Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumwezesha Mtoto Afurahie Maisha Yake ya Utotoni

Kumwezesha Mtoto Afurahie Maisha Yake ya Utotoni

Kumwezesha Mtoto Afurahie Maisha Yake ya Utotoni

KUFURAHIA maisha ya utotoni hutegemea sana malezi mazuri. Lakini malezi mazuri yanahusisha nini? Huenda umesikia mashauri mbalimbali kuhusu kulea watoto. Tumia wakati pamoja na watoto wako. Wasikilize. Wape mwongozo thabiti. Furahi pamoja nao na usikitike pamoja nao. Uwe rafiki yao wa kweli bila kuachilia madaraka yako ukiwa mzazi. Bila shaka kanuni hizo ambazo hurudiwa-rudiwa zitawasaidia wazazi wawalee watoto wao vizuri. Lakini kuna jambo jingine la msingi na la muhimu zaidi.

Mamilioni ya wazazi ulimwenguni pote wametambua kwamba kufuata kanuni za Biblia ni muhimu ili kutoa malezi bora. Kwa nini? Kwa sababu Mtungaji wa Biblia mwenye hekima, Yehova Mungu, ndiye aliyeanzisha mpango wa familia. (Mwanzo 1:27, 28; 2:18-24; Waefeso 3:15) Kwa hiyo, Neno lililoandikwa kwa uongozi wake linafaa zaidi kutoa mwelekezo wa kulea watoto. Hata hivyo, kitabu cha zamani kama Biblia chawezaje kutoa mwongozo kuhusu mwelekeo wa kisasa wa kuwaharakisha watoto? Acheni tuchunguze kanuni za Kimaandiko zinazohusu jambo hilo.

“Kwa Kadiri ya Mwendo wa Watoto”

Yakobo, mwana wa Isaka, alikuwa baba ya watoto zaidi ya kumi na wawili. Biblia inaeleza maneno yake yenye hekima aliyoyasema wakati familia yake ilipokuwa safarini: “Watoto ni wachanga [dhaifu, NW] . . . Tafadhali Bwana wangu [Esau, ndugu mkubwa wa Yakobo] na apite mbele ya mtumwa wake; nami nitawaongoza polepole . . . kwa kadiri ya mwendo wa watoto.”—Mwanzo 33:13, 14.

Yakobo alijua ya kuwa watoto wake hawangeweza kufanya mambo kama watu wazima. Walikuwa “dhaifu”—wadogo, hafifu, na wenye mahitaji mengi zaidi kuliko watu wazima. Badala ya kuwalazimisha watoto wasafiri kwa mwendo wake, alipatanisha mwendo wake na mwendo wao. Kwa kufanya hivyo, alionyesha hekima ambayo Mungu huwapa watoto wake walio duniani. Baba yetu wa mbinguni anajua kwamba kuna mambo fulani tusiyoweza kutimiza. Yeye hatarajii tufanye mambo ambayo hatuwezi.—Zaburi 103:13, 14.

Hata wanyama fulani wana hekima kama hiyo kwa sababu Mungu aliwaumba na “hekima ya kisilika.” (Mithali 30:24, NW) Kwa mfano, wataalamu wa wanyama wamechunguza tembo na kuona kwamba kundi la tembo hutembea kulingana na mwendo wa tembo mchanga anayetembea katikati ya kundi. Wao huendelea kutembea polepole mpaka tembo huyo mdogo anapojimudu kutembea pamoja nao.

Siku hizi watu wengine hupuuza hekima ya kimungu. Hata hivyo, si lazima uwaige. Kumbuka kwamba watoto wako ni “dhaifu” na hawayawezi matatizo na madaraka ya watu wazima. Kwa mfano, iwapo wewe ni mzazi aliye peke yake na una tatizo kubwa la kibinafsi ambalo unahisi ni lazima umweleze mtoto wako, kinza mwelekeo huo. Badala yake, tafuta msaada wa rafiki mkomavu ambaye anaweza kukusaidia, hasa yule atakayekusaidia kutumia mashauri yenye hekima ya Biblia.—Mithali 17:17.

Vilevile, usimlemee mtoto wako na matatizo chungu nzima, shughuli nyingi sana, au kumbana sana kiasi cha kumfanya asifurahie maisha yake ya utotoni. Mlee mtoto wako kwa kuzingatia uwezo wake, bali si kulingana na ulimwengu wa leo unaosonga mbio. Biblia inashauri hivi kwa hekima: “Usiruhusu ulimwengu unaokuzunguka ukufinyange kulingana na mtindo wake.”—Waroma 12:2, Phillips.

“Kwa Kila Jambo Kuna Majira Yake”

Shauri lingine la hekima la Biblia linasema: “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” Bila shaka kuna wakati wa kufanya kazi pia. Watoto wana kazi nyingi ya kufanya, kutia ndani kazi ya shule, kazi za nyumbani, na mambo ya kiroho. Hata hivyo, kitabu hicho chasema pia kwamba kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kucheza.”—Mhubiri 3:1, 4.

Watoto wana uhitaji wa pekee wa kucheza, kucheka, na kutumia nguvu zao za ujana kwa furaha. Ikiwa wakati wao wote utapangiwa mambo ya shule, shughuli za baada ya shule, na madaraka mengine mazito, basi uhitaji wa kucheza hautatimizwa. Hiyo inaweza kuwafanya wakasirike, au hata washuke moyo.—Wakolosai 3:21.

