Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana na Dawa za Kulevya

Vijana na Dawa za Kulevya

Vijana na Dawa za Kulevya

“Je, walistahili kufa?”

Hilo ndilo swali lililozushwa kwenye jalada la gazeti Veja la Brazili. Jalada hilo lilikuwa na picha za vijana wenye afya na wenye kuvutia ambao walikufa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya.

IJAPOKUWA hatari za kutumia dawa za kulevya zinaonekana wazi, watu huendelea kuzitumia, na jambo hilo huharibu maisha ya watu wengi. Kila mwaka, matumizi ya dawa za kulevya nchini Marekani husababisha hasara ya dola bilioni 100 kupitia matibabu, kupungua kwa utendaji kazini, kupungua kwa mapato, na uhalifu. Lakini vijana hasa—kutia ndani watoto—ndio wanaoathiriwa zaidi. Gazeti Jornal da Tarde liliripoti kuhusu uchunguzi uliofanywa huko Brazili ambao ulionyesha kwamba asilimia 24.7 ya vijana walio kati ya umri wa miaka 10 na 17 tayari wametumia aina moja ya dawa ya kulevya.

Ijapokuwa idadi ya vijana wanaotumia dawa za kulevya imepungua nchini Marekani katika miaka ya hivi karibuni, inashangaza jinsi vijana wengi wamekuwa watumiaji sugu wa dawa za kulevya. Kwa mfano, fikiria kuhusu vijana wanaokaribia kumaliza shule ya sekondari. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 37 kati yao walivuta bangi mwaka uliopita. Asilimia 20 kati yao walivuta bangi mwezi uliopita. Asilimia 10 hivi kati yao walitumia dawa fulani ya kulevya inayosababisha msisimuko mwaka uliopita. Zaidi ya asilimia 6 walitumia dawa ya LSD.

Ripoti kutoka sehemu zote za ulimwengu zinasikitisha. Shirika fulani la takwimu huko Uingereza linaripoti kwamba “asilimia 12 ya wanafunzi wa shule wenye umri wa miaka 11-15 walitumia dawa za kulevya mwaka uliopita . . . Kuna uwezekano mkubwa kwamba walivuta bangi.” Jambo la kuhuzunisha zaidi ni kwamba “zaidi ya thuluthi moja kati yao (asilimia 35) walikuwa wamepewa dawa moja au zaidi za kulevya.”

Vilevile, ripoti moja iliyodhaminiwa na Umoja wa Nchi za Ulaya inaonyesha kwamba “siku hizi [vijana] wengi zaidi wanalewa chakari.” Pia, ripoti hiyo inasema kwamba “ulevi unasababisha hatari mbalimbali zinazotokea ghafula kama vile misiba ya barabarani, ujeuri na kunywa sumu, na vilevile unaathiri ukuzi na uwezo wa mtu wa kuchangamana na wengine.” Ripoti moja kutoka Japan inasema kwamba “mara nyingi vijana nchini Japan hunusa gundi na petroli, na hilo linaweza kuwafanya watumie dawa nyingine za kulevya.”

Ndiyo sababu Katibu-Mkuu wa UM, Kofi Annan, alisema hivi: “Dawa za kulevya zinaharibu jamii zetu, zinaongeza uhalifu, zinaeneza magonjwa kama UKIMWI, zinawaua vijana wetu na kuharibu matumaini yetu ya wakati ujao.” Mara nyingi, watumiaji wa dawa za kulevya hujiingiza katika uhalifu kama vile ulanguzi wa dawa za kulevya na mauaji. Isitoshe, watu wengi hujiingiza katika ujeuri, huumia, au wanafanya ngono bila kutarajia kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya. Na ikiwa unafikiri familia yako iko salama, basi uwe chonjo! Ripoti moja ya serikali ya Marekani ilisema hivi: “Kutumia dawa za kulevya si tatizo linalowakumba watu maskini tu, watu wachache wa tabaka fulani, au watu wanaoishi katika mitaa ya mabanda pekee. . . . Watu wa matabaka yote hutumia dawa za kulevya. Kila mtu huathiriwa na tatizo la dawa za kulevya.”

Hata hivyo, mara nyingi wazazi hutambua kwamba watoto wao wanaweza kuathiriwa na dawa za kulevya mambo yakiisha kwenda mrama. Fikiria kisa cha msichana mmoja Mbrazili. “Alikuwa akinywa pombe,” asema dadake mkubwa Regina. * “Watu katika familia waliona kuwa jambo hilo ni sawa kabisa. Lakini jambo hilo lilimfanya aanze kutumia dawa za kulevya pamoja na marafiki wake wavulana. Kwa kuwa wazazi wangu hawakuchukua hatua yoyote, aliharibika hata zaidi. Mara kwa mara alitoweka nyumbani. Na kila mara msichana yeyote alipopatikana ameuawa, polisi walimpigia simu babangu ili kumuuliza iwapo huyo alikuwa dadangu! Hilo liliitaabisha familia yetu sana.”

Shirika la Afya Ulimwenguni linaeleza sababu tano ambazo huenda zikawafanya vijana waanze kutumia dawa za kulevya:

(1) Wanataka kujiona kuwa watu wazima na kujifanyia maamuzi

(2) Wanataka kuwa kama marika wao

(3) Wanataka kustarehe na kujihisi vizuri

(4) Wanataka kujihatarisha na kuasi

(5) Wanataka kujua jinsi mtu huhisi anapotumia dawa hizo

Vijana wanaweza kuathiriwa sana iwapo dawa hizo zinapatikana kwa urahisi na wanapochochewa na marafiki wao kuzitumia. Kijana mmoja Mbrazili anayeitwa Luiz Antonio anasema hivi: “Wazazi wangu hawakunieleza lolote kuhusu dawa za kulevya. Walimu shuleni walizungumzia tatizo hilo kijuujuu tu.” Marafiki wake walimchochea kutumia dawa hizo na akaanza kuzitumia alipokuwa na umri wa miaka 14. Baadaye, alipojaribu kuacha kuzitumia, “marafiki” waliokuwa wakimletea dawa hizo walimtisha kwa kisu asithubutu kuacha!

Je, unakubali kwamba watoto wako wanaweza kuwa hatarini? Umefanya nini ili kuwalinda kutokana na dawa za kulevya? Makala inayofuata itazungumzia mambo fulani ambayo wazazi wanaweza kufanya ili kuwalinda watoto wao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Dawa za kulevya zinaharibu jamii zetu, zinaongeza uhalifu, zinaeneza magonjwa kama UKIMWI, zinawaua vijana wetu na kuharibu matumaini yetu ya wakati ujao.”—KOFI ANNAN, KATIBU-MKUU WA UM

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

© Veja, Editora Abril, May 27, 1998