Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Maisha Yangu Yalivyobadilika Nilipojeruhiwa

Jinsi Maisha Yangu Yalivyobadilika Nilipojeruhiwa

Jinsi Maisha Yangu Yalivyobadilika Nilipojeruhiwa

SIMULIZI LA STANLEY OMBEVA

Mnamo mwaka wa 1982, niligongwa na gari lililokuwa linaenda kasi. Nilitibiwa na muda si muda nikarudia shughuli zangu za kila siku, licha ya kupatwa na maumivu mara kwa mara kwa sababu ya gegedu lililoteguka kati ya shingo na kifua changu. Lakini miaka 15 baadaye, nilikumbwa na tukio lililojaribu imani yangu zaidi katika maisha yangu yote.

KABLA na baada ya msiba huo kutokea, nilikuwa mtu mwenye nguvu. Nilikuwa nikifanya mazoezi kwa ukawaida, kama vile kukimbia umbali wa kilometa 10 hadi 13 mwishoni mwa juma, kucheza skwoshi, na kufanya kazi ngumu za mikono. Nilisaidia kujenga Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova na Jumba kubwa la Kusanyiko jijini Nairobi, Kenya, nchini kwetu.

Kisha, mnamo mwaka wa 1997, nilianza kuhisi maumivu makali kifuani mwangu mara kwa mara. Uchunguzi wa kitiba ulionyesha kwamba gegedu lililo katikati ya mgongo wangu lilikuwa limeteguka na lilikuwa linafinya uti wa mgongo. Hiyo ilisababishwa na ule mkasa niliotaja mwanzoni.

Kabla afya yangu haijaanza kudhoofika, nilifanya kazi ya kuuza bidhaa. Kazi hiyo ilinisaidia kuwa na bima ya afya ya familia. Matumaini yangu ya kifedha yalikuwa mazuri. Lakini katikati ya mwaka wa 1998, mwili wangu ulianza kupooza toka kifuani hadi miguuni. Siku baada ya siku, afya yangu ilizidi kuzorota.

Muda si muda, nilipoteza kazi yangu na marupurupu yangu yote. Binti zangu wawili, Sylvia na Wilhelmina, walikuwa na umri wa miaka 13 na 10. Kwa kuwa sikuwa na kazi, tulilazimika kutegemea pato la mke wangu, Joyce. Ilitubidi tupunguze matumizi yetu na tukafaulu kutosheleza mahitaji yetu ya lazima.

Hisia Zisizofaa

Hali ilipozidi kuwa mbaya, nilianza kuwa na hisia zisizofaa, nikawa mbinafsi, na niliudhika upesi. Nyakati nyingine niliudhika na kukasirishwa na mambo madogo-madogo tu. Kila wakati nilikuwa karibu kuvunjika moyo. Kila mmoja katika familia aliathiriwa na hali hiyo ngumu. Mke wangu na binti zetu walikabiliana na hali ambazo hawakuzielewa hata kidogo.

Wakati huo, nilihisi kwamba maoni yangu yalifaa. Uzito wangu uliongezeka sana. Tumbo langu lilichafuka sana na nilikuwa na matatizo ya kuzuia mkojo wangu. Niliona haya mara nyingi. Ilikuwa kawaida kuniona mahali fulani nikiwa peke yangu nikilia machozi. Nyakati nyingine nilikasirika sana. Nilijua sikuwa nikishughulikia hali yangu kwa njia inayofaa.

Nikiwa mzee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, nilikuwa nimewashauri Wakristo wenzangu wasimlaumu Yehova kamwe wanapopatwa na mateso ya aina yoyote. Hata hivyo, nilijiuliza hivi mara nyingi, ‘Mbona Yehova ameruhusu nipatwe na jambo hili?’ Ingawa nilikuwa nimetumia maandiko kama vile 1 Wakorintho 10:13 kuwaimarisha na kuwatia wengine moyo, nilihisi kwamba yale yaliyonipata yalikuwa zaidi ya vile ningeweza kustahimili!

