Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Usio na Dawa za Kulevya Hivi Karibuni

Ulimwengu Usio na Dawa za Kulevya Hivi Karibuni

Ulimwengu Usio na Dawa za Kulevya Hivi Karibuni

Je, unaweza kuwazia ulimwengu usio na dawa za kulevya?

KATIBU-MKUU wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan aliyaomba mataifa yote yajitahidi kufanyiza ulimwengu kama huo. Alitangaza hivi: “Ni lazima tuchukue hatua mpya na madhubuti kuangamiza uovu huo; tatizo ambalo limewanasa watoto wetu wengi sana.”

Ingawa huenda viongozi wakakubali kupunguza utengenezaji na uuzaji wa dawa haramu ulimwenguni pote, hiyo ni kazi ngumu sana. Hennadiy Udovenko kutoka Ukraine, alisema hivi alipokuwa rais wa kikao cha pekee cha Baraza Kuu la UM: “Magendo ya dawa za kulevya ni mojawapo ya biashara za kichinichini zenye faida kubwa sana kwani inakadiriwa kwamba yanaleta faida ya dola zaidi ya bilioni 400 za Marekani kila mwaka, . . . na yanaweza kuharibu au kuangusha biashara nyingine duniani.” Aliongeza kusema kwamba tatizo la dawa za kulevya “linakumba ulimwengu mzima na hakuna taifa lisiloathiriwa nalo.”

Ni vigumu kuwazia ulimwengu usio na dawa za kulevya. Ni wazi kwamba serikali za wanadamu zimeshindwa kuzikomesha. Hata hivyo, hakuna mtu awaye yote anayeweza kumzuia Mungu Mweza-Yote asitimize kusudi lake la kuifanya dunia kuwa paradiso ambako mahitaji yote ya kihisia, ya kimwili, na ya kiroho yatatoshelezwa. (Zaburi 145:16; Luka 23:43; 2 Petro 3:13) Kama vile nabii Isaya asemavyo, Neno la Mungu ‘halitamrudia bure, bali litatimiza mapenzi yake, nalo litafanikiwa katika mambo yale aliyolituma.’—Isaya 55:11.

Tunaweza kufaidika sana hata sasa tunapotumaini ahadi hizo. Kwa mfano, mtu mmoja anayeitwa Edmundo alikuwa mtumiaji wa dawa za kulevya. Lakini alipokubali ahadi ya Biblia kuhusu ulimwengu mpya wenye uadilifu alianza kujichunguza. Sasa Edmundo anasema hivi: “Nilifanya upumbavu kwa kupoteza wakati wangu.” Kwa kuwa anataka kuendelea kupata kibali cha Mungu, Edmundo ameazimia kutotumia dawa za kulevya kamwe. Naam, ujuzi kumhusu Mungu na ahadi zake unapaswa kutuchochea ‘kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’—Waefeso 4:24.

Wengine wengi ambao walikuwa watumiaji wa dawa za kulevya hapo zamani wanafurahia uhusiano wa karibu pamoja na Muumba wao sasa. Maneno haya ya mtunga-zaburi yanawatia moyo sana: “Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, wala maasi yangu. Unikumbuke kwa kadiri ya fadhili zako, Ee BWANA kwa ajili ya wema wako. BWANA yu mwema, mwenye adili, kwa hiyo atawafundisha wenye dhambi njia.” (Zaburi 25:7, 8) Wazazi walio na watoto wakaidi wanaweza kufarijiwa sana kujua kwamba watoto wao wanaweza kubadilika. Wazazi wakijitahidi sana, wanaweza kuwasaidia watoto wao kupambana na tatizo la dawa za kulevya na kupata “mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,” ambao utakuwepo katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Timotheo 6:19.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tumaini la kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu limewachochea watu wengi waliotumia dawa za kulevya kubadili maisha yao