiyo. Tafadhali mshukuruni Janelle kwa kutueleza yaliyompata.

J. C., Marekani