Matatizo ya Kitiba

Haikuwa rahisi kupata matibabu yanayofaa. Ningetumia siku nzima kuwaona madaktari wa maungo na mtaalamu anayetibu kwa kuchoma sindano ya kuamsha mishipa ya fahamu. Nilipata nafuu ya muda tu. Niliwaona madaktari kadhaa, kutia ndani mpasuaji wa mifupa na mpasuaji wa mfumo wa neva. Wote walikubaliana kuhusu jambo moja: Nilihitaji kufanyiwa upasuaji ili kupunguza maumivu niliyokuwa nayo na kuondoa gegedu lililoteguka. Kwa sababu ya imani yangu inayotegemea Biblia, niliwaeleza madaktari hao kwamba singekubali kutiwa damu katika hali yoyote ile.—Matendo 15:28, 29.

Daktari wa kwanza alisema kwamba angefanya upasuaji kupitia mgongoni. Nilielezwa kwamba njia hiyo ya upasuaji ingekuwa hatari sana. Lakini daktari huyo hakunihakikishia kwamba ningepasuliwa bila kutiwa damu. Sikwenda kumwona tena.

Daktari wa pili alisema kwamba angefikia uti wangu wa mgongo kwa kunipasua shingoni. Niliogopa sana. Ingawa alikubali kunipasua bila kunitia damu, alitaka nipasuliwe upesi na akatoa madokezo machache. Sikurudi kumwona.

Hata hivyo, niliweza kupata daktari mwenye kushirikiana kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova katika Halmashauri ya kwetu ya Uhusiano na Hospitali. Utaratibu alioeleza daktari wa tatu ulikuwa sawa na ule uliotolewa na daktari wa pili, yaani kupasua kupitia shingoni. Njia hiyo haikuwa na hatari nyingi.

Niliogopa sana nilipoonyeshwa jinsi ambavyo upasuaji huo ungefanywa. Niliogopa zaidi nilipotambua kwamba upasuaji huo ungefanywa karibu na viungo nyeti kama vile moyo na mapafu. Je, upasuaji huo ungefaulu? Bila shaka hiyo iliongeza tu hofu yangu.

Mnamo Novemba 25, 1998, nilifanyiwa upasuaji uliofaulu ambao ulichukua saa nne katika hospitali moja jijini Nairobi. Upasuaji huo pia ulihusisha kuondoa kipande cha mfupa wa nyonga. Kipande hicho kilichongwa na kuunganishwa na sehemu iliyokuwa imeathiriwa kwa kutumia vipande vya chuma na skurubu. Hiyo ilisaidia, lakini matatizo yangu hayakuisha. Nilitembea kwa shida sana. Bado mimi hupooza mara kwa mara.

Maoni Yanayofaa

Kama nilivyotaja, nilikuwa nimetumia wakati mwingi sana nikijihurumia na kujisikitikia kwa sababu ya hali yangu. Kwa upande mwingine, wafanyakazi wa hospitali walinipongeza kwa kuwa mtulivu na kudumisha maoni yanayofaa. Kwa nini walihisi hivyo? Kwa sababu licha ya kuwa na maumivu makali, niliwaambia kuhusu imani yangu katika Mungu.

Ingawa mara kwa mara niliudhiwa na kukasirishwa na yale yaliyonipata, nilimtegemea Yehova. Daima alinitegemeza sana katika matatizo yangu yote hivi kwamba niliona haya wakati mwingine. Niliazimia kabisa kusoma na kutafakari kuhusu maandiko niliyojua yangenifariji. Baadhi ya maandiko hayo ni:

Ufunuo 21:4: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” Kufikiria baraka zilizo katika Biblia kuhusu ulimwengu mpya ambao hautakuwa na machozi na maumivu kamwe kulinifariji.

Waebrania 6:10: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” Ingawa kimwili nililemewa, nilijua kwamba Yehova alithamini jitihada zangu za kumtumikia.

Yakobo 1:13: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Hiyo ni kweli kabisa! Ingawa Yehova aliruhusu niteseke, yeye hakusababisha mateso yangu.

