Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Nina Wazazi Walezi?

Kwa Nini Nina Wazazi Walezi?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Nina Wazazi Walezi?

“Ni kama kuwa na ulemavu wa kudumu. Ni ugonjwa wa moyoni usioweza kuponywa.”—Robert.

NDIVYO alivyosema mtu mmoja aliyechukuliwa na wazazi walezi baada tu ya kuzaliwa. Anaendelea kusema hivi: “Karibu kila siku ya maisha yako unatamani sana kujibiwa maswali kama vile, Familia yangu halisi iko wapi? Wanaishi wapi? Kwa nini waliniacha?”

Chantial, binti ya baba aliyetunzwa na wazazi walezi, anasikitika kwamba hajui babu na nyanya yake. Anasema hivi: “Ninahisi uchungu kwa sababu sina wajomba, shangazi, na binamu.” Si watoto wote waliotunzwa na wazazi walezi huhisi hivyo. Lakini baadhi yao huhisi hivyo. Kwa nini?

Kisababishi cha Uchungu

Mtoto anaweza kuwa na matatizo makubwa ya kihisia akigundua kwamba wazazi waliomzaa wamemwacha. Catrina, aliyechukuliwa na wazazi walezi akiwa mchanga, anasema: “Nilikuwa na uchungu mwingi kwa sababu sikujua kwa nini mama yangu mzazi alinikabidhi kwa wazazi walezi. Nilifikiri kwamba mama yangu aliniacha kwa sababu sikuwa na sura yenye kuvutia na singeweza kupendwa. Laiti angenipa nafasi, ninajua ningeufurahisha moyo wake. Kila mara ninapomfikiria mama yangu mzazi uchungu wangu unaongezeka.”

Uhusiano wa Catrina na wazazi wake walezi ulikumbwa pia na matatizo makubwa. Anasema, “nilihisi kwamba wazazi wangu walezi walinichukua kwa nguvu kutoka kwa mama yangu mzazi. Kwa hiyo niliwakasirikia sana.” Naam, nyakati nyingine mtu hupandwa na hasira kwa sababu ya kukabidhiwa kwa wazazi walezi.

Hasira hiyo yaweza kuwa hatari. Nyakati nyingine, kama kisa cha Catrina kinavyoonyesha, unaweza kukasirika isivyofaa au kuwakasirikia watu wasio na hatia. Biblia inashauri hivi: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Utafanyaje hivyo? Neno la Mungu linasema hivi pia: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.” (Mithali 19:11) Hasira yako inaweza kupoa ukishughulikia hali yako kwa busara. Jinsi gani?

Kurekebisha Maoni Yasiyofaa

Busara inaweza kukusaidia kuchanganua maoni yanayochochea hasira yako. Kwa mfano, ikiwa unatunzwa na wazazi walezi, je, wewe hudhani kwamba wazazi waliokuzaa walikuacha kwa sababu ulikuwa na kasoro? Catrina alifikiri hivyo. Lakini je, ndivyo ilivyo nyakati zote? Huenda usiweze kujua kilichowafanya wazazi wako wakuache, lakini kuna sababu nzuri za kuepuka maoni hayo yasiyofaa. Kwa kawaida, kwa nini wazazi huwaacha watoto wao watunzwe na wazazi walezi? Mara nyingi, wanaona kwamba hawana la kufanya.

Fikiria mfano wa Musa. Simulizi la Biblia katika Kutoka sura ya 2 linasema kwamba Farao wa Misri alipoagiza watoto wote wavulana Waisraeli wauawe, Yokebedi alimficha Musa mwanaye mchanga, kwa miezi mitatu. Mwishowe hangeweza tena kumficha, lakini hangevumilia kumwona mwanaye akiuawa. Kwa hiyo “alipokuwa hawezi kumficha tena, akampatia kisafina cha manyasi akakipaka sifa na lami, akamtia mtoto ndani yake, akakiweka katika majani kando ya mto.”—Kutoka 2:3.

Bila shaka haikuwa rahisi kwake kumwacha mtoto wake kwa njia hiyo. Lakini hakuwa na la kufanya. Alimpenda mtoto wake sana hivi kwamba alifanya jambo alilofikiri lingemwokoa. Bintiye alisimama karibu na kumchunga nduguye mchanga hadi alipochukuliwa. Huenda mama yake mwenye wasiwasi alimwomba afanye hivyo.

Bila shaka, si wote wanaowaacha watoto wao mikononi mwa walezi hufanya hivyo kwa sababu ya hali za dharura kama hizo, lakini mara nyingi wanakuwa na makusudi yaleyale. Robert asema: “Nilizaliwa nje ya ndoa. Ingekuwa vigumu sana kwa wazazi wa mama yangu kunilea kwa sababu walikuwa na watoto wengine. Huenda mama yangu alifikiri kwamba ningekuwa na maisha bora kama ningechukuliwa na wazazi walezi.”