Ona jinsi unavyoweza kutumia kanuni hiyo kwa njia nyingine. Kwa kuwa kila jambo lina wakati wake, je, hiyo haionyeshi kwamba wakati wa utotoni ni wakati wa kuwa mtoto? Labda utajibu ndiyo, lakini huenda watoto wako wasikubaliane nawe sikuzote. Mara nyingi, wavulana na wasichana wadogo hupenda kuiga yale wanayoona watu wazima wakifanya. Kwa mfano, wasichana wachanga huenda wakashawishiwa kuvalia na kujipamba kana kwamba ni wanawake. Wale wanaobalehe mapema wanaweza kuhisi kwamba wanapaswa kuwa kama watu wazima.

Wazazi wenye hekima hutambua hatari ya mwelekeo huo. Matangazo fulani ya biashara na burudani nyingine katika ulimwengu huu uliopotoka huonyesha kwamba watoto wanafahamu kuhusu ngono na wamekomaa. Watoto wengi zaidi hujipodoa na kuvalia mavazi yanayoonyesha uchi. Mbona tuwafanye watoto wavutie watu ambao wanaweza kuwasumbua kingono? Wazazi wakiwasaidia watoto wao wavalie mavazi yanayofaa umri wao, watakuwa wanatumia kanuni ya Biblia inayosema: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.”—Mithali 27:12.

Mfano mwingine ni huu: Ukiwaruhusu watoto waone michezo kuwa jambo la maana zaidi, hawataishi kwa usawaziko. Hawatatambua kwamba kila jambo lina wakati wake. Biblia inashauri hivi kwa hekima: “Kwa maana mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Timotheo 4:8.

Usiwaruhusu watoto wako wafikiri kwamba “kushinda ndilo jambo muhimu zaidi.” Wazazi wengi huwafanya watoto wasifurahie michezo kwa kuwachochea wawe washindani mno na washinde kwa vyovyote vile. Hivyo watoto wengine huona kwamba ni lazima watumie ujanja au wawaumize wachezaji wenzao ili washinde. Ama kweli, mtu hahitaji kutumia njia hizo ili ashinde!

Kujifunza Kujidhibiti

Mara nyingi watoto hushindwa kutambua kwamba kuna wakati wa kila jambo. Haiwi rahisi kwao kungojea wanapotaka kitu fulani. Jambo baya hata zaidi ni kwamba wanadamu wana mwelekeo wa kutimiziwa mahitaji yao papo kwa hapo. Vyombo vya habari mara nyingi huwapa watu ujumbe huu: “Jipatie unachokitaka haraka!”

Usiige mwelekeo huo wa kuwaendekeza na kuwaharibu watoto. “Mtu anayeweza kudhibiti hisia zake hutambua kwamba ni muhimu awe na subira,” chasema kitabu The Child and the Machine. “Kujitia nidhamu na kupatana na watu wengine ni dawa muhimu ya kuzuia jeuri ya watoto ndani na nje ya shule.” Biblia inatoa kanuni hii muhimu: “Ambembelezaye mtumwa wake tangu utoto, mwishowe mtumwa huyo atamrithi.” (Mithali 29:21, Biblia Habari Njema) Ingawa mstari huo unazungumzia jinsi ya kuwashughulikia watumishi wachanga, wazazi wengi wameona kwamba kanuni hiyo huwafaidi sana watoto wao.

Mojawapo ya mahitaji muhimu zaidi ya watoto ni “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova,” kama Biblia inavyosema. (Waefeso 6:4) Nidhamu yenye upendo huwasaidia watoto wasitawishe sifa kama vile kujidhibiti na subira. Sifa hizo zitawasaidia wafurahi na kuridhika maishani.

Mambo Yanayotishia Maisha ya Utotoni Yatakapokoma

Hata hivyo huenda ukajiuliza, ‘Je, Mungu mwenye upendo na mwenye hekima ambaye alitoa kanuni hizo alitaka ulimwengu uwe jinsi ulivyo? Je, alitaka watoto walelewe katika mazingira hatari kama haya?’ Unaweza kufarijiwa kufahamu kwamba Yehova Mungu na Mwanaye, Kristo Yesu, wanawapenda sana wanadamu, kutia ndani watoto wa umri wote. Hivi karibuni watawaondoa waovu wote duniani.—Zaburi 37:10, 11.

Je, ungependa kujua jinsi hali zitakavyokuwa wakati huo wenye amani na furaha? Hebu wazia hali hii kama inavyoelezwa kwa njia yenye kuvutia katika Biblia: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.” (Isaya 11:6) Tukiwa katika ulimwengu ambamo maisha ya utotoni yanaharibiwa au kuharakishwa kikatili, inafariji kama nini kujua kwamba Mungu ameahidi wakati ujao mzuri kama huo kwa wanadamu hapa duniani! Ni wazi kwamba Muumba anataka watoto wafurahie maisha yao ya utotoni, na badala ya kuharakishwa, yawe na baraka.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Badala ya kumlemea mtoto wako na matatizo ya kibinafsi, mwendee mtu mwingine mkomavu

[Picha katika ukurasa wa 9]

Watoto wana uhitaji wa kucheza