Wafilipi 4:6, 7: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Sala ilinisaidia kupata amani ya akili niliyohitaji sana, na iliniwezesha nikabiliane vyema zaidi na hali yangu.

Nilikuwa nimetumia maandiko hayo kuwatia moyo wengine waliotaabika, na yaliwasaidia sana! Hata hivyo, nilitambua kwamba sikuwa nimejua thamani yake kikamili. Punde tu nilipokuwa mgonjwa sana, ndipo nilipojifunza kuwa mnyenyekevu na kutambua kwamba nilihitaji kumtegemea Yehova kabisa.

Misaada Mingine Yenye Kutia Nguvu

Wengi husema kwamba udugu wa Kikristo ni nguzo na tegemezo wakati wa magumu. Hata hivyo, ni rahisi sana kuwapuuza ndugu na dada zetu. Kweli, huenda wasiweze kusaidia kwa mambo yote, lakini sikuzote wako tayari kusaidia. Ilikuwa hivyo kwangu. Akina ndugu na dada walinitembelea hospitalini, wakati mwingine asubuhi na mapema. Hata walijitolea kunisaidia kulipia gharama za matibabu. Ninawashukuru kutoka moyoni wote walionihurumia na kunisaidia.

Katika kutaniko letu, Mashahidi wenzangu wanajua kwamba siwezi kufanya mambo fulani. Mimi hutumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi na hufanya kazi pamoja na baraza la wazee wakristo lenye ushirikiano sana. Sijaacha kuwa wa kawaida katika huduma. Nilipokuwa mgonjwa sana, niliwasaidia wawili kuweka maisha zao wakfu kwa Yehova. Mmoja anatumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova la Nairobi.

Sijui nimshukuru vipi mke wangu ambaye amekuwa nami katika majaribu hayo yote. Alivumilia hasira yangu, hisia zangu zilipobadilika-badilika, na wakati niliposononeka. Nilipolia na kuumwa, alinitia moyo na kunifariji. Uvumilivu wake chini ya taabu hunistaajabisha sana. Amekuwa “rafiki wa kweli . . . nyakati zote.”—Mithali 17:17, NW.

Binti zetu wamejifunza kukabiliana na hali zangu. Wao hufanya wawezayo ili kunisaidia. Wanajua mahitaji yangu nao hunisaidia haraka, na kuhakikisha nimestarehe wakati mama yao hayuko. Sylvia amekuwa “mkongojo” wangu, akinisaidia kutembea hapa na pale ndani ya nyumba ninapokuwa dhaifu.

Vipi kuhusu Mina binti yetu mdogo? Nakumbuka wakati fulani ambapo nilianguka na kushindwa kusimama nikiwa nyumbani. Ni sisi wawili tu tuliokuwepo nyumbani. Alijikakamua, akaniinua, na kunipeleka polepole chumbani kwangu. Bado hajui jinsi alivyoweza kufanya jambo hilo. Sitasahau tendo hilo kamwe.

Kukabiliana na jeraha hilo ndilo jambo gumu sana ambalo nimewahi kukabiliana nalo maishani. Ni jambo ambalo bado ninapambana nalo. Hakuna jambo jingine ambalo limetahini imani yangu kama hilo. Nimejifunza kuwa mnyenyekevu, mwenye kuwafikiria wengine, na kuonyesha hisia-mwenzi. Kumtegemea Yehova kabisa kumenisaidia kushinda jaribu hilo.

Nimejifunza ukweli wa maneno haya ya mtume Paulo: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Mimi hupata faraja nyingi kutokana na ahadi ya Mungu ya “mbingu mpya na dunia mpya.” (2 Petro 3:13) Ninasali kwamba Yehova ataendelea kunisaidia hadi niingie dunia hiyo mpya kwa kuwa bado mimi ni dhaifu, na kuna mambo mengi ambayo siwezi kufanya kwa nguvu zangu mwenyewe.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kushiriki utendaji wa Kikristo pamoja na familia yangu hunisaidia kuvumilia