Kwa kweli, kuna sababu nyingi zinazofanya watoto wapelekwe kwenye familia nyingine ili kutunzwa. Lakini kama mifano hiyo inavyoonyesha, si lazima iwe ni kwa sababu mama anamchukia mtoto wake au mtoto ana kasoro. Mara nyingi, mama huamini kabisa kwamba mtoto wake atakuwa na maisha bora akitunzwa na familia nyingine.

Umuhimu wa Kupendwa

Busara inaweza kukusaidia unapofikiria sababu zilizofanya wazazi wakuache. Mfikirie tena Musa. Baada ya muda, “binti ya Farao alimwokota na kumlea kama mwana wake mwenyewe.” (Matendo 7:21) Ni nini kilichomchochea binti ya Farao amlinde mtoto ambaye alijua alikuwa Mwebrania aliyechukiwa? Biblia inasema, ‘mtoto alikuwa akilia, basi akamhurumia.’ (Kutoka 2:6) Kwa hiyo, Musa alichukuliwa na mlezi kwa sababu alipendwa wala si kwa sababu alichukiwa au kukataliwa.

Watoto wengi wanaotunzwa na wazazi walezi hugundua kwamba wazazi wao halisi hawakuwatupa tu—ingawa kuna visa vingi kama hivyo siku hizi—lakini waliwapeleka kwenye shirika fulani ambalo lingehakikisha kwamba wanatunzwa ifaavyo. Nao walichukuliwa kwa sababu mtu fulani aliwapenda sana hata akajitolea kuwatunza. Je, twaweza kusema hivyo kukuhusu? Kutilia maanani na kuuthamini upendo ambao umeonyeshwa kunaweza kupunguza uchungu wowote ambao huenda ukahisi.

Isitoshe, waweza kupendwa na wengine mbali na familia inayokutunza. Ikiwa wewe ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo, unaweza kunufaika sana kwa kuwa na akina mama, baba, dada, na ndugu wengi wa kiroho ambao wanakupenda. (Marko 10:29-30) Wazee Wakristo wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:2) Usisite kuongea na Wakristo wenzako wakomavu na kuwajulisha mambo yaliyo moyoni na akilini mwako.

Robert anahisi kwamba ni muhimu kuwa na uhusiano mzuri na wengine katika kutaniko la Kikristo. Anakiri hivi: “Bado mimi huhisi upweke. Hata hivyo, upendo ambao ninaonyeshwa na ndugu na dada zangu wa kiroho unapunguza upweke na uchungu ulio moyoni mwangu.”

Unaweza Kufaulu

Kwa hiyo epuka maoni yasiyofaa. Maoni kama vile, huwezi kufaulu maishani kwa sababu ulitunzwa na wazazi walezi. Maoni kama hayo yasiyofaa yanaweza kukuvunja moyo kabisa! (Mithali 24:10) Na isitoshe, si ya kweli hata kidogo.

Kumbuka, Musa alitumia vyema fursa zote alizopata. Biblia inasema: “Kwa sababu hiyo Musa akafunzwa katika hekima yote ya Wamisri. Kwa kweli, yeye alikuwa mwenye nguvu katika maneno na vitendo.” (Matendo 7:22) Na la muhimu zaidi ni kwamba Musa alijifunza maagizo ya kiroho kwa bidii sana hivi kwamba Yehova, Baba yake wa mbinguni, alikuwa halisi kabisa kwake. (Waebrania 11:27) Je, alifaulu maishani?

Baadaye Musa alikuja kuwa kiongozi wa taifa kubwa lenye watu wapatao milioni tatu au zaidi. Akawa nabii, mwamuzi, amiri, mwanahistoria, mpatanishi wa agano la Sheria, na mwandishi wa vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Zaidi ya hayo, kwa kawaida inasemekana kwamba ndiye aliyeandika kitabu cha Ayubu na Zaburi 90. Bila shaka, Musa alifaulu kabisa maishani. Watoto wengi waliotunzwa na wazazi walezi hufaulu vivyo hivyo, na wewe pia unaweza kufaulu.

Robert alifaulu kulea watoto wawili na hivi sasa ni mzee katika kutaniko la Kikristo. Anasema hivi anapokumbuka maisha yake akiwa mtoto aliyetunzwa na wazazi walezi: “Nimejifunza kutofikiria mno mambo nisiyoweza kubadili lakini kuthamini baraka ambazo nimepata.”

Ikiwa sasa unaishi na wazazi walezi au unatunzwa na familia nyingine, huenda mara kwa mara ukasumbuliwa na mawazo yasiyofaa. Lakini jaribu kufikiria mambo yenye kujenga. Andiko la Wafilipi 4:8, 9 linaahidi kwamba ‘Mungu wa amani atakuwa pamoja nawe’ endapo ‘utaendelea kufikiria mambo’ yanayompendeza Mungu. Hata hivyo, ni hatua zipi nyingine zinazofaa ambazo waweza kuchukua ili kufaulu kuishi na wazazi walezi? Makala ya wakati ujao katika mfululizo huu itazungumzia swali hilo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ulichukuliwa na walezi kwa sababu mtu fulani alikupenda sana hata akaamua kuishi nawe na kukutunza